WABUNGE WA TANZANIA NAO WASUSIA KIKAO CHA BUNGE LA AFRIKA MASHARIKI
Kikao cha Bunge la Afrika Mashariki (EALA), jana kilivunjika kwa mara ya pili baada ya Wabunge wa Tanzania, kutoka ndani ya ukumbi wakipinga kanuni kuvunjwa juzi.
Baada ya wabunge wa Tanzania kutoka nje, Spika wa 
Bunge hilo, Margareth Zziwa aliahirisha Bunge kwa dakika 15 ili kuweka 
mambo sawa, lakini jitihada za kuwashawishi ziligonga mwamba na kuamua 
kuahirisha Bunge hadi leo.
Hata hivyo, Mbunge wa Tanzania, Makongoro Nyerere 
hakuungana na wenzake kugoma kwani alibakia ukumbini na kuungana na 
wabunge 32 wa Burundi, Kenya, Uganda na Rwanda.
  
Awali, Mbunge Abdullah Ali Hassan Mwinyi alitoa 
msimamo wa wabunge wa Tanzania kuwa walitoka, kupinga kitendo cha 
wabunge wengine kudharau kiti cha Spika juzi na kutoka nje ili 
kushinikiza hoja yao.
 
Mwinyi alisema ili kushinikiza kuheshimiwa kiti 
cha Spika, wameamua kutoka nje ya ukumbi huo kwa kuonyesha hawaungi 
mkono, tabia ya baadhi ya wabunge kushinikiza hoja zao, kujadiliwa na 
Bunge hata kwa kukiuka kanuni na taratibu.
  
                
              
“Jana(juzi) ilikuwa ni mara ya pili wenzetu, 
kudharau kiti cha Spika na kutaka kutoa hoja na kujadiliwa bila kufuata 
kanuni, sasa tumeona ni vizuri na sisi kwa kupinga kuvunjwa kanuni, 
tutoke ili kuonyesha tunapinga mchezo huu,” alisema Mwinyi.
 
                
              
Mwinyi alisema kitendo cha wabunge wenzao kutoka 
nje ya ukumbi kwa kukataliwa kuvunja taratibu, kinadhalilisha kiti cha 
Spika na hata wabunge wenyewe.
  
                
              
Mbunge mwingine wa Tanzania, Twaha Taslima alisema
 kanuni zipo wazi kuwa kama mbunge ana hoja na kutaka Bunge lijadili 
mambo ambayo si ya dharura ni lazima aiwasilishe saa 24 kabla kwa Spika.
  
                
              
“Sasa jana(juzi), Mbunge wa Kenya, Peter Mathuki 
alitaka hoja yake ya kutaka utaratibu wa kufanyika bunge kwa mzunguko 
ijadiliwe kitu ambacho hakikuwa sahihi,” alisema Taslima.  
Muthuki, juzi aliungwa mkono na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), isipokuwa Tanzania.
                
              
Jana aliwasilisha hoja hiyo kwa kufuata utaratibu lakini haikujadiliwa baada ya wabunge wa Tanzania kutoka nje.
  
                
              
Katika hoja hiyo, msimamo wa wabunge wa Tanzania 
na Kamati ya Uongozi ya Bunge ni kuwa vikao vyote vifanyike katika 
ukumbi wa Bunge, Arusha baada ya kukamilika.
Wabunge wa Tanzania ambao jana walitoka ni Shyrose Bhanji, Profesa Nderakindo Kessy na Taslima. Wabunge wanne hawakuwapo.
  
Kwa mujibu wa kanuni za Bunge hilo, kama wabunge 
watatu wa nchi moja, wakitoka nje kupinga jambo lolote basi kikao 
kinaahirishwa kwa dakika 15 na wasiporejea bunge linaahirishwa.
  
Akizungumzia mgogoro huo, Ofisa Habari wa EALA, 
Bobi Odiko alisema kilichotokea jana si ukiukwaji wa taratibu na 
kuongeza kuwa ana imani mambo yatakuwa sawa na vikao vitaendelea leo kwa
 amani.

No comments:
Post a Comment