WAZIRI MKUU KUTOA MIZINGA 25 KWA KIKUNDI CHA SANAA
WAZIRI
 MKUU Mizengo Pinda ameahidi kutoa mizinga ya nyuki 25 ya kisasa na ya 
kibiashara kwa ajili ya kikundi cha sanaa cha kata ya Mamba wilayani 
Mlele mkoani Katavi ili waweze kuzalisha mali na kujiendesha wenyewe.
Alitoa ahadi hiyo jana jioni 
(Jumatano, Desemba 19, 2012) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya 
Mamba kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya saba ya ziara yake 
jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
“Nitawapa mizinga 25 ya kuanzia 
ili muongeze na ile miwili mliyopewa na Dk. Kikwembe (Mbunge wa Viti 
Maalum mkoa wa Katavi)… nataka ninyi muwe chachu ya mabadiliko hapa 
mamba ili vijana wengine na wazee waige kutoka kwenu,” alisema.
Aliwataka wabadili mtazamo wao 
katika kufuga nyuki kwa kuweka mizinga ardhini au kwenye mabanda badala 
ya kuitundika kwenye miti. “Mnapaswa kufuga kisasa ili muweze kuikagua 
mara kwa mara, sasa ukiitundika juu ya mti utaendaje kuchungulia kama 
nyuki wameingia kwenye mzinga au la? Utajuaje kama masega yaliyomo yana 
asali ya kutosha? Alihoji.
Alisema wanapaswa watambue kwamba nyuki anafugwa kama ilivyo kwa viumbe wengine kama vile kuku, mbuzi, bata au ng’ombe.
“Faida mtakayopata hapa ni kuwa 
karibu na msitu wa Lyamba lya Mfipa. Tungeweka mizinga pale chini ya 
msitu  jioni hii, kesho asubuhi mngekuta nyuki wameshaingia na kuanza 
kazi,” aliongeza.
Kesho (Ijumaa, Desemba 21, 2012)
 Waziri Mkuu atakwenda kata ya Usevya ambako atazindua mradi wa umemejua
 kwenye sekondari ya kata ya Usevya na kuhutubia wananchi.
No comments:
Post a Comment