MCHAKATO KURA YA MAONI YA KATIBA WAANZA

Historia inatarajia kuandikwa katika 
Mkutano wa 12 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano unaoanza leo, mjini Dodoma
 wakati litakaposafisha njia kwa Watanzania kwa mara ya kwanza, kupiga 
kura ya maoni ya Katiba.Bunge litajadili Muswada wa Sheria ya Kura ya 
Maoni 2013, ambao ndiyo utakaotoa njia kwa Watanzania kuamua Katiba Mpya
 baada ya Bunge la Katiba kumaliza kazi yake.
                        
        
        
        
            
Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Tanzania Bara kupiga kura ya
maoni ya aina yoyote ile tangu Uhuru 
mwaka 1961 na ya pili kwa Zanzibar ambayo ilifanya hivyo kwa mara ya 
kwanza mwaka 2010 kutoa nafasi ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa 
Kitaifa.
Kuelekea mchakato huo wa Katiba Mpya, 
Bunge pia litajadili Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya 
Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013.
Hatua hiyo inatokana na safari ndefu 
ya mchakato wa ukusanyaji wa maoni ya wananchi iliyoanza Aprili 13, 
mwaka jana kwa Rais Jakaya Kikwete kuzindua Tume ya Mabadiliko ya Katiba
 chini ya Jaji Joseph Warioba.
Juni 3, mwaka huu, Jaji Warioba 
alizindua Rasimu ya Katiba baada ya mchakato huo na kuruhusu uundwaji wa
 Mabaraza ya Katiba kwa kutegemea makundi maalumu ambayo mchakato wake 
unamalizika Agosti 31, mwaka huu.
Baada ya hatua hiyo, Bunge 
litapelekewa maboresho ya mapendekezo ya rasimu hiyo na kuyajadili 
ikiwamo kupitisha sheria ya mabadiliko hayo na baadaye kuweka muundo wa 
sheria na muundo wa kupigiwa kura hatua itakayofuata katika Bunge la 
Katiba baadaye Novemba, mwaka huu.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na 
Ofisi ya Bunge, hoja hizo mbili zimetengewa siku tano kuanzia Septemba 9
 hadi 13, mwaka huu na mjadala wa marekebisho hayo unatarajiwa kuchukua 
nafasi hasa kwa wabunge wa pande mbili, CCM cha Chadema juu ya 
kutengeneza muundo.
Chadema, kimeshatoa baadhi ya 
mapendekezo yake katika muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko 
ya Katiba na Kura ya Maoni ikiwamo kupinga Rais kuteua wajumbe wa Bunge 
Maalumu wasiotokana na Bunge na Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
No comments:
Post a Comment