Ujerumani haioni matumaini katika mzozo wa Ukraine

Frank Walter Steinmeier (kushoto) na Sergei Lavrov mjini Moscow
Waziri wa
 mashauri ya kigeni wa Ujerumani Frank Walter Steinmeier alisema Jumanne
 (18.11.2014) haoni sababu za kuwa na matumaini kuhusu mzozo unaoendelea
 Ukraine kutokana na machafuko kuongezeka mashariki mwa nchi hiyo.
Katika 
mkutano na waandishi wa habari pamoja na waziri wa mambo ya kigeni wa 
Urusi Sergei Lavrov hapo jana, Steinmeir alionya kuhusu hali ya kutisha 
inayoendelea nchini Ukraine. Alizitolea mwito pande zote zinazohusika 
katika mzozo wa Ukraine kuuheshimu mkataba wa makubaliano uliofikiwa 
katika mkutano wa mjini Minsk nchini Belarus uliofanyika Septemba 5 
mwaka huu ambao kwa kiwango kikubwa unaonekana kusuasua.(P.T)
Steinmeier
 alisema itakuwa hasara kubwa kuachana na mkataba huo ambao umefaulu 
kusitisha mapigano mengi, lakini umeshindwa kuepusha kuzuka machafuko ya
 hapa na pale katika maeneo muhimu. "Hata kama tuna shaka kama mkataba 
unafanya kazi katika kila kipengele, hata kama tutaripoti vipengele 
muhimu vimekiukwa katika wiki zilizopita, itakuwa hasara kubwa kuukataa 
mkataba huu. Lazima tufanye juhudi kujaribu kutafuta kilichokwenda kombo
 baada ya mkataba kusainiwa ili tuendeleze kazi ya kuvitekeleza 
vipengele hivyo."
Steinmeier
 alikwenda Moscow akitokea Kiev ambako alikutana na waziri mkuu wa 
Ukraine Arseniy Yatsenyuk. Mwanadiplomasia huyo wa Ujerumani alitaka kwa
 haraka kuwekwe eneo lisiloruhusiwa mapigano kati ya majeshi ya serikali
 ya Ukraine na waasi wanaoegemea Urusi mashariki mwa Ukraine kuuokoa 
mkataba wa makubaliano ya kusitisha mapigano.
Waziri wa
 mambo ya kigeni wa Urusi Sergei Lavrov aliunga mkono mwito wa 
Steinmeier na kusisitiza umuhimu wa kuutekeleza kikamilifu mkataba wa 
Minsk. "Lengo kuu ni kuzuia mzozo wa kijeshi kusini mashariki mwa 
Ukraine, kuweka eneo la kuzitenganisha pande mbili na kuondoa silaha 
nzito. Lakini tutatafakari njia za kuleta uthabiti wa muda mrefu Ukraine
 bila kusahau umoja wa taifa, maelewano na maridhiano. Na hatupaswi 
kuyasahau mageuzi ya katiba yaliyosainiwa na Ukraine mjini Geneva Aprili
 17."
Misimamo tofauti yajitokeza
Tofauti 
zilijitokeza kati ya Steinmeier na Lavrov katika mkutano na waandishi wa
 habari huku wote wakionekana kutotulia mara kadhaa. Ingawa viongozi 
wote walisisitiza umuhimu wa mkataba wa Minsk, Lavrov alisema mdahalo 
kati ya pande zinazohasimiana Ukraine unapaswa kuzingatia uchaguzi wa 
Novemba 2 ulioandaliwa na waasi katika maeneo wanayoyadhibiti katika 
hatua ya kukaidi uchaguzi wa bunge uliofanyika siku chache kabla.
Lavrov 
alisema hakuna mbadala wa ushirikiano kati ya Urusi na Umoja wa Ulaya 
akiongeza kuwa Urusi haipaswi kulaumiwa kwa mahusiano mabovu na umoja 
huo kwa sababu ya mzozo wa Ukraine.
Steinmeier
 alikutana pia na rais wa Urusi, Vladimir Putin, lakini ikulu ya Kremlin
 haikutoa maelezo yoyote kuhusu mazungumzo kati ya viongozi hao. Waziri 
Steinmeier ni kiongozi wa kwanza wa ngazi ya juu kutoka Ulaya kuzuru 
Moscow tangu mwezi Julai mwaka huu, katika ishara inayoonyesha namna 
gani uhusiano kati ya mataifa ya magharibi na Urusi ulivyovurugika tangu
 kumalizika kwa vita baridi kutokana na mzozo mashariki mwa Ukraine.
Mwandishi:Josephat Charo/AFPE/RTRE
Mhariri:Daniel Gakuba
Chanzo:DW
No comments:
Post a Comment