TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Tuesday, October 7, 2014

Polisi wachana bango la walimu linalohoji posho Bunge Maalumu 

Wafanyakazi wakiwa na bango wakiingia kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam palipofanyia maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, juzi. Picha na Silvan Kiwale
Maandamano ya walimu kuingia katika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba kuadhimisha Siku ya Walimu Duniani, jana yalipata mtafaruku baada ya polisi kuyaingilia na kuchana bango mojawapo lililohoji posho za wajumbe wa Bunge la Katiba.
Bango hilo la kitambaa cheupe lilikuwa na maandishi yanayohoji posho ya Sh300,000 waliyokuwa wanapata wajumbe wa Bunge la Katiba, yakilinganishwa na kazi kubwa wanayofanya walimu.
Ujumbe wenyewe ulisomeka hivi: "Haki iko wapi usawa uko wapi, posho ya mjumbe wa Bunge la Katiba kwa siku shilingi laki tatu, mshahara wa mwalimu shilingi 370 kwa mwezi. No big results without big salary (Hakuna matokeo makubwa bila mshahara mkubwa)".
Ujumbe huo ulikuwa ukifanya rejea ya viwango vya malipo ya Sh300,000 kwa siku ambazo walikuwa wakilipwa wajumbe wa Bunge Maalumu zikiwa ni Sh230,000 kama posho ya kujikimu na Sh70,000 ambazo ni posho ya vikao.(P.T)
Hata hivyo bango hilo lilichanwa hatua chache kabla ya walimu hao hawajaingia uwanjani humo, ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Mwenyekiti wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), mkoani Kagera Dauda Bilikesi, alisema amesikia habari za bango hilo kuharibiwa lakini akasema asingezungumza kwa kina kuhusu suala hilo kwa kuwa hayo yamepita.
Waibuka na shairi
Muda mfupi baada ya polisi kuharibu bango hilo lisionekane uwanjani, walimu hao walipiga chenga kiana wakaibuka na ujumbe ule ule kwa njia ya shairi.
Kupitia shairi hilo liliposomwa mbele ya Pinda, walimu walihoji ukubwa wa posho za wajumbe wa Bunge la Katiba zikilinganishwa na mshahara wanaopata, hali iliyosababisha umati wa walimu uliokuwa uwanjani hapo kulipuka kwa sauti kubwa za shangwe.
Shairi hilo lililosomwa na Mwalimu Betwel Magoso kutoka Wilaya ya Biharamulo, lilisababisha kuvurugika kwa muda kwa utaratibu uliopangwa kwa mujibu wa ratiba, pale alipohoji wajumbe wa Bunge la Katiba kupata Sh1 milioni kwa siku tatu ambazo ni mkopo wa mwalimu kwa miaka mitatu.
Mwalimu Magoso alimgusa Pinda ambaye kabla ya kuanza hotuba yake alianza kwa kusema kuwa mwalimu huyo alitumia ujanja kufikisha ujumbe wake na kuwa baadhi ya maneno katika shairi lake yalikuwa ni mazito.
Kanuni za mafao zasitishwa
Katika hatua nyingine, Serikali imesitisha matumizi ya kanuni mpya za ukokotoaji mafao ya pensheni ambao umeibua malalamiko kuwa malipo ya mkupuo yalipunguzwa kutoka asilimia hamsini hadi ishirini na tano.
Kanuni hizo ni zile zilizotungwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) na kutangazwa Agosti 6, mwaka huu mjini Dodoma na Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudentia Kabaka.
Tangu kutangazwa kwake kanuni hizo zilizua malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali hususan wafanyakazi ambao walisema kuwa hayalengi kuboresha wala kuhuisha mafao, bali yanapunguza stahili hiyo tofauti na ilivyokuwa mwanzo.
Akihutubia sherehe hizo, Pinda alisema suala hilo linarejeshwa tena serikalini kuangaliwa upya.
"Acha suala hili tulirejeshe serikalini tukalitazame upya kwa sababu halikubaliki na hatuwezi kulishurutisha kwa sababu nyie ndiyo wadau, siyo sisi. Tutawaambia walitazame tena na warudi wawashirikishe vizuri wawaeleze mlikubali au mlikatae," alisema Pinda.
Waziri Mkuu alisema pamoja na kuwa lengo lilikuwa ni kuboresha maisha ya wafanyakazi kwa kuleta mfumo mpya wa ukokotoaji wa mafao ya pensheni, suala hilo lilihitaji ushirikishwaji mpana zaidi ikiwa ni pamoja na wadau wenyewe.
Katika kuunga mkono kilio cha walimu, Pinda alitoa mfano wa wabunge wanaopata mafao yao yote wanapomaliza kipindi cha uwakilishi kwa miaka mitano na kuwa kabla ya hapo mafao hayo yalitolewa baada ya kumaliza miaka kumi, jambo ambalo halikupendelewa na wabunge.
Kauli hiyo ilitokana na risala ya walimu iliyosomwa na Katibu Mkuu wa CWT, Yahya Msulwa aliyesema mabadiliko hayo yamezua manung'uniko makubwa hasa kwa walimu wanaobeba idadi kubwa ya watumishi.
Alisema mfumo wa ukokotoaji wa mafao wa zamani, pamoja na kuwa mishahara yao ni midogo, ulifanya mafao yao ya uzeeni yawe na unafuu kwa kiwango fulani, ikilinganishwa na mfumo mpya ambao ukokotoaji unafanyika kwa kuangalia wastani wa mishahara ya miaka mitatu ya mwisho.
Kabla ya mapendekezo hayo, ukokotoaji wa mafao ulifanyika kwa kuangalia mshahara wa mwisho wa mtumishi na malipo yalitolewa kwa asilimia hamsini ya mafao yote baada ya ukokotoaji kufanyika.
Chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment