SERIKALI YATENGE SH.BILLION MOJA KUJENGE DARAJA LA KAVUU
 SERIKALI
 imetenga kiasi cha sh. bilioni moja kwa ajili ya kazi za awali za 
ujenzi wa daraja la mto Kavuu linalounganisha kata za Mamba, Kasansa, 
Majimoto, na kijiji cha Inyonga yalipo makao makuu ya wilaya mpya ya 
Mlele.
Hayo yamesemwa na Waziri Mkuu 
Mizengo Pinda jana jioni (Jumatano, Desemba 19, 2012) wakati akizungumza
 na wakazi wa kata ya Mamba kwenye uwanja wa mpira akiwa katika siku ya 
saba ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
Waziri Mkuu alisema Serikali ina
 nia ya kufungua mawasiliano kati ya bonde la Rukwa na mikoa ya 
kaskazini ambako kuna uhaba wa chakula. “Bonde hili linasifika kwa 
uzalishaji mkubwa wa nafaka kwa hiyo kujengwa kwa daraja hilo ni 
ukombozi mkubwa wa kufungua soko kwa mazao mnayozalisha huku,” alisema.
Alisema katika mwaka huu wa 
fedha, barabara ya kutoka Sitalike kupitia Kibaoni, Majimoto, Mamba hadi
 Kasansa yenye urefu wa kilomita 33.5 imetengewa sh. milioni 837/- na 
kwamba wakandarasi wawili wamekwishapatikana ili kuifanyia ukarabati 
barabara hiyo.
Kuhusu barabara ya Majimoto hadi
 Inyonga yenye urefu wa kilometa 135, Waziri Mkuu alisema zimetengwa sh.
 milioni 943/- kwa ajili ya ujenzi wa madaraja katika barabara hiyo.
Alipoulizwa kuhusu kuwepo kwa 
fedha hizo, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Katavi, 
Mhandisi Isaack Kamwelwe alimthibitishia Waziri Mkuu kuwepo kwa fedha 
hizo.
“Fedha zimeshatengwa na leo 
nimepokea kibali cha kutangaza zabuni za ujenzi wa daraja hilo. Zabuni 
zitatangazwa kuanzia Januari 2013,” alisema.
Kutokuwepo kwa daraja la Kavuu 
kunawafanya wakazi waishia bonde la Rukwa (maeneo ya Majimoto na Mamba) 
kila wanapotaka kwenda Inyonga, walazimike kupitia Mpanda yaliko makao 
makuu ya wilaya yao ambako ni zaidi ya kilometa 350.
Kesho (Ijumaa, Desemba 21, 2012)
 Waziri Mkuu atakwenda kata ya Usevya ambako atazindua mradi wa umemejua
 kwenye sekondari ya kata ya Usevya na kuhutubia wananchi.
No comments:
Post a Comment