TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Thursday, December 20, 2012

SHERIA MPYA YA UVUVI NAMBA 7 YA MWAKA 2010 YAJADILIWA ZANZIBAR






















NA: RAMADHANI ALI/MAELEZO 
Washiriki wa semina ya Uelewa juu ya Athari za uvuvi haramu na udhibiti wake unaotokana na sheria mpya ya uvuvi namba 7 ya mwaka 2010 wameeleza kutoridhika na ushirikiano mdogo wanaopata kutoka Idara ya uvuvi.
Wakitoa michango katika semina iliyoandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort, Mbweni, washiriki hao ambao ni Majaji, mahakimu na waendesha mashtaka wamesema tatizo hilo limepelekea kesi nyingi zinazohusu uvuvi haramu kufutwa kwa kukosa ushahidi.
Wamesema tatizo la kesi za uvuvi haramu zinazopelekwa kwenye vyombo vya sheria ni ushirikiano mdogo unaotolewa na Idara ya Uvuvi kwa wapelelezi, Waendesha Mashtaka na Mahakimu wanaosimamia kesi hizo.
Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kusini Unguja Jongo Juma Jongo amesema ili kupunguza tatizo la uvuvi harama Zanzibar, Idara ya uvuvi inapaswa kuwasaidia wavuvi wadogo wadogo vifaa vya kuvulia ili kuweza kuendeleza maisha yao.
Amesema utaratibu wa sasa unaofanywa na Idara hiyo ya kutoa zana chache za uvuvi kwa wavuvi wa kijiji kizima hauwezi kuwakomboa wavuvi kuacha uvuvi usiotakiwa.
Ameshauri baada ya wavuvi kupatiwa vifaa vinavyokubalika, Idara iweke bandari rasmi kwa ajili ya wavuvi kuuza samaki na wale watakaopatikana na makosa ya kuvua kinyume na sheria washughulikiwe.
Akizungumzia sheria mpya ya uvuvi namba 7 ya mwaka 2010, Mkurugenzi wa Idara ya uvuvi Mussa Aboud Jumbe amesema lengo ni kuwaongezea kipato wavuvi na kulinda rasilimali za baharini kwa ajili ya kizazi cha sasa na kizazi kijacho.
Amesema uvuvi wa kutumia baruti, mabomu, sumu ama nyavu za macho madogo yanaharibu mayai ya samaki na samaki wadogo ambao hawajafikia kiwango cha kuvuliwa.
Mkurugenzi wa Idara ya uvuvi amewaeleza washiriki wa semina hiyo kuwa Serikali inampango wa kuliongeza eneo la Hifadhi ya Ghuba ya Menai kutoka bahari ya Mzuri hadi kufikia kijiji cha Bwejuu, Kati Mashariki ya kisiwa cha Unguja ambapo vijiji 27 vitaingizwa katika Hifadhi hiyo.
Aidha amesema Serikali inafikiria kuligawa eneo la Hifadhi ya Kisiwa cha Mnemba na Ghuba ya Chwaka na kuanzisha eneo la hifadhi mpya ya Tumbatu.
Mapema akifungua Mkutano huo Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdillah Jihad Hassan amesema sheria mpya namba 7 ya mwaka 2010 iliundwa baada ya kupata michango ya Kamati za uvuvi za vijiji vyote vya Unguja na Pemba.
Amesema sheria hiyo ni mali ya wavuvi wenyewe na hakuna sababu ya kwenda kinyume na wanapaswa kuilinda na kuitekeleza kwa vitendo.

No comments:

Post a Comment