TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, May 18, 2015

17 mahakamani kwa jaribio la kumpindua Nkurunziza 


Jenerali Niyungeko Juvenal (katikati) akipelekwa katika Mahakama Kuu mjini Bujumbura kujibu shtaka la kujaribu kumpindua Rais Pierre Nkurunziza. Picha na AFP.
Bujumbura, Burundi. Maofisa 17 wa Jeshi la Burundi wametiwa mbaroni wakiwamo majenerali watano na kufikishwa mahakamani kwa kosa la kuipindua Serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.
Wanajeshi watatu wametajwa kuwa vinara wa kupanga njama za kuipindua Serikali ya Burundi wakiwamo maofisa wawili wa ngazi za juu wa polisi.
Msemaji wa Ikulu ya Burundi, Gervais Abayeho alisema jana kwamba washtakiwa wengine wanne ni maofisa wenye vyeo vya chini na wanane ni wanajeshi wa kawaida.
Mpaka sasa hakuna taarifa yoyote ya kukamatwa kwa Meja Jenerali Godefroid Niyombare ambaye aliongoza mapinduzi hayo.
Askaribi hao wanatuhumiwa kufanya jaribio la kumpindua Rais Nkurunziza wakipinga uamuzi wake wa kugombea urais kwa muhula wa tatu.
Abayeho alisema wakati maandamano yakiendelea Bujumbura kupinga uamuzi wa Chama cha CNDD-FDD kumteua Nkurunziza kugombea nafasi hiyo kwa mara nyingine, Meja Jenerali Niyombare alitangaza kutomtambua Nkurunziza kama rais wa nchi hiyo. Mawakili wanaowatetea watuhumiwa hao walisema kwamba baada ya wateja wao kukamatwa waliteswa na kuumizwa.
"Wamepigwa na ukiwatazama wamechoka na hawana mashati wala viatu," alisema mmoja wa mawakili wanaowatetea watuhumiwa hao kutoka Kampuni ya Mawakili ya Bar, Miburo Anatole.
Anatole alisema anamwakilisha Meja Jenerali Cyrille Ndayirukiye ambaye alikuwa waziri wa zamani wa ulinzi wa nchi hiyo na maofisa wawili wa polisi.
Wakili mwingine, Cyriaque Nibitegeka alisema mteja wake ambaye ni ofisa wa jeshi la nchi hiyo alilazimishwa kwa mtutu wa bunduki kukiri kwamba alihusika kuipindua nchi hiyo. Alisema mteja huyo amegoma kula tangu walipokamatwa wiki iliyopita.
Taarifa zilieleza kwamba endapo watuhumiwa hao watapatikana na hatia watahukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani.
Ijumaa iliyopita, Nkurunziza alirejea mjini Bujumbura akitokea Tanzania, huku maandamano ya kumpinga yakiendelea.
Licha ya Serikali kuzuia kufanyika kwa maandamano, waandamanaji vikiwamo vyama vya upinzani na wananchi wameapa kuendelea hadi Rais Nkurunziza atakapotangaza kuacha mpango wake wa kugombea tena urais.CHANZO: MWANANCHI (Muro)

No comments:

Post a Comment