OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI YAFUNGUA OFISI 23 KATIKA MIKOA MBALIMBALI

Wakili wa serikali Mkuu, Ofisi ya 
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Bw. Frederick Manyanda (kulia) akieleza kwa
 waandishi wa (hawapo pichani) mkakati wa kuhakikisha kuwa huduma ya 
usimamizi na utoaji wa haki inawafikia wananchi wote kwa karibu kwa 
kufungua ofisi zaidi Mikoani, Katika mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara
 ya Habari(MAELEZO) leo Jijini Dar es Salaam,katikati ni Afisa Habari 
toka ofisi hiyo Bi. Asiatu Msuya na Kulia kushoto ni Afisa Habari wa 
Idara ya Habari Bi. Georgina Misama.(P.T)

Afisa Habari, Ofisi ya Mwanasheria 
Mkuu wa Serikali Bi. Asiatu Msuya (kushoto) akieleza kwa waandishi wa 
Habari (hawapo pichani) kuhusu ufunguaji wa ofisi 23 katika mikoa 
mbalimbali nchini ili kutekeleza Mpango wa kutenganisha Upelelezi na 
uendeshaji wa Mashtaka, wakati wa mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya
 Habari (MAELEZO) leo Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Wakili wa serikali 
Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Frederick Manyanda.
PICHA NA HASSAN SILAYO> MAELEZO
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
OFISI
 YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI YAFUNGUA OFISI 23 KATIKA MIKOA 
MBALIMBALI KUFANIKISHA MPANGO WA UTENGANISHWAJI WA SHUGHULI ZA UPELELEZI
 NA UENDESHAJI WA MASHTAKA NCHINI
______________________________
Utangulizi
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali 
imefanikiwa kufungua Ofisi 23 katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, 
Tanga, Kilimanjaro (Moshi), Arusha, Mwanza, Kagera (Bukoba) Mara 
(Musoma), Shinyanga, Tabora, Singida, Iringa, Mbeya, Mtwara, Lindi, 
Dodoma, Rukwa (Sumbawanga),Ruvuma (Songea), Njombe, 
Manyara,Morogoro,Kigoma,Geita na Pwani. Aidha jumla ya Ofisi mbili (2) 
za zimefunguliwa katika Wilaya za Temeke na Monduli. Kwa mwaka wa fedha 
2012/2013 pekee jumla ya Ofisi tano (5) zimefunguliwa katika mikoa ya 
Pwani, Kigoma, Morogoro, Manyara, Njombe na Geita ikiwemo pia Ofisi 
mbili za Wilaya.
Lengo
Lengo kuanzishwa na kuimarishwa kwa 
Ofisi hizi za Mikoa na Wilaya ni kuhakikisha kuwa huduma ya usimamizi na
 utoaji wa haki inawafikia wananchi wote kwa karibu zaidi. Baadhi ya 
huduma zinazotolewa ni pamoja na kuendesha Mashtaka mahakamani, 
kushughulikia malalamiko na kero za wananchi kuhusiana na kesi za jinai 
na madai zinazowakabili, kutembelea mahabusu na kuratibu upelelezi wa 
kazi za upelelezi wa makosa ya jinai zinazofanywa na vyombo 
pelelezi/chunguzi ikiwemo Polisi, Magereza, Uhamiaji,TAKUKURU.
Utekelezaji wa Mpango wa kutenganisha Upelelezi na Mashtaka nchini
Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria 
Mkuu wa Serikali imeendelea kutekeleza mpango huu wa Utenganishwaji wa 
Upelelezi na Mashtaka kwa mujibu wa Sheria ambapo mfumo wa Sheria ambao 
uliwezesha kutungwa kwa Sheria ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, 2005 na 
Sheria ya Usimamizi wa Uendeshaji Mashtaka nchini, 2008 umeboreshwa; 
pamoja na kuanzishwa kwa Jukwaa la Ki-taifa la Haki-Jinai (National 
Criminal Justice Forum) Desemba 2009 linaloviunganisha pamoja vyombo 
vyote vinavyosimamia utolewaji wa Haki-Jinai nchini;
Serikali pia imeboresha Muundo wa 
Divisheni ya Mashtaka kwa kuweka Sehemu (Section) mahsusi inayosimamia 
utekelezaji wa mchakato wa utenganishaji wa kazi za upelelezi na 
Mashtaka na uratibu wa kazi za ki-pelelezi; pamoja na kuanzishwa kwa 
huduma ya Mashtaka ya moja kwa moja ambako Mawakili wa Serikali 
wanaendesha kesi; Hii imepelekea idadi ya kesi zinazofunguliwa 
Mahakamani ambako Mawakili wa Serikali wanaendesha Mashtaka kupungua 
ikilinganishwa na kipindi cha nyuma; Kuongezeka kwa ubora wa huduma 
zitolewazo na kupungua kwa kesi za kubambikizwa.
Utekelezaji wa Programu ya 
Utenganishwaji wa Mashtaka na Upelelezi (Civilianization) imetoa msukumo
 mkubwa kwa Ofisi kuingia uanachama na makubaliano ya mashirikiano na 
vyama vinavyohusiana na kazi za Uendeshaji Mashtaka duniani, kama 
vile-IAP, HOPAC, APA, EAAP, na ARINSA; Serikali itaendelea kupanua wigo 
wa uendeshaji wa Mashtaka kwa kuanzisha na kuimarisha Ofisi katika 
Wilaya zote nchini pamoja na Mikoa miwili iliyobaki ya Katavi na Simiyu.
Tunapenda kuwakumbusha Wadau wetu wote
 na Wananchi kwa ujumla kuwa mstari wa mbele katika kutoa taarifa za 
uhalifu au jinai yoyote katika jamii kwa vyombo husika kupitia utaratibu
 unaofaa; na kutoa ushahidi Mahakamani pale unapohitajika kwa kuwa hizi 
ni nguzo muhimu katika uendeshaji wa kesi mbalimbali. Aidha tunatoa wito
 kwa umma, wadau wetu na wananchi wote kwa ujumla pamoja na vyombo vya 
habari nchini kufuatilia mtiririko, hoja zinazowalishwa Mahakamani na 
uamuzi uliotolewa na Mahakama katika kesi mbalimbali zinazoendelea kuwa 
na taarifa sahihi ya kuhusu kesi hizo.
Imetolewa Na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
Ijumaa, Septemba 27, 2013
Kwa mawasiliano zaidi
OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI
SLP 9050
KIVUKONI FRONT
DAR ES SALAAM
SIMU: +255 22 21181778
NUKUSHI: +255 22 2113236
BARUA PEPE: 
 info@agctz.go.tz
TOVUTI: www.agctz.go.tz
No comments:
Post a Comment