RAISI KIKWETE KUFUNGUA MAONYESHO YA KIMATAIFA YA UTALII
RAIS
 Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maonyesho ya 
kimataifa ya utalii yanayojulikana kama Swahili Tuorism Expo 
yanayotarajiwa kufanyika Dar es Salaam Oktoba mwaka huu.
Waziri
 wa Maliasili na Utalii Razaro Nyalandu aliyasema hayo mwishoni mwa wiki
 Dar es Salaam alipozindua rasmi tovuti ya taarifa za maonyesho hayo 
inayojulikana kama Swahili Tourism Expo (S!TE).
Maonyesho
 hayo yatakayohusisha kampuni binafsi, taasisi za kiserikali kama Bodi 
ya Utalii Tanzania (TTB) pamoja na washirika wengine katika sekta hiyo 
yanatarajiwa kufanyika tarehe 1 mpaka 4 Oktoba, mwaka huu katika ukumbi 
wa Mlimani City Dar es Salaam.
Waziri
 Nyalandu alisema maonyesho hayo ni fursa ya kipekee kwa Tanzania 
kupanua wigo wa sekta ya utalii ambapo nchi zote za ukanda wa Afrika 
Mashariki pamoja na Sudan zinatarajiwa kushiriki lakini pia mataifa 
mbalimbali yataalikwa.
Alisema
 tayari 50% ya nafasi za maonyesho zimeshachukuliwa na kwamba mialiko 
kwa mataifa mbalimbali imeshatumwa ambapo ofisi yake itafuatilia kwa 
karibu mialiko hiyo na kuhakikisha nchi nyingi kwa kadri inavyowezekana 
zinashiriki.
“Kutokana
 na ukubwa wa tukio hili Rais Kikwete anatarajiwa kuwa mgeni rasmi 
lakini pamoja na TTB kupewa jukumu la kuratibu pia ofisi yangu itachukua
 jukumu la kipekee  kufuatilia mialiko iliyotumwa nchi mbalimbali 
kuhakikisha zinashiriki,” alisema Waziri.
 
Aliongeza
 kuwa maonyesho hayo yanatarajiwa kuongeza biashara ya kitalii nchini 
ambapo baada ya hapo Tanzania inatarajiwa kupokea watalii zaidi ya 
milioni 2 kwani maonyesho hayo yataitangaza nchi husika kwa kiasi 
kikubwa.
Kwa
 upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TTB, Balozi Charles 
Sanga alisema maonyesho hayo yatakuwa chachu ya kukuza utalii wa ndani 
na kuwajengea tabia watanzania kutembelea vivutio tulivyonavyo.
Alisema
 tumekuwa tukipokea watalii kutoka mataifa mbalimbali kuja kujionea 
utajiri wa maliasili tulizonazo lakini idadi ya watalii wazalendo 
imekuwa ndogo sana ambapo pamoja na mambo mengine muamko na taarifa za 
vivutio hivi zimekuwa haziwafikii na hivyo maonesho hayo yatakuwa chachu
 ya kuongeza idadi ya watalii wa ndani.
“Maonyesho
 kama haya ni maarufu katika nchi za wenzetu na yamekuwa yanawasaidia 
sana katika kukuza sekta zao za utalii hivyo nasi tunaanza na litakuwa 
linafanyika kila mwaka,”
“Kupitia
 maonyesho haya sekta na biashara nyingi za kitalii zitapanuka lakini 
kubwa zaidi tunaamini baada ya hapo watanzania wengi watakuwa na taarifa
 za kutosha kuhusu maliasili tulizonazo na watahamasika na hatimaye 
kuongeza idadi ya watalii wa ndani ya nchi,” alisema Balozi Sanga.
Wizara
 ya Maliasili kupitia TTB imekuwa na mikakati mbalimbali ya kuhakikisha 
sekta ya utalii inakuwa na mchango wa kipekee katika pato la taifa 
ambapo pamoja na maonyesho hayo pia ina mikataba mbalimbali ya matangazo
 na nchi mbalimbali duniani katika kuhakikisha taarifa za vivutio vyetu 
zinawafikia watu wengi zaidi.(A.I)

No comments:
Post a Comment