Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta Amsimamisha Kazi Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA),Madeni Kipande
Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta amemsimamisha kazi Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Madeni Kipande kutokana na kile kilichoelezwa kuwa uendeshaji mbovu wa utoaji wa zabuni.
Aidha, amemteua Awadhi Massawe kushika wadhifa huo. Kabla ya uteuzi huo, Massawe alikuwa Meneja wa Bandari.
Akizungumza
 na waandishi wa habari, Sitta alisema uamuzi huo umetokana na kuwapo 
malalamiko ya kutofuatwa kwa taratibu za zabuni na ucheleweshaji wa 
barua kwa wanaoshinda.
“Ni
 muhimu sana taratibu zetu za ununuzi katika bandari ziwe wazi na 
ziheshimike duniani kote, maana miradi hii ni mikubwa sana inayopitishwa
 na bodi ya zabuni ya TPA,” alisema.
Sitta
 alisema,  aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Dk Harrison Mwakyembe alianza
 kushughulikia masuala hayo, lakini hayajakaa vizuri. Alisema hakuna 
uwazi na kumekuwa na ubabaishaji mkubwa, ikiwemo kubadilika majina ya 
kamati za kutathmini zabuni.
Wakati huo huo  Sitta ameunda timu ya watu sita itakayochunguza tuhuma za Kipande. Imepewa wiki mbili iwe imefanya kazi hiyo.
Timu
 hiyo itaongozwa na Jaji mstaafu, Augusta Bubeshi na Katibu wake, 
Deogratius Kasinda ambaye ni mtumishi wa Wizara ya Uchukuzi.
Wajumbe
 wengine wa timu hiyo ni Mkurugenzi Mkuu mstaafu wa Mamlaka ya Manunuzi (
 PPRA) Dk Ramadhani Mlinga, Samson Lugigo , Happiness Senkoro na Flavian
 Kinunda ambao walishawahi kushika nyadhifa za juu ndani ya TPA.
“Nimejitahidi
 kuchukua hawa wastaafu kwa sasa hivi hawatafuti cheo chochote, naamini 
watatenda haki, watachunguza tu bila kufanya uonevu,” alisema Sitta.
Waziri
 Sitta alisema bandari ni eneo muhimu, kwani takwimu zinaonesha kwamba 
asilimia 43 ya makusanyo ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), yanatokana
 na kodi ya ushuru wa forodha. Kati ya makusanyo hayo, asilimia 87 
yanakusanywa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Kwa upande wa Kipande,  alisema hawezi kupinga hatua iliyochukuliwa na waziri .
Hata hivyo, alisema anaamini kipindi chote cha uongozi wake, alifanya ambayo yalikuwa sahihi na hana wasiwasi na uamuzi huo.
"Mimi
 sina wasiwasi na hilo sababu huo ni uamuzi wake; lakini nina imani kuwa
 katika bandari hii, nimefanya kile ambacho nilikuwa natakiwa kufanya,  
hivyo sina shaka na hilo," alisema Kipande.
Katika
 hatua nyingine, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za 
Serikali (PAC), Kabwe Zitto ametaka serikali kujenga matangi ya 
kuhifadhia mafuta na kujenga bomba la mafuta kwenda mikoani.
Aidha,
 kamati hiyo imetaka TPA kuangalia uwezekano wa kununua hisa 50 za 
Kampuni ya Kuhifadhi Mafuta (Tiper) imilikiwe kwa asilimia 100 na 
Serikali.
Kuhusu
 ujenzi wa matangi, Zitto alisema hatua ya Serikali kujenga matangi yake
 ya kuhifadhi mafuta, itasaidia kujua kiasi cha mafuta yanayoingia na 
kuweza kukadiria kodi kwa uhakika.
Akitoa
 mfano wa Kenya, alisema Serikali inamiliki matangi ya kuhifadhia 
mafuta,  wanayapima kujua kiasi cha mafuta kilichoingia na kukitoza 
kodi  kabla ya kupelekwa kwenye matangi ya waagizaji.
“
 Walichofanya, wamemtaka kila muagizaji kuwa na flow meter  yake na 
yakitoka kwenye meli yanaingia kwenye matangi ya Serikali na baada ya 
kujua kiasi na kutozwa kodi hupelekwa kwa walionunua,” alisema.
Zitto 
 alisema wakati umefika sasa kwa serikali kujenga mabomba ya 
kusafirishia mafuta na kwa kuanzia yakawa matatu, ambayo yatasaidia 
kuondoa mfumo wa sasa wa kusafirisha kwa magari.
“Linaweza
 kujengwa bomba moja kwenda Mbeya, likawa na matoleo kwa ajili ya mikoa 
ya Morogoro, Iringa na mikoa iliyo jirani, kwa kufanya hivyo tutaondoka 
na hali ya sasa ya kusafirisha mafuta kwa magari,” alisema.
Alisema
 katika kuimarisha reli, ni vyema ukaanzishwa mfumo wa kutoza kodi 
asilimia 1.5 kwa kila bidhaa inayoingia nchini na fedha hizo ziimarishe 
usafiri wa reli.
“Kwa
 sasa asilimia 99 ya mizigo inasafirishwa kwa barabara, hili si jambo 
jema kwa uchumi, najua nikisema hivyo wenye malori watalalamika, lakini 
wanaweza kufanya biashara nyingine,” alisema.
Kwa
 upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa TPA, Awadhi Massawe alisema asilimia 
60 ya mafuta yanayoingia nchini hupitia kwenye boya la Single Buoy 
Mooring (SBM).
Alisema
 wamejipanga kujenga mita ya kisasa ya kupimia mafuta maeneo ya 
Kigamboni huku ile ambayo haitumiki, wamepanga kuiboresha na kuwa ya 
kisasa.
Kuhusu
 maendeleo ya ujenzi wa gati namba 13 na 14 ambazo zabuni  yake iliingia
 utata, Massawe alisema ripoti ya maandishi wataipeleka kwa Kamati hiyo 
ya Bunge ifikapo Machi Mosi mwaka huu.
Pia,
 Massawe alisema hatua ya kitengo cha kupakua kontena kupewa mtu 
binafsi, inawapunguzia mapato na kuwa hiyo ndio sekta ambayo inaingiza 
fedha nyingi.

No comments:
Post a Comment