TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, November 24, 2014

Yanga SC yanasa straika aliyewaumbua Zamalek 

YANGA iko kwenye harakati za karibu sana za kumshawishi straika wa Uganda na AS Vital ya DR Congo, Yunus Sentamu atue Jangwani na wakimpata wana imani kwamba watakuwa wamemaliza kazi na tatizo sugu kwenye fowadi yao.
Mchezaji huyo mwenye miaka 20 ndiye mchezaji aliyefunga bao pekee la AS Vital lililoing'oa Zamalek ya Misri jijini Alexandria kwenye mechi ya kufuzu nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kuwaacha Waarabu wengi midomo wazi.
Sentamu pia alifunga moja kati ya mabao mawili walipocheza na CS Sfaxien na kufuzu fainali ya Ligi ya mabingwa Afrika hivikaribuni. Ni miongoni mwa wachezaji wanaothaminiwa sana kwa sasa nchini Uganda kiasi cha kufanya kocha wa nchi hiyo, Sredejovic Milutin 'Micho' awasahau Hamis Kiiza wa Yanga na Emmanuel Okwi wa Simba.
Yanga imeanza kupambana kimyakimya kumpata straika huyo hata kabla ya Kocha Marcio Maximo kusitisha mkataba wa Mbrazil Geilson Santos 'Jaja' na kutangaza kumleta kiungo mkabaji Emerson Rouqe wa Brazil.(P.T)
Straika huyo wa AS Vita yupo katika orodha ya CAF ya wachezaji wanaowania tuzo ya uchezaji bora Afrika kwa upande wa wachezaji wanaocheza ndani.
Habari za ndani ya kamati ya Usajili ya Yanga, zinasema Sentamu ni kati ya washambuliaji wanaotakiwa sana ili kuwa na straika mmoja mkali wa Afrika ambaye ni mtu wa kazi na mwenye uzoefu kuliko kujaribujaribu na kuingia hasara kila mara.
"Viongozi wanafanya kazi ya kutafuta straika wa maana mwenye uwezo wa kufunga ili kuonyesha kwamba bado Afrika ina wachezaji wazuri tofauti na fikra za kocha (Marcio Maximo)," alidokeza kiongozi huyo na kuongeza kwamba endapo huyo akitua huenda safari ikamkumba Hamis Kiiza au wakaachana na Emerson anayekuja nchini kesho Jumanne na Maximo.
Si Yanga pekee wanamtaka mchezaji huyo kwani CS Sfaxien ya Tunisia nao wameingia kwenye kinyang'anyiro lakini Yanga wamegundua kwamba mchezaji huyo ameambiwa kwamba Tanzania kuna fedha na anataka kucheza karibu na nyumbani.
Awali wakati ishu ya Sentamu inaanza, Yanga kulikuwa na malumbano kwenye kamati ya usajili kwani baadhi ya viongozi wanataka kusajili mchezaji kutoka nje ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kutokana na usumbufu wanaoupata kutoka kwao mara kwa mara na kwamba wengi wao wana viwango vinavyofanana na wachezaji wa Tanzania.
Bado Yanga ipo katika kuhakikisha pia inamnasa kiungo mshambuliaji wa Mbeya City, Deus Kaseke ambaye amerudi Mbeya baada ya kutokamilika kwa mazungumzo ya kwanza jijini Dar es Salaam wiki iliyopita.
Ili Sentamu asajiliwe katika kikosi cha Yanga, ni wazi klabu hiyo itabidi iachane na mmoja wa wachezaji wake wa kigeni kati ya Hamis Kiiza (Uganda), Haruna Niyonzima au Mbuyu Twite wote wa Rwanda lakini Kiiza ndiye yupo katika wakati mgumu kwani tayari Maximo anaonekana hamhitaji kikosini mwake.
Chanzo:Mwanaspoti

 

No comments:

Post a Comment