TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, March 30, 2015

Wabunge wavurugana Mahakama ya Kadhi.. semina-pinda_300_172_4ea8d.jpg

Waziri mkuu Mizengo Peter Pinda
BAADA ya kutokea kutoelewana miongoni mwa wabunge juu ya marekebisho ya muswada wa sheria inayoruhusu kuundwa kwa Mahakama ya Kadhi, Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema kuna haja ya Serikali kutafakari upya kuhusu suala hilo kabla ya kuliwasilisha bungeni.
Akifunga semina ya Wabunge kuhusu muswada huo mjini hapo, Pinda alisema baada ya majadiliano makali ya wabunge na mgawanyiko uliojitokeza miongoni mwa wabunge, alisema wamebaini kuwa Waislamu wenyewe hawana msimamo mmoja kuhusu jambo hilo.
Alisema ni jukumu la Serikali kuhakikisha kuwa watakachokiandaa juu ya muswada huo, kinakubalika na Waislamu wote juu ya uanzishwaji wa mahakama hiyo.
Pinda alisema jambo hilo pamoja na nia yake kuwa njema, Waislamu hawajalielewa na Wakristo nao wana wasiwasi mkubwa hali inayowafanya Serikali kwenda kuliangalia upya.
“Zipo fikra kwamba hata hiki tulichojaribu kufanya hapa wa kuleta muswada huu, sio chenyewe na hatujawafikisha sehemu wanapotaka Waislamu wenyewe na kwamba tulichofanya ni kama kilemba cha ukoka,” alisema Pinda.
Alisema kile ambacho kilipelekwa na serikali bungeni kilitokana na ule mjadala ulioibuka kwenye Bunge Maalumu la Katiba kuhusu kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi na hatimaye kwenye Kamati ya Maridhiano.
Eneo lingine ambalo Waziri Mkuu alisema linafanya Serikali ikalitazame upya suala hilo ni kwamba baadhi ya wabunge wameonesha wasiwasi kuwa kuna ujanja ujanja mwingine nyuma yake kwenye sheria hiyo ambao unahusisha watu kukatwa mikono, hivyo kuibua hofu kwa watu wa imani nyingine.
Nusura warushiane makonde Awali wabunge wakati wanachangia kuhusu muswada huo, walitofautiana kwa kiasi kikubwa hali ambayo ilisababisha almanusura warushiane makonde huku wengine wakiishia kunyosheana vidole, kuzomeana na kupeana mipasho.
Hali hiyo, ilijitokeza baada ya Mbunge wa Kisarawe Seleman Jafo, kutoa maoni yanayotofautiana na wabunge wote walioanza kuchangia ambapo kwa upande wake, alitaka muswada huo uwasilishwe bungeni na maeneo yanayohitaji marekebisho, yarekebishwe.
Wakati akichangia maoni yake hayo, hali ya hewa ilibadilika katika kikao hicho, ambapo wabunge walianza kumzomea na ndipo alipokatisha hoja yake na kuwataka Waislamu wote wabunge wakutane nje baada ya kikao.
Kauli hiyo ilizua mtafaruku na kikao hicho kilisimama kwa muda kurushiana maneno na kuishia kunyosheana vidole hali iliyosababisha polisi wa Usalama kuingia ukumbini humo kwa ajili ya kusimamia amani.
Vurugu hizo zilizosababisha kikao hicho kusimama kwa muda, zilidumu kwa takribani dakika 20 huku Mbunge wa Kasulu Mjini Moses Machali (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Nyamagana Hezekiah Wenje (Chadema), wakisimama na kutaka kurusha ngumi kwa wapinzani wao ambao ni Jafo.
Sakata hilo, lilitatuliwa na Spika wa Bunge, Anne Makinda, aliyewataka wabunge waheshimiane na kujenga utamaduni wa kuvumiliana hata pale mbunge mwingine akitoa hoja isiyopendwa na kusubiri muda wao na wao wajenge hoja.
“Wabunge nawaambieni utani wenu ni mauti yetu sisi, kuna wabunge hapa wanafahamika kwa fujo, Machali na mwenzie Wenje, waacheni wenzenu wazungumze kwanza hoja zao hata kama hamzipendi, kama mtu uvumilivu umemshinda atoke nje,” alisema Makinda.
Awali akizungumza katika semina hiyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alifanunua kuhusu ukweli juu ya kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ya Kadhi, ambapo alibainisha kuwa mahakama hizo hazianzishwi na Serikali bali Waislamu wenyewe na tayari zimeshaanzishwa nchini tangu mwaka 2012.
Alikanusha madai ya baadhi ya watu kuwa Serikali ina mpango wa kuingiza Mahakama hiyo kwenye Katiba.
“Hili halina ukweli na niweke wazi tu kuwa uwezekano wa Mahakama hii kuingia kwenye Katiba haupo, nimekutana na wadau mbalimbali wakiwemo maaskofu na mashehe na nimewafafanulia vizuri tu,” Naye Mtoa Mada katika semina hiyo Jaji wa Mahakama Kuu Dk Robert Makaramba, alisema Tanzania ni moja ya nchi zinazojiendesha bila kufungamana na dini yoyote lakini imekuwa ikisimamia na kulinda haki za waumini wa dini yoyote na kwamba kutungwa kwa Sheria hiyo ni sehemu ya usimamizi wa Serikali kwa Waislamu.
Akifafanua kuhusu muswada huo wa Sheria ya Kiislamu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, alisema muswada huo una vifungu vinne na lengo lake ni kutatua migogoro ya masuala yanayohusu ndoa, mirathi, talaka na wakfu.
Alisema kwa mujibu wa Sheria hiyo, Mufti ndiye atakayechagua makadhi mbalimbali na kutunga kanuni za sheria hiyo, zitakazotumika kusimamia na kuendeshea mashauri mbalimbali katika Mahakama hiyo ya Kadhi. CHANZO: HABARI LEO

No comments:

Post a Comment