TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, June 18, 2014

SERIKALI YASISITIZA KUFUTWA HATI MASHAMBA YA MKONGE


SERIKALI imesisitiza kufuta baadhi ya hati miliki za mashamba ya mkonge katika Mkoa wa Tanga na kugawia wananchi. Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, aliliambia Bunge jana kuwa tayari baadhi ya mashamba yamepelekwa Ofisi ya Rais kwa ajili ya kufutiwa hati miliki.
Chiza pia alisema wakulima wengi wameshindwa kuendeleza mashamba hayo kutokana na kuwapo migogoro kwa wamiliki kutumia mashamba hayo kujipatia mikopo kutoka kwenye benki
Akitoa mfano wa utekelezaji wa hilo, Chiza alisema kuwa serikali imefanikiwa kurejesha mashamba ya Pongwe, na tayari ardhi hiyo imepimwa na kugawiwa kwa wananchi.
“Tunawafuatilia wawekezaji wengine katika sekta ya mkonge ili tujue changamoto zinazowakabili kabla ya kuwanyang’anya na kuwatafuta wawekezaji wengine kwa ajili ya kuendeleza mashamba,” alisema.
Alisema kuna baadhi ya wawekezaji ambao wamechukua mikopo benki kwa kutumia mashamba kama udhamini na wameshindwa kulipa mikopo hiyo, jambo ambalo limelazimisha benki kushikilia hati miliki.
Chiza alielezea uamuzi wa kubinafsisha mashamba makubwa ulifikiwa na serikali kati ya mwaka 1996 na 1999 na kutekelezwa na Tume ya Kurekebisha Mashirika ya Sekta ya Umma (PSRC).
Alisema lengo lilikuwa ni kuinua uzalishaji, lakini baadhi yao wameshindwa na kutolea mfano mashamba ya Marungu, Pongwe, Amboni na Kilimangwido.
Chiza alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Amina Mohamed Mwidau (CUF) aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani na mashamba ya mkonge katika Wilaya ya Tanga na Pangani ambayo hayazalishi tena.
CHANZO:HABARILEO

No comments:

Post a Comment