SIMU ZA WATU MILLION 8 KUFUNGIWA

WATUMIAJI
 wa simu wapatao milioni nane wapo hatarini kufungiwa simu zao ifikapo 
mwishoni mwa mwezi huu, Tanzania Daima limebaini.
Tayari 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeziandikia kampuni za simu waraka wa 
kuzitaka zianze kukata kodi mpya ya laini (simu card) mara moja kuanzia 
Julai 30, 2013.(hd)
            
Kwa maana hiyo kila anayemiliki laini 
moja ya simu atakatwa sh 3,000; anayemiliki laini mbili sh 6,000 na 
anayemiliki laini tatu sh 12,000, lengo ni kuhakikisha serikali 
inakusanya sh bilioni 178 zitakazopelekwa kwenye bajeti kuu ya serikali.
Watumiaji wa simu sasa watalazimika kulipia kodi hiyo ya miezi mitatu ya Julai, Agosti na Septemba kwa wakati mmoja.
Bunge 
kupitia Kamati ya Bajeti inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, 
Andrew Chenge (CCM) lilitaka kuwapo kwa kodi hiyo ili kusaidia shughuli 
za bajeti ya Serikali Kuu.
Kupitishwa
 kwa kodi hiyo kuliibua malalamiko ya wanasiasa dhidi ya Chenge 
anayelazimisha kuwapo kwa kodi hiyo, huku akishindwa kuamini kwamba kuna
 Mtanzania anayekosa sh 1,000 kwa mwezi kwa ajili ya laini ya simu.
Malalamiko
 hayo yaliendelea hadi kwa wananchi na baadhi ya wabunge wa Chama cha 
Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) waliotaka posho za wabunge zipunguzwe 
ili kuziba pengo hilo badala ya kuwabebesha wananchi mzigo.
Inadaiwa 
kwamba msimamo wa Chenge unaungwa mkono na Spika wa Bunge, Anne Makinda,
 jambo lililosababisha kutojadiliwa kwa hoja binafsi ya Mbunge wa Kawe, 
Halima Mdee (CHADEMA) iliyohusu kodi hiyo katika mkutano wa Bunge 
lililopita kwa kisingizio cha kukosekana kwa muda wa kufanya hivyo.
Hata 
hivyo, takwimu zilizotolewa na kampuni za simu zinaonyesha kuwa miongoni
 mwa wamiliki wa laini za simu milioni 22; milioni nane wanatumia chini 
ya sh 1,000 kwa mwezi.
Baada ya 
malalamiko hayo, Rais Kikwete alikutana na wadau wa mawasiliano ambao ni
 wamiliki wa kampuni za simu Tanzania (MOAT), Naibu Waziri wa 
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Waziri wa Fedha, 
William Mgimwa, kisha kuwaagiza waiondoe kodi hiyo.
"Rais 
alisema lengo kuu la mkutano huo liwe kupendekeza jinsi ya kuziba pengo 
la sh bilioni 178 zitakazopotea katika bajeti iwapo kodi hiyo itafutwa.
"Alisema 
hawezi kuifuta moja kwa moja kodi hiyo, bila kutafuta njia nyingine za 
kupata fedha kujazia pengo litakalotokeza huku tayari Bunge limezipangia
 matumizi," alinukuliwa Makamba baada ya kikao hicho na rais.
Kwa 
upande wake, rais alikaririwa akiwaambia wadau hao wa mawasiliano 
kwamba: "Nakuombeni kaeni pamoja, wekeni bongo zenu pamoja, wekeni akili
 yenu pamoja tutafute namna gani tutajaza pengo hili la sh bilioni 178 
endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha wananchi mzigo mzito, na
 kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni ngumu."
Licha ya 
agizo hilo la rais kutekelezwa kwa MOAT kutakiwa kuongeza kodi nyingine 
iitwayo 'Excise duty' kutoka asilimia 14 hadi 17 bila kujali kwamba 
katika Bunge la bajeti kodi hiyo iliongezwa kutoka asilimia 12 hadi 
asilimia 14, tozo hiyo ya laini za simu haijaondolewa.
Wachambuzi
 wa masuala ya siasa na mawasiliano walisema kutojadiliwa kwa mabadiliko
 ya kodi hiyo ya simu ni dalili kwamba Waziri wa Fedha amezidiwa nguvu 
na kiti cha spika kinachounga mkono hoja hiyo ya Chenge na kushindwa 
kutekeleza agizo la rais.
Wataalamu
 wa mawasiliano walilieleza gazeti hili kwamba kuongezeka kwa kodi hiyo 
kutaifanya Tanzania kuwa na kiwango cha juu cha kodi kuliko nchi 
nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Ushauri 
wa wataalamu hao ulibainisha kwamba kuongezeka kwa kodi hiyo kunaleta 
nafuu kidogo kuliko ile ya laini za simu inayomuumiza zaidi mwananchi wa
 kawaida:CHANZO TANZANIA DAIMA
No comments:
Post a Comment