Watanzania waonywa urais wa fedha, udini

WAZIRI wa
 Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe amewataka 
Watanzania kuwapuuza wanasiasa wenye kutaka kutumia fedha, dini, ukabila
 na aina yoyote ya ubaguzi kujijengea uhalali na kuombea kura katika 
uchaguzi mkuu ujao.
Akifunga 
Mkutano wa Kimataifa wa Utume wa Kanisa la Waadventista Wasabato, Dar es
 Salaam juzi, Membe ameliomba kanisa hilo kuzungumza na vijana wao na 
kuwakumbusha wajibu wao wa kulinda amani na kufanya uchaguzi sahihi na 
kutokubali kutumika.
“Nawasihi
 muwapuuze wanasiasa wenye mwelekeo huo... hawa ni hatari kwa umoja na 
upendo wetu. Tuwachague wale wenye ulimi wa upendo, unyenyekevu, utu na 
amani. Tumwepuke shetani na kazi zake za ufisadi, rushwa na maovu 
mengine,” alisema Membe.
Mkutano 
huo wa kimataifa wa utume maarufu kama ‘Mission Extravaganza’ ulianza 
Jumatano wiki iliyopita katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na 
uliwahusisha waumini wa kanisa hilo kutoka nchi 11 zilizoko katika 
ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, lengo lake likiwa ni kuwaandaa watu 
kiakili, kijamii na kiroho ili waweze kuishi maisha yenye uadilifu.
Zaidi ya 
watu 2,400 walibatizwa katika mkutano huo. Membe alisema mwaka huu, 
licha ya nchi kufanya uchaguzi mkuu lakini pia ina tukio lingine la kura
 ya maoni ya katiba, hivyo akasisitiza waumini wa kanisa hilo kuliweka 
taifa kwenye maombi.
“Nasisitiza hilo kwa kutambua kuwa kipindi kama hiki huja na migongano na mivutano katika nchi zenye demokrasia changa.”
Membe pia
 alitoa rai kwa waumini wa Kanisa hilo la Waadventista Wasabato 
kushiriki kikamilifu katika kutengeneza viongozi bora wa Serikali 
wanaozingatia misingi ya uadilifu, upendo na unyenyekevu.
Membe 
alisema kuwa dini na madhehebu yanayo nafasi kubwa katika kujenga jamii 
yenye maadili na hofu ya Mungu, wakiwemo viongozi na hivyo kusababisha 
taifa kuwa na amani, upendo na mshikamano.
Alieleza 
kuwa kama Waziri wa Mambo ya Nje, amejifunza kuwa diplomasia na hofu ya 
Mungu vikifanya kazi pamoja hakuna changamoto yoyote isiyoweza 
kukabiliwa.
“Dini na 
Diplomasia vinahusiana pale masuala ya amani, ulinzi na usalama 
yanapoguswa. Hivyo nawaomba mshiriki katika kutengeneza viongozi bora 
katika jamii zetu kwa misingi ya uadilifu ambao watasimamia amani na 
kujiepusha na vitendo viovu ikiwemo rushwa,” alisema Membe.
Aidha, 
alilipongeza kanisa hilo kwa kuwa mfano mzuri wa ustahimilivu na 
uvumilivu wa kidini hapa nchini. Alieleza kwamba kamwe hajawahi kusikia 
Kanisa la Waadiventista Wasabato limeingia katika mgogoro na Serikali, 
dhehebu au dini nyingine.
Alisema 
hilo ni funzo kubwa kwa Watanzania, kwamba kutofautiana kiitikadi, 
kidini, kikabila au rangi si sababu tosha ya kuwagombanisha na kuvuruga 
amani ya nchi.
“Nalipongeza
 kanisa lenu kwa kuwa mfano mzuri wa uvumilivu wa kidini na imani, 
mnaendesha mambo yenu kwa uvumilivu mkubwa na kushirikiana na dini zote 
na hili linatufundisha kuwa kutofautiana kwetu sio sababu tosha ya 
kugombana,” alisisitiza Membe.
Membe 
alilihakikishia kanisa hilo dhamira ya Serikali ya kuendelea 
kushirikiana nalo kwa ajili ya ustawi wa nchi na kufafanua kuwa Serikali
 itaendelea kulinda uhuru wa kuabudu kwa dini zote kama inavyoelezwa 
kwenye Katiba ya nchi.
“Serikali
 inao wajibu wa kusaidia dini na madhehebu kufanya kazi kwa uhuru. 
Bahati nzuri Katiba inayopendekezwa imezingatia kulinda uhuru huo hivyo 
tuiunge mkono,” alifafanua Waziri Membe.
Aidha, 
amelisifu kanisa hilo kwa kuanzisha miradi ya huduma zikiwemo Shule 15 
za Sekondari na Msingi, Chuo Kikuu na Hospitali mbili ambavyo vinatoa 
mchango mkubwa kwa serikali na wananchi kwa ujumla.
Awali 
akimkaribisha Waziri Membe kufunga kongamano hilo, Kiongozi Mkuu wa 
Kanisa hilo duniani, Askofu Dk Ted Wilson alisema kuwa anawaombea 
viongozi wa Tanzania waendelee kuwa na maono kwa ajili ya kuwatumikia 
wananchi na kwamba wakimtumaini Mungu atawawezesha kupata maono mapya 
kwa ajili ya kulitumikia Taifa hili.
Kwa 
upande wake, Kiongozi wa Kanisa hilo Kanda ya Afrika Mashariki na Kati, 
Askofu Blasius Luguri aliipongeza Tanzania kwa kudumisha amani ambayo 
imechangia kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa Kongamano hilo 
lililoshirikisha Mataifa zaidi ya 20.
Aidha, 
alimwomba Waziri Membe kufikisha ujumbe kwa Rais Jakaya Kikwete kuwa 
wana imani na Tanzania kuwa ni nchi ya amani, usalama na utulivu.
Kanisa la
 Sabato ni kanisa linalokua duniani likiwa na waumini milioni 307 huku 
waumini milioni 30 wakiwa Afrika na takriban milioni 5 wakiwa Tanzania.CHANZO:HABARI LEO
No comments:
Post a Comment