Manchester City 4 - 1 Manchester United

*Wachakazwa 4-1 na Manchester City
*Arsenal wafanya kweli, waongoza ligi
*Arsenal wafanya kweli, waongoza ligi
Wakati Arsenal wakishika usukani wa 
Ligi Kuu ya England, Manchester United wameoga kichapo cha mwaka, baada 
ya kuzama 4-1 kwa Manchester City.
Huo ulikuwa mtanange wa kwanza baina ya watani hao wa jadi msimu huu, ambapo wote wanafundishwa na makocha wapya.
Katika dimba la Etihad, Man U chini ya David Moyed hawakuwa na mshambuliaji wao tegemeo, Robin van Persie mwenye maumivu kidogo.(P.T)
Man City chini ya Manuel Pellegrini 
walionekana kujiamini zaidi na kucheza kwa ari tangu mwanzo, na kuwaacha
 washabiki wakiwa na cheko la aina yake mwishoni, huku mmiliki, Sheikh 
Mansour aliyehudhuria akitosheka.
Mabao ya Man City yaliwekwa kimiani na
 Sergio Aguero, Yaya Toure, kabla ya Alvaro Negredo na Samir Nasri. 
Yalikuwa maumivu kwa mabingwa watetezi waliofutwa machozi na mkwaju wa 
adhabu ndogo wa Wayne Rooney.
Mshambuliaji huyo aliepuka kadi mapema
 baada ya rafu mbaya kisha kumpiga mchezaji wa Man City na mpira na 
nyingine kadhaa, lakini hadi mwisho alipata kadi ya njano tu.
Katika mechi ya awali, Arsenal walijipandisha kileleni mwa msimamo wa ligi kwa kuwapiga wagumu wa Stoke City kwa mabao 3-1.
Arsene Wenger alikuwa mwenye furaha, 
baada ya wachezaji wake kufanya kile alichowatuma, mabao yao yote matatu
 yakiandaliwa na mchezaji wake mpya, Mesut Ozil.
Waliopachika mabao wavuni ni Aaron 
Ramsey anayewika sana msimu huu na mabeki wake waliofunga kwa vichwa, 
nahodha Per Mertesacker na Bacary Sagna.
Stoke walionesha kujiandaa vyema kwani
 walisawazisha bao la kwanza kupitia kwa Mmarekani Geoff Cameron, lakini
 Arsenal hawakuwa tayari kukubaliana na sare.
Alimwanzisha kinda Sergre Gnabry 
badala ya Theo Walcott aliyegunduliwa kuwa na matatizo muda mfupi kabla 
ya mechi, na chaguo hilo la Kijerumani lililipa vyema kwa jinsi 
alivyojiamini na kumiliki mpira.
Katika mechi nyingine Tottenham 
Hotspur walipata bao la 'jioni' dhidi ya Cardiff City huko Wales na 
kuibuka na ushindi wa 1-0 ambao ni muhimu kwao.
Swansea nao waliwafunga Crystal Palace mabao 2-0 jijini London.
Kutokana na matokeo ya Jumapili hii na yale ya Jumamosi, Arsenal wanakali kiti cha uongozi, ambapo timu zote zimeshacheza mechi tano.
Kutokana na matokeo ya Jumapili hii na yale ya Jumamosi, Arsenal wanakali kiti cha uongozi, ambapo timu zote zimeshacheza mechi tano.
Arsenal wana pointi 12 sawa na Spurs, 
lakini wanawazidi wapinzani hao wa London Kaskazini kwa tofauti ya bao 
moja tu katika uwiano wao, wakifuatiwa na Man City na Chelsea wote wenye
 pointi 10 kama Liverpool.
Nafasi ya sita inashikwa na Everton kwa pointi zake tisa huku Southampton wakiwafuatia wakiwa na nane.
Man United msimu huu wamejikuta wakiwa nafasi ya nane wakifungana pointi na Swansea, Stoke, Hull na Newcastle.
Aston Villa wanafuatia katika nafasi 
ya 13 wakiwa na pointi sita, nyuma yao wanakuja West Bromwich Albion 
wenye tano sawa na West Ham na Cardiff.
Ukingoni mwa msimamo wanakuja Norwich 
wenye pointi nne sawa na Fulham, lakini nyuma yao wapo Crystal Palace 
wanaoshikilia pointi tatu na walipanda daraja msimu huu tu, na 
wanaozibeba timu zote ni Sunderland wenye pointi moja pekee
No comments:
Post a Comment