TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Thursday, May 7, 2015

WALINDA AMANI WAWILI WA TANZANIA WAPOTEZA MAISHA DRC. 

 

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ( DRC) Bw. Martin Kobler akiwafariji walinzi wa amani kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania ( JWTZ) wanaohudumu katika Misheni ya MONUSCO ( DRC) kufuatia shambulio lililotokea siku ya Jumanne huko Ben,i Magharibi ya Jimbo la Kivu. Katika shambulio hilo na ambalo limelaaniwa vikali na Katibu Mkuu, Ban Ki Moon, walinzi wawili wamepoteza maisha na wengine 13 wamejeruhiwa.
Na Mwandishi Maalum
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amelaani vikali kuuawa kwa walinzi wawili wa amani kutoka Tanzania wanaohudumu katika Misheni ya Kulinda Amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ( MONUSCO).
Walinzi hao wamepoteza maisha baada ya kushambuliwa na kundi la waasi linalosadikiwa kuwa ni la Allied Democratic Forces ( ADF), shambulio hilo limetokea siku ya jumanne katika eneo la Beni, Magharibi ya Jimbo la Kivu ambapo walinda Amani wengine 13 wamejeruhiwa.
Shambulio hilo limetokea wakati kikosi hicho cha walinzi wa Amani kutoka JWTZ wakielekea kutoa ulinzi kwa wananchi na ndipo waliposhambuliwa.
Walinzi wa Amani waliopoteza maisha ni Private Juma Ally Khamis na Koplo John Leonard Mkude.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa jumanne jioni, inaelezea
masikitiko makubwa ya Katibu Mkuu, Ban ki Moon, kufuatia tukio hilo la kusikitisha na ametoa pole kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na familia za marehemu.
Ban Ki Moon katika salamu zake amesema, walinzi hao wamepoteza maisha yao wakati wakielekea kutoa ulinzi kwa raia kwa mujibu wa mamlaka waliyokabidhiwa na Umoja wa Mataifa, na kusisitiza kwamba suala la kuwalinda raia litaendelea kupewa muhimu kama ilivyoainisha kupitia azimio namba 2211(2015) la Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Aidha taarifa ambazo Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, imezipata kutoka Idara ya Ulinzi wa Amani ya Umoja wa Mataifa ( DPKO) zimetaarifu kwamba walinzi wengine wanne ambao walikuwa hawajulikani walipo wamepatikana wakiwa hai.
Wakati huo huo, Mshauri wa Masuala ya Kijeshi katika Umoja wa Mataifa, Luteni General Magsood Ahmed naye ametoa salamu zake za pole kwa Serikali na familia ya marehemu kufuatia shambulio hilo.
Katika salamu zake kupitia kwa Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Lt. General Ahmed pamoja na kulaani shambuli hilo amesifu na kupongeza namna wanajeshi wa Tanzania wanaolinda Amani kupitia Misheni hiyo ya MONUSCO wanavyotekeleza majukumu yao ya ulinzi kwa weledi mkubwa.
Katika hatua nyingine, Mwakilishi Maalum wa Katibu MKuu katika DRC. Bw. Martin Kobler naye ameelezea kusikitishwa kwake kufuatia shambulio hilo. Na kwamba hatavumilia kuona matukio ya kushambuliwa kwa walinzi wa Amani katika eneo hilo ya Beni yakiendelea.(Muro)

No comments:

Post a Comment