TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, October 27, 2014

Viwango vya Fifa vinatupa ukweli tunaouficha

KATIKA siku za hivi karibuni vyombo vya habari hasa vya michezo vimepambwa na taarifa za Tanzania kupanda viwango vya soka kwa mujibu wa takwimu za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).
Habari hizo zimepokewa katika namna nzuri ya kuonyesha kwamba Tanzania imepiga hatua na hivyo jambo hilo kuonekana ni la kujivunia.
Si nia yetu kubeza wanaojivunia mafanikio hayo kwani ndio ukweli wenyewe hasa unapoviangalia viwango hivyo na kuvifananisha na vilivyopita.
Kwa mfano takwimu za Fifa za mwezi Septemba, zilionyesha kwamba Tanzania ilikuwa ya 115 na takwimu zilizotolewa mwezi huu zinaonyesha kwamba Tanzania sasa ni ya 110.
Wengi waliopata taarifa hizo walijifariji hasa baada ya kuona Tanzania imepiga hatua hiyo na kuizidi hata nchi ya Kenya ambayo kwa mujibu wa viwango hivyo inashika nafasi ya 116.(P.T)
Kwa kuziangalia takwimu hizo hizo utaona kwamba Kenya imepata pigo kwa kuporomoka kutoka nafasi ya 111 iliyokuwa mwezi uliopita hadi kufikia ya 116 iliyopo sasa.
Hata hivyo tungependa kutoa tahadhari kwamba pamoja na hatua tuliyoipiga kwa mujibu wa viwango hivyo lakini bado wadau wanatakiwa kuviangalia viwango hivyo kwa mapana zaidi jambo ambalo tunaamini litawafanya watafakari kwa kina.
Tunasema hivyo kwa sababu ukivichambua kwa kina viwango hivyo utaona kama Tanzania haijapiga hatua yoyote ya kutisha, badala yake imeendelea kupanda na kushuka.
Kuna usemi wa siku hizi uliozoeleka wa homa za msimu, si vibaya kulifananisha soka la Tanzania na homa za msimu kama utaamua kuvichambua viwango vya Fifa.
Unaizungumziaje nchi ambayo rekodi zilizotolewa na Fifa mwezi Agosti zilionyesha kwamba ilikuwa ya 110, Septemba ikawa ya 115, Oktoba ikarudi nafasi ya 110?
Je ni vibaya kuzingatia takwimu hizo na kuliona soka letu kuwa ni mfano wa homa za msimu. Hatulisemi hili kwa nia mbaya bali tunachotaka ni kuona wadau wanavitumia vizuri viwango hivi kwa kujichambua na si tu kujivunia kupanda.
Katika kipindi chote cha mwaka huu, wakati pekee ambao Tanzania ilionyesha matumaini kwa mujibu wa rekodi za Fifa ni mwezi Julai kwa kushika nafasi ya 106 wakati ambao jirani zetu Kenya walishika nafasi ya 95.
Mwezi Juni ripoti zilionyesha kwamba Tanzania ilikuwa ya 113, Mei 122, Aprili 122, Machi 117, Februari 116 na Januari 118.
Kwa mantiki hiyo tangu tuuanze mwaka 2014, Tanzania haijawahi kuwa miongoni mwa timu 100 bora kwa mujibu wa rekodi za Fifa jambo ambalo linatosha kutufanya tuukubali ukweli kwamba soka letu bado.
Katika viwango vya Fifa Tanzania mara zote inashindanishwa kati ya nchi 207, kati ya nchi hizo Tanzania inazishinda baadhi ya nchi ambazo hazijulikani katika ulimwengu wa soka na tuna hakika wapo Watanzania ambao hawajawahi hata kuzisikia.
Mfano nchi kama Macau, Anguilla, Bhutan, Visiwa vya Cayman, Visiwa vya Cook, Montserrat, Vanuatu, Guam, Belize na nyinginezo.
Tunachotaka kukisisitiza hapa ni kwamba tufurahie kupanda lakini tuukubali ukweli kwamba soka letu bado lina kazi ya kufanya ili walau tuwe chini ya timu 100 bora duniani na tudumu katika nafasi hizo si kupanda na kushuka.
Chanzo:Mwanaspoti

No comments:

Post a Comment