TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Thursday, December 20, 2012

WAZIRI MKUU KUTOA MIZINGA 25 KWA KIKUNDI CHA SANAA
 
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameahidi kutoa mizinga ya nyuki 25 ya kisasa na ya kibiashara kwa ajili ya kikundi cha sanaa cha kata ya Mamba wilayani Mlele mkoani Katavi ili waweze kuzalisha mali na kujiendesha wenyewe.
Alitoa ahadi hiyo jana jioni (Jumatano, Desemba 19, 2012) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mamba kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya saba ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
 
“Nitawapa mizinga 25 ya kuanzia ili muongeze na ile miwili mliyopewa na Dk. Kikwembe (Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Katavi)… nataka ninyi muwe chachu ya mabadiliko hapa mamba ili vijana wengine na wazee waige kutoka kwenu,” alisema.
 
Aliwataka wabadili mtazamo wao katika kufuga nyuki kwa kuweka mizinga ardhini au kwenye mabanda badala ya kuitundika kwenye miti. “Mnapaswa kufuga kisasa ili muweze kuikagua mara kwa mara, sasa ukiitundika juu ya mti utaendaje kuchungulia kama nyuki wameingia kwenye mzinga au la? Utajuaje kama masega yaliyomo yana asali ya kutosha? Alihoji.
 
Alisema wanapaswa watambue kwamba nyuki anafugwa kama ilivyo kwa viumbe wengine kama vile kuku, mbuzi, bata au ng’ombe.
 
“Faida mtakayopata hapa ni kuwa karibu na msitu wa Lyamba lya Mfipa. Tungeweka mizinga pale chini ya msitu  jioni hii, kesho asubuhi mngekuta nyuki wameshaingia na kuanza kazi,” aliongeza.
  
Kesho (Ijumaa, Desemba 21, 2012) Waziri Mkuu atakwenda kata ya Usevya ambako atazindua mradi wa umemejua kwenye sekondari ya kata ya Usevya na kuhutubia wananchi.

No comments:

Post a Comment