MEMBE:MSIJE DAR WAKATI WA ZIARA YA OBAMA

Rais wa Marekani, Barack Obama
Waziri wa
 Mambo ya Nje, Bernard Membe amewashauri watu walioko mikoani kusitisha 
safari za kuja Dar es Salaam wakati wa ziara ya Rais wa Marekani, 
Barrack Obama kutokana na wingi wa wageni katika jiji hilo. Ugeni huo 
pamoja na ule wa viongozi kumi na moja kutoka nchi mbalimbali duniani 
watakaohudhuria mkutano wa kimataifa wa Smart Partnership 
utakaofunguliwa kesho na Rais Jakaya Kikwete kwenye Ukumbi wa Mikutano 
wa Kimataifa wa Julius Nyerere, umesababisha kuimarishwa kwa ulinzi 
katika maeneo mbalimbali hasa katika hoteli za kitalii ambazo 
zimeanza....
 utaratibu wa upekuzi kwa wageni wake.
Akizungumza na katika mahojiano na Redio ya Clouds jana, Membe alisema jiji limefurika kwa wingi wa wageni.
“Hoteli na nyumba za wageni zimefurika
 wageni na magari mengi yamekodiwa. Kwa ujumla, huduma za kijamii 
zitakuwa shida,” alisema.
Rais Obama na mkewe Michelle 
watawasili nchini Jumatatu na tayari wapambe na maofisa usalama kutokana
 Marekani wameanza kuwasili. Mbali ya ujio huo, wake wa marais kutoka 
nchi 14 za Afrika watakaokutana na Laura Bush, mke wa Rais wa zamani wa 
Marekani, George Bush. Pia Michelle atahudhuria mkutano huo 
utakaofanyika Jumanne na Jumatano ijayo.
“Jiji la Dar es Salaam litakuwa na 
mambo mengi kwa hiyo wale wenye kuja kutaka kustarehe wafute safari 
zao,” alisema na kuongeza: “Kama kuna watu ambao hawapo Dar es Salaam na
 hawana sababu za kuja mjini waache tu mpaka wageni watakapoondoka kwa 
sababu jiji la litakuwa limejaa na baadhi ya barabara zitachukuliwa 
zitumike na wageni hao.”
Alisema katika kipindi cha siku tano 
zijazo, baadhi ya barabara za Jiji la Dar es Salaam zitakuwa na shughuli
 nyingi na nyingine zitalazimika kufungwa. Barabara itakayofungwa ni 
pamoja na ile ya Mwai Kibaki na ile ya Bagamoyo itakuwa na shughuli 
nyingi pia wakati Michelle atakapokwenda Jumba la Makumbusho, Jumanne 
ijayo.
Wasafiri wa mikoani
Wasafiri wa mikoani wataathirika zaidi
 Jumanne ijayo wakati Rais Obama atakapokwenda kutembelea mitambo ya 
kufua umeme ya Kampuni ya Symbion Ubungo.
Kituo hicho kipo Barabara ya Morogoro, ambayo ndiyo inayotumiwa na magari yanayoingia na kutoka mikoani.
Rais Obama atakwenda katika kituo 
hicho yapata saa 4.00 asubuhi na kwa kiasi kikubwa itaathiri magari ya 
usafirishaji wa mizigo na abiria yatakayokuwa yanatoka na kuingia Dar es
 Salaam kabla na wakati huo.
Wengine watakaoathirika ni wakazi wa 
Kimara, Mbezi, Kibamba hadi Kiluvya. Athari nyingine ya usafiri itakuwa 
katikati ya jiji ambako Obama na msafara watakuwa na shughuli nyingi na 
hasa ile ya ufunguzi wa barabara karibu na Ikulu na kukutana na 
wafanyabiashara kwenye Hoteli ya Hyatt Regency, Jumatatu ijayo.
Watumiaji wengine wa barabara 
watakaopata shida ni wale wa Barabara ya Bagamoyo hasa pale Rais Obama 
na mkewe watakapokwenda kuweka mashada ya maua kwenye ubalozi wa zamani 
wa Marekani uliopuliwa na mabomu mwaka 1998.
Ulinzi hoteli za kitalii
Mashushushu wa ndani na nje ya nchi 
wamezingira kwenye hoteli kubwa za Dar es Salaam na walionekana katika 
baadhi ya hoteli hizo, wakiwatumia mbwa maalumu kufanya ukaguzi wa 
chumba hadi chumba.
Tofauti na utaratibu uliozoeleka, 
baadhi ya hoteli zenye hadhi ya nyota tano zimeanza kutumia mitambo 
maalumu ya kompyuta kuwafanyia ukaguzi wageni wote wanaoingia.
Wamchongea JK
Mtandao wa Kutetea Waandishi wa Habari
 Duniani (CPJ), umemwandikia barua Rais Obama ukimtaka kujadiliana kwa 
kina na mwenyeji wake Rais Kikwete wakati wa ziara yake nchini kuhusiana
 na vitendo vya kuuawa na kuteswa kwa waandishi wa habari wa Tanzania.
Katika barua hiyo iliyosainiwa na 
Mtendaji Mkuu wa CPJ, Joel Simon na nakala yake kusambazwa kwa viongozi 
mbalimbali akiwemo Rais Kikwete mwenyewe, mtandao huo ulitolea mfano wa 
kuuawa kwa Mwandishi wa Channel 10, Daudi Mwangozi na Issa Ngumba wa 
Redio Kwizera. Pia kupigwa na kuteswa kwa Mhariri Mtendaji wa Habari 
Corporation, Absalom Kibanda.
Marais waja Smart Partnership
Akizungumzia mkutano wa Smart 
Partnership utakaoanza kesho, Membe alisema utajadili jinsi ya kutumia 
sayansi na teknolojia kukuza uchumi.
Viongozi watakaohudhuria mkutano huo 
ni Waziri Mkuu wa Malayasia, Najib Razak, Rais wa Uganda, Yoweri 
Museveni, Uhuru Kenyetta (Kenya), Boni Yayi (Benin), Ali Omar Bongo 
(Gabon), Ikililou Dhoinine (Comoro), Faure Gnassingbe (Togo), Ernest 
Koroma (Sierra Leone), Blaise Compaore (Burkina Fasso), Mahinda 
Rajapaska (Sri Lanka) na Mfalme wa Swaziland, Mswati II, ambaye 
aliwasili jana. Chanzo: mwananchi
No comments:
Post a Comment