MAREKANI YAIWEKA PABAYA TANZANIA YAIITA KITOVU CHA ‘BIASHARA’ YA BINADAMU

Marekani 
imetoa ripoti inayozungumzia usafirishaji wa binadamu ya mwaka 2013, 
huku ikiitaja Tanzania kuwa kinara wa kunyanyasa wasichana, 
kuwatumikisha katika ngono na usafirishaji wa binadamu.
Ripoti 
hiyo iliyotolewa na idara ya nchi hiyo inayohusika na diplomasia (US 
Department of State, Diplomacy in Action), pia inaitaja Tanzania kuwa ni
 kitovu cha njia ya kusafirisha wanawake, watoto na wanaume ambao 
hutumikishwa kwenye kazi za mashambani na biashara ya ngono.(HD)
Ripoti 
hiyo iliyozinduliwa Julai mwaka huu na Waziri wa Mambo ya Nje wa 
Marekani, Seneta John Kerry inaweka bayana kwamba biashara ya 
usafirishaji wa binadamu hufanywa na baadhi ya ndugu na marafiki ambao 
hutoa ahadi kwa wahusika kwamba wanakwenda kuwasomesha au kuwatafutia 
ajira nzuri mijini.
"Unyonyaji
 wa wasichana wadogo na utumikishaji majumbani ndilo tatizo 
linaloongoza, ingawa kesi za watoto kusafirishwa kwa ajili ya biashara 
ya ngono katika mpaka wa Tanzania na Kenya zinaongezeka. Pia, wasichana 
wananyonywa kwenye maeneo ya utalii," inasema sehemu ya ripoti hiyo.
Kwa 
mujibu wa ripoti hiyo, watoto kutoka Burundi na Kenya, watu wazima 
kutoka Bangladesh, Nepal, Yemen na India wanatumikishwa kufanya kazi 
kwenye sekta za kilimo, madini na majumbani nchini Tanzania.
"Baadhi 
ya raia kutoka nchi jirani huingia Tanzania kwa hiari yao, lakini 
hulazimishwa kufanya kazi majumbani kabla ya kupelekwa kutumikishwa 
kwenye biashara ya ngono Afrika Kusini, Ulaya na Mashariki ya Kati," 
inaeleza.
Naibu 
Waziri wa Katiba na Sheria, Angela Kairuki alimtaka mwandishi kumtumia 
ripoti hiyo kwa njia ya baruapepe ili aweze kuisoma na kuitolea maelezo.
Alipotafutwa
 siku ya pili, alisema kuwa ameipokea na kuikabidhi ofisi ya Mkurugenzi 
Mkuu wa Mashtaka (DPP) ili ifanyiwe kazi na baadaye kutoa majibu.
"Ripoti 
niliipata nikaikabidhi ofisi ya DPP kwa kuwa wao ndio wanaoweza kuitolea
 maelezo baada ya kuisoma. Maoni yangu lazima yawe ya kitaalamu siwezi 
kusema bila kupata taarifa kutoka kwao," alisema.
Lawama kwa Serikali
Ripoti 
hiyo inaitupia lawama Tanzania kwa kutokuwa na sheria thabiti za 
kupambana na biashara haramu ya kusafirisha binadamu, huku ikitolea 
mfano namna ilivyoshindwa kuwasaidia raia wake waliokuwa wakinyanyaswa 
nje ya nchi.
"Kamati 
ya Serikali ya kupambana na usafirishaji binadamu, haijachukua hatua za 
kutosha katika kutekeleza mpango mkakati wa kupambana na vitendo hivyo,"
 inaeleza na kuongeza:Serikali imeshindwa kutenga fedha kwa ajili ya 
kuwasaidia waathirika wa usafirishaji wa binadamu kama ambavyo 
inaelekezwa kwenye sheria ya kudhibiti biashara hiyo ya 2008."
Taarifa 
hiyo inaitaka Tanzania kuongeza nguvu katika kutekeleza sheria ya 
kudhibiti biashara ya kusafirisha binadamu ya 2008 kwa kuwakamata na 
kuwashtaki wahusika wote, lakini ikaikosoa kwa kusema inatoa adhabu 
ndogo kwa mtu anayebainika kufanya makosa, ikiwa ni pamoja na kumhukumu 
kwenda jela miaka 10, kulipa faini au vyote viwili kwa pamoja.
"Sheria 
hiyo haifanani na nyingine kama za mtu anayepatikana na kosa la kubaka 
au kufanya kosa jingine la jinai. Mamlaka imesema ina kesi nne 
inazozichunguza, saba zipo mahakamani toka mwaka jana, zikiwepo mbili 
mpya," inasema ripoti.
Pia, 
Serikali ya Tanzania imelaumiwa kwa kushindwa kuripoti maendeleo ya 
uchunguzi wa maofisa wake waliotuhumiwa kujihusisha na biashara ya 
usafirishaji binadamu.
LHRC na TGNP
Mkurugenzi
 wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba 
alisema tatizo la usafirishaji wa binadamu pia linachangiwa na wasichana
 kuwa na tamaa ya maisha mazuri, hivyo kukubali ahadi ambazo hupewa 
kwamba wanapelekwa kusoma, wasifahamu wanarubuniwa.
"Wengi 
wanatamani kwenda 'majuu' wakidhani watapata elimu, lakini baadaye 
wanaingizwa kwenye vitendo vinavyowafedhehesha na kuwafanya wakate tamaa
 kabisa," alisema.
Naye 
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Usu Mallya 
alisema katika siku za karibuni kumekuwa na ongezeko kubwa la vitendo 
vya unyanyasaji dhidi ya wasichana waliochukuliwa vijijini kwenda mijini
 kufanya kazi.
Alisema 
pamoja na tatizo hilo kuongezeka hapa nchini, hakuna tafiti za kutosha 
ambazo zimefanywa na wadau mbalimbali kuonyesha madhara yaliyopatikana 
hadi sasa.
"Katika 
siku za usoni kumekuwa na ongezeko kubwa la vitendo vya kunyimwa 
chakula, kupigwa na kufukuzwa kazi huku wasichana wengine wakitumika 
kwenye biashara ya ngono," alisema na kuongeza:
"Ripoti hii isiishie kwenye makabrasha bali ifanyiwe kazi ili jamii yote ijue kuwa hili ni tatizo."
Ripoti 
hiyo inabainisha kuwa watu 47,000 pekee ndio walioweza kuokolewa mwaka 
jana kutoka kwenye mazingira ya utumikishwaji kati ya milioni 27 waliopo
 katika hali hiyo duniani.Tanzania imetajwa kuwa ni miongoni mwa nchi 44
 ambazo zinajaribu kupambana na biashara hiyo, lakini hali inazidi kuwa 
mbaya zaidi.:CHANZO MWANANCHI
No comments:
Post a Comment