TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, June 10, 2015

Mkasa uliompata Rais wa Misri nchini Ujerumani 

Rais wa Misri Abdal-Fattah Al-Sisi
Kisa cha kushangaza na kufadhaisha kimetokea katikati ya wiki iliyopita katika mji mkuu wa Ujerumani, Berlin.
Rais wa Misri, Abd al-Fattah Al-Sisi, alikuwa katika ziara rasmi ya siku tatu ambayo ilizusha mabishano miongoni mwa wanasiasa wa Ujerumani kabla na zaidi wakati ilipokuwa inafanyika.
Wako wale waliosema kwamba licha ya utawala wa Al-Sisi tangu ulipompindua kutoka madarakani na kumtupa gerezani mtangulizi wake, Mohammed Mursi wa Chama cha Udugu wa Kiislamu, umefurutu ada katika kukandamiza haki za binadamu, hata hivyo, ni vizuri kufanya mazungumzo na kiongozi huyo.
Hawa walitoa sababu kuwa Misri ni taifa kubwa la Kiarabu ambalo liko katika eneo tete na lenye ufunguo wa kuyatatua matatizo ya eneo hilo.(P.T)
Lakini kuna wanasiasa wengine waliohoji kwamba madikteta kama huyo wa Misri- aliyewahi kuwa waziri wa ulinzi chini ya Mursi, ni mtu anayekanyaga haki za binadamu na kuwafumba midomo maelfu ya wapinzani wake kwa kuwatia magerezani, hivyo hastahiki kupokelewa Ujerumani.
Spika wa Bunge la Ujerumani, Nobert Lammert, alisema hana nafasi ya kukutana na mkuu huyo wa kutoka Mto Nile. Alimlaumu kwa kwenda kinyume na misingi ya demokrasia na kuthubutu hata kumtia gerezani Spika wa Bunge alilolivunja.
Hata hivyo, Rais wa Ujerumani, Joachim Gauk, alimpokea kwa mazungumzo punde alipowasili, japokuwa mazungumzo yao yanasemekana yalikuwa ya moto. Gauk alimpa mgeni huyo darasa juu ya haki za binadamu na kuheshimu roho za wanadamu.
Japokuwa Serikali ya Ujerumani hapo kabla ilitoa sharti kwamba Kansela Angela Merkel atakuwa tayari tu kukutana na Al-Sisi ikiwa uchaguzi wa Bunge utafanywa huko Misri, hata hivyo, hilo halijatimizwa.
Wakati ulipowadia, Merkel aliamua ni kwa masilahi ya Ujerumani kukutana na mgeni huyo. Misri ina umuhimu wa kijeshi katika eneo lililojaa mizozo, ubavuni mwake ikiwapo Libya ambako huko mifumo ya kidola imesambaratika, na Syria iliyovurugika kutokana na vita vya kienyeji.
Kansela anahisi Misri inaweza kutoa mchango mkubwa katika kupatikana suluhisho la Mashariki ya Kati baina ya Israel na Wapalastina.
Katika mkutano wao wa pamoja na waandishi wa habari, Merkel alitaja kwamba kumekuwako tofauti baina ya misimamo yao. Kwa mfano, Wajerumani hawakubaliani na adhabu ya kifo na inataka kuwapo kwa uhuru kwa dini zote nchini Misri.
Naye Al-Sisi alijinata na kujibu:“ Na sisi tunaishi katika demokrasia na uhuru, lakini tunaishi katika wakati mgumu.“ Alisema hatakubali kuiachia Misri itumbukie katika vita vya kiraia kama vile Syria, Iraq na Yemen, kwa hivyo ataendelea kupambana na wapinzani wake kwa nguvu zake zote.

No comments:

Post a Comment