TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, June 18, 2014

BAJETI KAA LA MOTO BUNGENI 

ChengeBungeni_4fae9.png
KAMATI ya Kudumu ya Bajeti imeonesha wasiwasi kuhusu ongezeko la haraka la deni la taifa na kusema hali hiyo inatishia ukuaji endelevu wa uchumi. Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Andrew Chenge aliliambia Bunge jana, ongezeko la ghafla la deni la taifa kutoka Sh trilioni 23.67 Machi mwaka jana, hadi Sh trilioni 30.56 Machi, mwaka huu, linadhihirisha wasiwasi wa matumizi mabaya ya fedha za umma.
"Ingawa Serikali imesema deni hilo ni himilivu, ongezeko hili la Sh trioni 1.6 kwa mwaka linatia wasiwasi kama ukusanyaji mapato na matumizi vinawiana," alisema Chenge wakati na kushauri pawepo nidhamu katika matumizi ya Serikali.
Chenge ambaye alikuwa akiwasilisha maoni ya Kamati katika kujadili Bajeti Kuu ya Serikali, alisema kumekuwapo ongezeko la deni la ndani ambalo halijajumuishwa katika deni la taifa jambo ambalo linaonesha kuwa deni hilo si himilivu kama ilivyosemwa na Serikali.
Serikali imepanga kutumia Sh trilioni 4.354, ikiwa ni asilimia 21.93 ya bajeti kuu ya Sh trilioni 19.6 kwa mwaka 2014/2015 kwa ajili ya kulipia deni la taifa. Chenge alisema kamati inashawishika kuona kwamba serikali haina ubunifu wa vyanzo vipya vya mapato.
Aidha alisema Serikali imepuuza ushauri wa kamati yake juu ya vyanzo vipya vya mapato yasiyo ya kodi ambayo ni pamoja na uvuvi wa kina kirefu, uwindaji katika vitalu, mazao ya misitu na madini.
Wiki iliyopita, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum aliliambia Bunge kwamba deni la taifa ni himilivu kutokana na tathimini ya madeni (DSA) iliyofanywa mwaka juzi katika kutathimini madeni ya nchi.
Aidha, Kamati imesisitiza kuwapo kwa usimamizi wa matumizi ya fedha za umma. "Pamoja na Serikali kuahidi kuzingatia ushauri wa Kamati, lakini hakuna mabadiliko yoyote na uchambuzi wa Kamati umebaini hakuna mabadiliko katika kudhibiti mapato na matumizi ya fedha za umma," alisema Chenge.
Aidha, Chenge alisema Kamati imebaini kuwapo kwa madeni makubwa kwa baadhi ya wizara na taasisi za umma. Alitoa mfano wa Wizara ya Ujenzi ambayo imekuwa na malimbikizo ya madeni hivyo kulazimu kutumia bajeti kulipia madeni badala ya kutekeleza miradi iliyoidhinishwa kwa mwaka husika.
Kamati pia imeishauri Serikali kuagiza maofisa Maduhuli wote nchini kulipa madai ya wazabuni kwa wakati kuepushia Serikali malimbikizo ya madeni na kusababisha hasara kwa makandarasi na uwezo wa makandarasi.
Nidhamu ya matumizi Waziri Kivuli wa Wizara ya Fedha, James Mbatia ametaka Serikali kutunga Sheria ya Bajeti kudhibiti ukopaji na matumizi ya Serikali na kupendekeza kuwa mikopo yote ya serikali ipitie bungeni kabla ya kukopa ili kujadili na kuridhiwa.
Ametaka serikali kuonesha nia ya dhati katika nidhamu ya fedha na kupambana na matumizi ya kifahari, ikiwa ni pamoja na matumizi ya magari ghali kwa ajili ya maofisa wake.
Akiwasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani Bungeni kuhusu bajeti ya Serikali ya mwaka 2014/2015, Mbatia pia alionesha wasiwasi wa kambi yake juu ya kuongezeka kwa deni la taifa.
Alisema limefika kiwango ambacho si himilivu tena. " Hali hii ya ongezeko la deni la taifa haijawahi tokea katika historia ya taifa hili," alisema.
Alisema, " Ukuaji wa uchumi ni asilimia sita, wakati deni la taifa linaongezeka kati ya asimilia 15 hadi 30, hivyo bila kuwa na vyanzo vipya vya mapato italeta matatizo katika uchumi."
Katika hatua nyingine, Kambi ya Upinzani imetaka Serikali ieleze kama fedha zilizokopwa ndani ya miaka saba zimetumika katika maendeleo na imechangia kiasi gani katika kuleta maendeleo.
" Kama fedha zilizokopwa ndani ya miaka saba ambazo ni Shilingi trilioni 25, zingeelekezwa kuinua kilimo, basi kila kata hapa nchini ingepata trekta 281 jambo ambalo lingeifanya nchi kuongeza uzalishaji wa chakula," alisema.
Akichangia bajeti hiyo, Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Abdallah Amour (CUF) alipongeza hatua ya Serikali ya kufuta baadhi ya misamaha ya kodi. Alitaka utekelezaji wake ufanywe kwa uangalifu na hatua kwa hatua.
Aidha alitaka Serikali kuwachukulia hatua wanaoibambikia Serikali madeni yasiyohalali.
Amour alitaka kufahamu ni kiasi gani kimepatikana kutokana na mfumo wa kuandika majina kwenye namba za magari.
Alishauri kama mfumo huo haujawa na mafanikio, Serikali iangalie uwezekano wa kupunguza tozo kutoka Sh milioni tano za sasa hadi Sh milioni mbili na pia fursa hiyo itolewe kwa usafiri wa pikipiki.
Naye Mbunge wa Tarime, Nyambari Nyangwine (CCM), alisema kuchelewa kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwamo ujenzi wa barabara imekuwa chanzo cha kuongeza deni la taifa.
Aidha, alisema katika kufikia uchumi wa kati, ni vyema Serikali ikawekeza katika kilimo na Serikali ihusike katika kutafuta masoko ya mazao hayo huku akiishauri Serikali kuhakikisha inakuja na mkakati utakaowafanya Watanzania kufanya kazi na kutoendelea kuwa kwenye vijiwe huku wakiwa walalamikaji.
CHANZO:HABARILEO

No comments:

Post a Comment