TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, July 17, 2013

JAJI AJITOA KUENDESHA KESI YA MAUAJI YA PADRI MUSHI

Kesi ya mauaji ya Padri Evarist Mushi imechukua sura mpya, kufuatia Jaji wa Mahakama kuu ya Zanzibar, Mkusa Isaac Sepetu kujitoa baada ya upande wa utetezi kuwasilisha ombi la mshatikiwa Omar Mussa Makame kutokuwa na imani naye.

Akisoma uamuzi baada ya kupokea maombi ya upande wa utetezi, ambayo yaliwasilishwa Julai 2 mwaka huu, Jaji Mkusa amesema kwamba uamuzi wa mshtakiwa ni haki yake kwa mujibu wa sheria lakini amesema hakubaliani na hoja zilizotolewa na Wakili Abdallah Juma Mohamed.


Wakili Abdallah Juma Mohamed aliwasilisha hoja tatu, akimtaka Jaji Mkusa ajiondoe katika kesi hiyo, kuutaka upande wa waendesha mashtaka wapewe muda maalum wa kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo na kuwasilisha mahakamani ili kesi hiyo iweze kusikilizwa kwa muda muafaka.

Akitoa uamuzi wake, Jaji Mkusa amesema hoja zote zilizowasilishwa hazina msingi wowote, na 

kinachoonekana kwa upande wa utetezi unajaribu kuiburuza mahakama ikiwemo kuchagua Jaji wa kusikiliza kesi hiyo kwa vile hoja za kumtaka kujiondoa hazikuzingatia mashiko ya kisheria.

Jaji Mkusa amesema suala la mshtakiwa kunyimwa dhamana lipo wazi kwa mujibu wa sheria ambapo makosa ya mauaji hayana dhamana lakini wakili wa utetezi wamekuwa akiwasilisha ombi la kutaka mteja wake aachiwe huru kila wakati kesi inapotajwa wakati jambo hilo limeshatolewa uamuzi zaidi ya mara tatu.

Jaji Mkusa amesema baada ya uamuzi wake wa kujitoa, jalada la kesi hiyo litarudishwa kwa Jaji Mkuu kwa ajili ya taratibu za kupangiwa Jaji mwingine, na kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti mosi mwaka huu.

Mtuhumiwa Omar Mussa Makame anakabiliwa na shtaka la kumuua Padri Evarist Mushi mnamo Febuari 17 mwaka huu katika eneo la Beitrasi kwa kumpiga risasi kinyume na kifungu cha 196 na 197 cha sheria namba 6 ya mwaka 2004 ya mwenendo wa makosa ya jinai ya Zanzibar.

No comments:

Post a Comment