SHERIA MPYA YA UVUVI NAMBA 7 YA MWAKA 2010 YAJADILIWA ZANZIBAR
NA: RAMADHANI ALI/MAELEZO 
Washiriki wa semina ya Uelewa juu ya Athari za uvuvi 
haramu na udhibiti wake unaotokana na sheria mpya ya uvuvi namba 7 ya mwaka 2010 
wameeleza kutoridhika na ushirikiano mdogo wanaopata kutoka Idara ya 
uvuvi.
Wakitoa michango katika semina  
iliyoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Hoteli ya Zanzibar 
Beach Resort, Mbweni, washiriki hao ambao ni Majaji, mahakimu na waendesha 
mashtaka  wamesema tatizo hilo limepelekea kesi nyingi zinazohusu 
uvuvi haramu  kufutwa kwa kukosa ushahidi.
Wamesema tatizo la  kesi za uvuvi haramu 
zinazopelekwa kwenye vyombo vya sheria ni ushirikiano mdogo unaotolewa na 
 Idara ya Uvuvi kwa wapelelezi, Waendesha Mashtaka na Mahakimu 
wanaosimamia kesi hizo.
Kamanda  wa Polisi Wilaya ya Kusini Unguja 
Jongo Juma Jongo amesema ili kupunguza tatizo la uvuvi harama Zanzibar, Idara ya 
uvuvi inapaswa kuwasaidia wavuvi wadogo wadogo vifaa vya kuvulia ili kuweza 
kuendeleza maisha yao.
Amesema utaratibu wa sasa unaofanywa na Idara hiyo ya 
kutoa zana chache za uvuvi kwa wavuvi wa kijiji kizima hauwezi kuwakomboa wavuvi 
kuacha uvuvi usiotakiwa.
Ameshauri baada ya wavuvi kupatiwa vifaa 
vinavyokubalika,  Idara iweke bandari rasmi kwa ajili ya wavuvi 
kuuza samaki  na wale watakaopatikana na makosa ya kuvua kinyume na 
sheria washughulikiwe.
Akizungumzia sheria mpya ya uvuvi namba 7 ya mwaka 2010, 
Mkurugenzi wa Idara ya uvuvi Mussa Aboud Jumbe amesema lengo ni kuwaongezea 
kipato wavuvi na kulinda rasilimali za baharini kwa ajili ya kizazi cha sasa na 
kizazi kijacho.
Amesema uvuvi wa kutumia baruti, mabomu, sumu ama nyavu 
za macho madogo yanaharibu  mayai ya samaki na samaki wadogo ambao 
hawajafikia kiwango cha kuvuliwa.
Mkurugenzi wa Idara ya uvuvi amewaeleza washiriki wa 
semina hiyo kuwa Serikali inampango wa kuliongeza eneo la Hifadhi ya Ghuba ya 
Menai kutoka bahari ya Mzuri hadi kufikia kijiji cha Bwejuu, Kati Mashariki ya 
kisiwa cha Unguja ambapo vijiji 27 vitaingizwa katika Hifadhi 
hiyo.
Aidha amesema Serikali inafikiria kuligawa eneo la 
Hifadhi ya Kisiwa cha Mnemba na Ghuba ya Chwaka na kuanzisha eneo la hifadhi 
mpya ya Tumbatu.
Mapema akifungua Mkutano huo Waziri wa Mifugo na Uvuvi 
Abdillah Jihad Hassan amesema sheria mpya namba 7 ya mwaka 2010 iliundwa baada 
ya kupata michango ya Kamati za uvuvi za vijiji vyote vya Unguja na 
Pemba.
Amesema sheria hiyo ni mali ya wavuvi wenyewe na hakuna 
sababu ya kwenda kinyume na wanapaswa kuilinda na kuitekeleza kwa 
vitendo.

No comments:
Post a Comment