Viwango vya Fifa vinatupa ukweli tunaouficha
KATIKA 
siku za hivi karibuni vyombo vya habari hasa vya michezo vimepambwa na 
taarifa za Tanzania kupanda viwango vya soka kwa mujibu wa takwimu za 
Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).
Habari 
hizo zimepokewa katika namna nzuri ya kuonyesha kwamba Tanzania imepiga 
hatua na hivyo jambo hilo kuonekana ni la kujivunia.
Si nia 
yetu kubeza wanaojivunia mafanikio hayo kwani ndio ukweli wenyewe hasa 
unapoviangalia viwango hivyo na kuvifananisha na vilivyopita.
Kwa mfano
 takwimu za Fifa za mwezi Septemba, zilionyesha kwamba Tanzania ilikuwa 
ya 115 na takwimu zilizotolewa mwezi huu zinaonyesha kwamba Tanzania 
sasa ni ya 110.
Wengi 
waliopata taarifa hizo walijifariji hasa baada ya kuona Tanzania imepiga
 hatua hiyo na kuizidi hata nchi ya Kenya ambayo kwa mujibu wa viwango 
hivyo inashika nafasi ya 116.(P.T)
Kwa 
kuziangalia takwimu hizo hizo utaona kwamba Kenya imepata pigo kwa 
kuporomoka kutoka nafasi ya 111 iliyokuwa mwezi uliopita hadi kufikia ya
 116 iliyopo sasa.
Hata 
hivyo tungependa kutoa tahadhari kwamba pamoja na hatua tuliyoipiga kwa 
mujibu wa viwango hivyo lakini bado wadau wanatakiwa kuviangalia viwango
 hivyo kwa mapana zaidi jambo ambalo tunaamini litawafanya watafakari 
kwa kina.
Tunasema 
hivyo kwa sababu ukivichambua kwa kina viwango hivyo utaona kama 
Tanzania haijapiga hatua yoyote ya kutisha, badala yake imeendelea 
kupanda na kushuka.
Kuna 
usemi wa siku hizi uliozoeleka wa homa za msimu, si vibaya kulifananisha
 soka la Tanzania na homa za msimu kama utaamua kuvichambua viwango vya 
Fifa.
Unaizungumziaje
 nchi ambayo rekodi zilizotolewa na Fifa mwezi Agosti zilionyesha kwamba
 ilikuwa ya 110, Septemba ikawa ya 115, Oktoba ikarudi nafasi ya 110?
Je ni 
vibaya kuzingatia takwimu hizo na kuliona soka letu kuwa ni mfano wa 
homa za msimu. Hatulisemi hili kwa nia mbaya bali tunachotaka ni kuona 
wadau wanavitumia vizuri viwango hivi kwa kujichambua na si tu kujivunia
 kupanda.
Katika 
kipindi chote cha mwaka huu, wakati pekee ambao Tanzania ilionyesha 
matumaini kwa mujibu wa rekodi za Fifa ni mwezi Julai kwa kushika nafasi
 ya 106 wakati ambao jirani zetu Kenya walishika nafasi ya 95.
Mwezi Juni ripoti zilionyesha kwamba Tanzania ilikuwa ya 113, Mei 122, Aprili 122, Machi 117, Februari 116 na Januari 118.
Kwa 
mantiki hiyo tangu tuuanze mwaka 2014, Tanzania haijawahi kuwa miongoni 
mwa timu 100 bora kwa mujibu wa rekodi za Fifa jambo ambalo linatosha 
kutufanya tuukubali ukweli kwamba soka letu bado.
Katika 
viwango vya Fifa Tanzania mara zote inashindanishwa kati ya nchi 207, 
kati ya nchi hizo Tanzania inazishinda baadhi ya nchi ambazo 
hazijulikani katika ulimwengu wa soka na tuna hakika wapo Watanzania 
ambao hawajawahi hata kuzisikia.
Mfano nchi kama Macau, Anguilla, Bhutan, Visiwa vya Cayman, Visiwa vya Cook, Montserrat, Vanuatu, Guam, Belize na nyinginezo.
Tunachotaka
 kukisisitiza hapa ni kwamba tufurahie kupanda lakini tuukubali ukweli 
kwamba soka letu bado lina kazi ya kufanya ili walau tuwe chini ya timu 
100 bora duniani na tudumu katika nafasi hizo si kupanda na kushuka.
Chanzo:Mwanaspoti
No comments:
Post a Comment