TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, June 18, 2014

TANZANIA YA PILI VITA DHIDI YA RUSHWA


WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Utawala Bora, George Mkuchika amesema Tanzania inashika nafasi ya pili kati ya nchi tano za Shirikisho la Afrika Mashariki katika suala la utawala bora na vita dhidi ya rushwa.
Waziri Mkuchika aliyasema hayo wakati akizindua Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma iliyoanza jana kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.
Alisema tangu Serikali ya Awamu ya Kwanza, Serikali ya Tanzania ilitangaza vita dhidi ya rushwa na imekuwa ikiimarisha mapambano dhidi ya adui huyo hadi katika Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete.
“Katika nchi za Afrika Mashariki suala la utawala bora na vita dhidi ya rushwa, Tanzania tunashika nafasi ya pili, Rwanda ni ya kwanza, ya tatu ni Uganda na ya nne ni Kenya,” alisema Waziri Mkuchika.
Waziri Mkuchika alikuwa akizungumzia madai yanayotolewa na baadhi ya watu hapa nchini kuwa Serikali ya Tanzania haina dhamira ya kupambana na rushwa.
Alikanusha madai hayo na kusema kuwa Serikali ina dhamira ya kupambana na rushwa ndio maana imepitisha Sheria dhidi ya Rushwa na kuiboresha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ambayo sasa ina matawi kila mkoa na kila wilaya.
Alisema kiashiria kingine cha kuthibitisha kuwa Serikali ya Tanzania inapambana na rushwa ni kufikishwa mahakamani kwa watu wanaotuhumiwa na rushwa.
Hata hivyo, alibainisha kuwa mtumishi wa Takukuru hawezi kuwafikisha watu mahakamani bila ya kupata taarifa kutoka kwa wananchi. Hivyo aliwataka Watanzania wote kutambua kuwa wana wajibu wa kupambana na rushwa kwa kutoa taarifa kwa mamlaka husika ili kufanikisha vita hiyo.
Aliwakumbusha Watanzania kuwa mtumishi yeyote wa umma kumhudumia mwananchi ni haki yake, hivyo mtumishi anayeomba rushwa ili atoe huduma anashiriki katika tendo la rushwa.
Kutokana na hali hiyo, aliwaomba watumishi wajiepushe na rushwa kwani inawanyima watu haki na kwamba kukiwa na malalamiko anayepata haki ni yule anayetoa rushwa. Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka huu inasema
“Mkataba wa Misingi na Kanuni za Utumishi wa Umma Barani Afrika ni Chachu ya Kuimarisha Utawala Bora na Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi.”
CHANZO:HABARILEO

 

No comments:

Post a Comment