TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, December 12, 2012

BODI YA CHUO CHA HABARI ZANZIBAR YAZINDULIWA
Picha ya pamoja ya wajumbe wapya wa Bodi hiyo wakiwa na Waziri wa Habari Utamaduni,Utalii na Michezo Saidi Ali Mbarouk.(Picha na Makame Mshenga)

Na: Khadija Khamis – Maelezo Zanzibar

 Waziri wa Habari Utalii Utamaduni na Michezo Said Ali Mbarouk amesema kuwa juhudi na utendaji kazi mzuri wa wajumbe wa Baraza la Chuo cha Uwandishi wa habari Zanzibar ndizo zitakazokipa sifa nzuri na ubora wa hali ya juu Chuo hicho.
 Ameyasema hayo jana huko katika ukumbi wa Chuo cha Habari Vuga mjini Zanzibar wakati akizindua Bodi mpya ya Baraza la Chuo hicho.
 Waziri Mbarouk amesema ubora wa taaluma inayopatikana Chuoni hapo inatokana na juhudi za makusudi ambazo zinapaswa kufanywa na Wajumbe wa Bodi hiyo mpya ambao wana wajibu wa kushauri na kuelekeza namna bora ya kukiendeleza Chuo.
 Amesema kushindwa kuwajibika kwa Bodi hiyo kutakifanya chuo kushindwa kutimiza malengo yake na kuwafanya wahitimu wake kuhitimu bila ya vigezo vinavyokubalika hasa katika kipindi hiki cha ushindani.
 “ Ili twende na wakati uliopo hivi sasa lazima Chuo kitoe wataalamu waliobobea katika fani za habari za kisasa na wenye vipaji vya kuweza kukabiliana na soko la ajira kwa faida yao na Taifa kwa ujumla” Alisema Waziri.
 Waziri huyo aliwataka wajumbe wa bodi hiyo kukikuza na kukiendeleza chuo hicho kwa ufanisi mkubwa ili kuwa mfano wa kuigwa katika vyuo vingine.
 Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina matumani makubwa na Bodi hiyo mpya na kwamba itaweza kukabiliana na changamoto ambazo zinaweza kujitokeza katika kipindi chote cha uwepo wa Bodi hiyo.
 Alizigusia baadhi ya Changamoto zinazokikabili Chuo hicho kuwa ni pamoja na Uhaba wa Madarasa na Ofisi na kuwataka Wajumbe wa Bodi hiyo kufikiria na kupanga namna bora kukukabiliana na jambo hilo.
 Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi hiyo Chande Omar aliishukuru Serikali kwa kuteuliwa na kuahidi kuwa watatekeleza kazi zao ipasavyo kwa mujibu wa sheria zinavyoelekeza.
 Amesema kuwa watajitahidi kufanya kazi kwa mashirikiano ya hali yajuu ili kutimiza malengo ya Chuo kama yalivyopangwa.
 Bodi hiyo iliyoteuliwa ina jumla ya Wajumbe saba ambao ni Saleh Yusuf Mnemo,Salim Said Salim, Ali Nasor Sultan, Najma Khalfani Juma,Yussuf Omar Chunda na Asha Bakari Makame na Mwenyekiti wao Chande Omar Omar.

No comments:

Post a Comment