USWISI SASA KUREJESHA MABILIONI YA MAFISADI
Mbunge wa 
Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (katikati) akiwa na maafisa wa Serikali ya
 Uswiss pamoja na timu uchunguzi kufuatilia mabilioni ya fedha 
zilizowekwa katika benki za nchi hiyo. Picha na Bernhard Reinhold
Sakata la vigogo kuficha mabilioni ya 
shilingi katika benki za Uswisi, limechukua sura mpya baada ya Serikali 
ya nchi hiyo kutunga sheria inayowabana walioweka fedha kwenye benki 
zake kuzithibitisha, la sivyo zitarejeshwa katika nchi husika.Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe alifanya mazungumzo na Serikali ya nchi hiyo ambayo imemweleza kuwa imebadili sheria zake ili kuwadhibiti wageni wanaoficha fedha nchini humo.
Akizungumza na gazeti hili, Zitto alisema amepata taarifa hizo juzi baada ya kukutana na Waziri wa Fedha wa nchi hiyo ambaye alimwandalia mazungumzo na watalaamu wake.
Alibainisha kuwa tangu kuibuka kwa sakata hilo mwaka 2012 na Bunge kuiagiza Serikali kufuatilia, Serikali haijaomba taarifa yeyote kutoka Uswisi kuhusu Watanzania waliohifadhi fedha nchini humo.(P.T)
"Jana nilikutana na Waziri wa Fedha na
 akatuacha na mazungumzo na wataalamu wake. Wamesema hadi sasa, Tanzania
 haijasaini mkataba wa kubadilishana taarifa za kikodi (Multilateral 
convention on administrative assistance in tax matters)," alisema Zitto 
na kuongeza;
"Kwa kutosaini, Tanzania inajinyima 
haki ya kupata taarifa hizi na kutoza kodi kwa watu walioficha fedha 
huku (Uswisi), maana Sheria ya Kodi ya Tanzania inataka kila Mtanzania 
popote anapopata kipato halali lazima alipe kodi."
Zitto alieleza kuwa kitendo cha 
Serikali ya Uswisi kubadili sheria zake, kinaiwezesha nchi hiyo kutoa 
taarifa za benki za watu walioweka fedha nchini humo wakiwamo 
Watanzania, ambao sasa watatakiwa kuthibitisha kama fedha hizo ni safi 
au la.
"Kiufupi, Tanzania haijaomba taarifa 
yeyote kutoka Uswisi. Ila Uswisi wamebadili sheria yao na sasa mmiliki 
wa fedha ndiyo anapaswa kuthibitisha kwamba ni safi, na ikithibitika 
kuwa hazina mwenyewe wala maelezo, zitarudishwa nchi husika," alisema.
Zitto alisema mbali na kukutana na 
watendaji hao wa Serikali amezungumza na Umoja wa Mabenki wa nchi hiyo 
uliobainisha kuwa Uswisi ina Watanzania wachache wenye fedha.
"Wamesema Watanzania wengi wana fedha 
Uingereza, Jersey, Cayman Islands na Mauritius. Dubai pia imetajwa 
sana," alisema Zitto. Zitto alielezea kuwa umoja huo wa benki za Uswisi 
umeanzisha mkakati wa kusafisha fedha uitwao 'clean money strategy', na 
wamegundua watu wengi ambao ni wanasiasa, wamezuia akaunti zao na 
kupeleka majina kwenye Serikali zao.
"Tanzania haijafanya maombi rasmi hapa
 Uswisi na hivyo wao kama benki hawawezi tu kutoa taarifa bila kuombwa. 
Sheria yao imerekebishwa ambapo sasa ni wajibu wa mwenye akaunti kusema 
kama fedha zake ni halali au hapana," alisema Zitto na kuongeza.
Hivi sasa hawapokei pesa kutoka nchi 
za Afrika au wanapokea kwa tahadhari sana, maana kuna reputational risk 
(kupoteza heshima)," alisema.
Wito wa timu ya uchunguzi
Zitto alipendekeza timu iliyoundwa 
kuchunguza fedha hizo itoe taarifa yake kwenye Mkutano wa Bunge unaoanza
 Oktoba 29, mwaka huu, akieleza kuwa, "Kuendelea kukaa na taarifa, 
kutaongeza tetesi za kweli au za uwongo."
Alisema mpango huo wa kusaka fedha 
zilizofichwa nchini Uswisi, umelenga zile zilizofichwa na watu binafsi 
kutokana na rushwa au kuuza dawa za kulevya na kampuni kubwa za 
kimataifa.
Alibainisha kuwa wengi waliotambulika ni wanasiasa, vigogo wa jeshi na wakuu wa mashirika ya umma na watendaji wa Serikali.
"Katika mabenki ya Uswisi, kuna kiasi 
cha Dola za Marekani 197 milioni. Fedha nyingi zipo katika benki za 
Uingereza na visiwa vyake, Dubai na Mauritius," alisema na kuongeza;
"Wapo watu waliopata fedha kihalali, 
lakini wanaficha fedha hizo na mali zao nje ili kukwepa kodi. Wengi wa 
hao ni wafanyabiashara wakubwa nchini. Tanzania inapoteza Dola za 
Marekani 1.25 bilioni kati ya mwaka 2001 na 2012 kwa njia hizi."
Alibainisha kuwa Tanzania lazima itunge sheria ya kufilisi mali ambazo mtu anashindwa kuthibitisha amezipataje.
"Tayari ninafanyia kazi muswada 
binafsi wa sheria wa kubadilisha sheria ya makosa ya jinai ya mwaka 
1991. Wasaidizi wangu wanafanyia kazi muswada huo ili usomwe kwa mara ya
 kwanza kwenye mkutano wa Bunge unaonza Oktoba 29 na kueleza kuwa sheria
 ya sasa ina upungufu," alisema.
Madai hayo ya Zitto yamekuja ikiwa 
umepita mwaka mmoja tangu Bunge kuipa Serikali muda wa kuchunguza sakata
 la vigogo walioficha mabilioni katika benki za Uswisi.
Zitto ndiye aliibua sakata hilo 
mwishoni mwa mwaka 2012. Kufuatia hoja hiyo, Serikali iliunda timu 
kutokana na Azimio la Bunge lililotolewa mwishoni mwa mwaka jana.
Werema ahoji Mwananchi ni Bunge?
Timu hiyo inaongozwa na Mwanasheria 
Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema ambaye jana baada ya kutafutwa 
na gazeti hili alisema, "Uchunguzi kuhusu walioficha fedha Uswisi bado 
haujakamilika."
Viongozi wengine wanaounda tume hiyo 
ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk
 Edward Hosea, Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Othman Rashid na Gavana 
wa Benki Kuu (BoT), Profesa Benno Ndulu.
Alipoulizwa kama kuna uwezekano wa 
ripoti hiyo kuwekwa wazi katika Mkutano ujao wa Bunge, Werema alisema, 
"Kwa nini, kwani wewe ndiyo Bunge. Uchunguzi bado unaendelea"
Hata hivyo, kwa mujibu wa agizo la 
Bunge, tume hiyo inatakiwa kuwa imekamilisha uchunguzi wake mwezi huu na
 kuwasilisha ripoti yake katika mkutano huo wa Bunge.
Alipoulizwa kuhusu ripoti hiyo, Naibu 
Spika, Job Ndugai alisema, "Wiki ijayo katika kikao cha Kamati ya 
Uongozi, Serikali itatakiwa kutoa taarifa za uchunguzi huo na kama 
haujakamilika kikao hicho kitaamua jambo la kufanya na endapo uchunguzi 
utakuwa umekamilika zitapangwa taratibu za kuiwasilisha ripoti bungeni."
Waziri wa Fedha anena
Chanzo:Mwananchi
Naye Waziri wa Fedha, Dk William 
Mgimwa alisema jana kuwa sheria za kimataifa zipo wazi kwamba fedha 
chafu zinazogundulika kufichwa nchi fulani, hurejeshwa katika Serikali 
ya nchi husika.
"Lengo la sheria hizi za kimataifa ni 
kuhakikisha kuwa fedha za wizi zinazoibwa nchi fulani, haziwezi 
kuhifadhiwa katika nchi nyingine," alisema.
Alipoulizwa kama wizara yake ina 
taarifa zozote kuhusu Watanzania walioficha fedha Uswisi alisema, "Kuna 
Tume iliundwa na Bunge kufuatilia suala hilo nadhani ndiyo itakuwa na 
majibu sahihi."
Uchunguzi wa walioficha mabilioni ya 
Uswisi uliibuka baada ya Benki ya Taifa ya Uswiss (SNB) kutoa taarifa 
mapema Juni 2012 kuhusu raia wa kigeni wanaomiliki akaunti za benki 
nchini humo.
Orodha hiyo inadaiwa kuwa na majina ya
 baadhi ya Watanzania wenye akaunti zinazofikia Dola 196 za Marekani 
milioni ambazo ni sawa na Sh323.4 bilioni

No comments:
Post a Comment