TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, March 17, 2014

SERIKALI BADO HAIJATOA SH.143 BIL KIGAMBONI 

Serikali imeingia kwenye lawama ikidaiwa kukwamisha kasi ya ujenzi wa Daraja la Kigamboni kutokana na kushindwa kutoa Sh.143.5 bilioni sawa na asilimia 40 ya fedha za mradi huo hadi kukamilika.
Lawama hizo zimekuja ikiwa miezi 15 imebaki kabla ya muda uliopangwa ujenzi huo kukamilika Juni mwakani.
Kwa upande wake, Serikali imesema haina taarifa ya kusuasua kwa kasi ya ujenzi na kwamba suala la utoaji wa asilimia 40 litatekelezwa kulingana na taratibu.
Mmoja wa wafanyakazi waandamizi wa mradi huo, ambaye hakutaka jina lake kuandikwa kwenye gazeti, alisema kuwa kasi ya ujenzi imepungua kutokana na fedha kidogo zinazotolewa kwa ajili ya uendelezaji.
"Kuna kazi hazijafanyika hivi sasa na zingine zimesimama kabisa," alisema.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Gerson Lwenge alisema hawajapokea malalamiko yoyote kutoka kwa makandarasi kuhusu suala la fedha kuchelewa kutoka serikalini.
"Suala la fedha kuchelewa ni 'logistic' za Serikali na siyo hoja ya msingi sana kama daraja linaendelea kujengwa na hakuna kazi zilizosimama," alisema.
Lwenge alisema kuwa fedha ambazo ni sehemu ya mchango wa Serikali zitapatikana na kuna kila dalili ujenzi ukakamilika kabla ya muda uliopangwa.
Mkuu wa Idara ya Uhusiano Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume alikiri kuwa fedha kutoka serikalini hazijatolewa mpaka sasa.
Alisema fedha za Serikali zinapaswa kutumika kujenga barabara zinazounganisha daraja hilo na maeneo ya Kigamboni kwa upande mmoja na Barabara ya Shimo la Udongo.
"Fedha za Serikali ni kwa ajili ya ujenzi wa barabara zenye urefu kilomita 1.5 kila upande kwa kiwango cha lami, lakini hadi sasa hatufahamu ujenzi wa barabara hizo utaanza lini," alisema.
Aliongeza: "Halitakuwa jambo zuri daraja kukamilika bila barabara hizo kujengwa, kwani hali hiyo inaweza kuchangia msongamano usio wa lazima. Kwanza siyo vizuri kwa daraja lenyewe kuwa na lami, kisha likaunganishwa na barabara za vumbi."
Mradi huo ulizinduliwa Septemba 2012 na unatekelezwa chini ya makandarasi wawili, Kampuni ya China ya Railway Jiangchang (T) Ltd na China Major Bridge.(P.T)

No comments:

Post a Comment