TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Tuesday, February 24, 2015

SERIKALI YAPATA SH. BILIONI 15 ZA KULIPA MADENI YA MAHINDI 

SERIKALI Serikali imepata mkopo wa sh. bilioni 15 ambazo zitatumika kulipa kiasi cha madeni ya mazao ya nafaka ambayo wakulima wanaidai kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA).
Hayo yamesemwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na wananchi wa Mkoa wa Iringa akiwa kwenye ziara ya kikazi ya kukagua maendeleo katika mkoa huo.
Akizungumza na wananchi mara baada ya kukagua Chama cha Ushirika cha Akiba na Mikopo (SACCOS) cha Mazombe kilichopo Ilula wilayani Kilolo, mwishoni mwa wiki, Waziri Mkuu alisema katika kipindi cha mwezi huu, Serikali imepata mkopo huo kutoka benki ya CRDB ambazo zimesambazwa kwenye mikoa mbalimbali ili kuwalipa wakulima hao.
Alisema hadi kufikia Machi mwaka huu, Serikali itahakikisha inamaliza kulipa madeni kwa wakulima ambao waliuza mazao yao kwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA).
Akifafanua kuhusu mgao wa fedha hizo, Waziri Mkuu alisema kanda ya Arusha wamepata sh. bilioni 1.72/-; kanda ya Dodoma sh. bilioni 2.02/-; kanda ya Kipawa sh. milioni 632.3/-; kanda ya Makambako sh. bilioni 4.58/-; kanda ya Shinyanga sh. milioni 238.85/-; kanda ya Songea sh. bilioni 1.97/- na kanda ya Sumbawanga sh. bilioni 3.82/-.
Alisema fedha hizo zimegawanywa kwenye vituo, vikundi na mawakala na kuongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika itatoa sh. bilioni 15 nyingine ili zigawanywe katika kanda na kumaliza kabisa madeni ya wakulima.
Alitoa ufafanuzi huo baada kutolewa malalamiko kuwa ucheleweshwaji wa malipo hayo kwa wakulima umewafanya baadhi yao washindwe kurejesha mikopo kwenye taasisi za fedha kwa wakati.
Alisema ucheleweshwaji wa malipo hayo ulitokana na ziada ya chakula kwenye msimu wa kilimo wa mwaka 2014 kuongezeka kwa kufikia zaidi ya tani milioni 1.3, ukilinganisha na ziada ya tani 300,000 za msimu uliopita. "Serikali ililazimika kununua mazao ya wakulima zaidi ya malengo yake... matokeo hayo mazuri ya kilimo, yalitokana na msisitizo wa Serikali kuwekeza kwenye pembejeo, mbegu bora pamoja na kuingiza nchini matrekta zaidi ya 1600.
Mapema, akisoma taarifa ya chama hicho mbele ya Waziri Mkuu, Mwenyekiti wa Mazombe SACCOS, Bw. Yohanes Mwemtsi, alisema kucheleweshwa kwa marejesho ya mikopo iliyochukuliwa na wakulima kunazorotesha maendeleo ya SACCOS hiyo kwa kushindwa kujiimarisha kimtaji.
Alisema licha ya changamoto hiyo, chama hicho kimeshatoa mikopo yenye thamani ya sh. bilioni 4.3 kwa wanachama wake zaidi ya 1,300 huku kukiwa na ongezeko la wanachama wapya kwa wastani wa asilimia 10 kila mwaka.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATATU, FEBRUARI 23, 2015

No comments:

Post a Comment