TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, May 14, 2014

WAZIRI AKWEPA HOJA ,AMSHAMBULIA LISSU

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan alikataa kueleza walipo waasisi sita wa Muungano ambao kambi ya upinzani ilidai kuwa waliuawa na kuzikwa handaki moja, badala yake akatumia nafasi hiyo kumshambulia mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akidai hizo ni propaganda na upotoshaji.
Juzi wakati akiwasilisha hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, Lissu aliitaka Serikali kutoa maelezo bungeni kuhusu sababu za kuuawa kwa waasisi sita wa Muungano wa Tangayika na Zanzibar na kuzikwa katika handaki moja visiwani Zanzibar.
Lissu aliwataja waasisi hao kuwa ni Abdalah Kassim Hanga, aliyekuwa waziri mkuu, Abdul Aziz Twalam aliyekuwa Waziri wa Fedha na Abdulaziz na Saleh Akida aliyekuwa mjumbe wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar.(P.T)
Pia aliwataja Othman Shariff, Mdungi Ussi na Jaha Ubwa ambao alisema nao waliuawa na kuzikwa katika handaki moja eneo la Kama nje kidogo ya Zanzibar.
"Tunataka kujua ukweli kama walifanya makosa, walishtakiwa katika mahakama gani iliyowahukumu adhabu ya kifo... tunataka kuambiwa ukweli kwanini mchango wao kuhusu Muungano umefichwa," alisema Lissu juzi.
Lakini alipoulizwa kuhusu madai hayo, Waziri Hassan alionekana kuzigeuza hoja hizo kuwa ni za Lissu pekee badala ya kambi ya upinzani na kumshambulia mbunge huyo akidai kuwa ni mpotoshaji, anayepiga propaganda na mchochezi.
Waziri huyo, ambaye ni Mzanzibari, alisema alipuuza maswali yote kuhusu waasisi hao akisema mbunge huyo wa Chadema alipotoka katika hotuba yake na ndio maana hakutaka kuzungumzia katika majumuisho ya bajeti ya ofisi yake bungeni.
"Yule Lissu sio mkweli na ndio maana sisi tulimpuuza," alisema waziri huyo.
"Hakuna kitu kama hicho na endapo kingekuwepo sisi Serikali tungeshatoa ufafanuzi ili watu wapate kujua ukweli wake," aliongeza Waziri Samia bila kutoa ufafanuzi wa nini kiliwatokea watu hao walioshika nafasi za juu serikalini mara baada ya Mapinduzi na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.
Pamoja na kudai kuwa aliona hoja hizo ni upotoshaji, Waziri huyo, ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa Bunge la Katiba, aliwasihi wabunge wa upinzani kupeleka hoja zao katika Bunge Maalumu la Katiba linalojadili uundwaji wa Katiba Mpya, ambalo pia limetawaliwa na suala la muundo wa Muungano na kero zake.
Waziri Samia alisema hoja hizo zinalenga kuwaaminisha Watanzania mambo ambayo hayapo ili kuwajaza chuki dhidi ya Serikali yao na pia alidai zina uchochezi ndani yake.
Waziri Samia aliwashauri wabunge pamoja na Watanzania kupuuza kauli hizo akidai mbunge huyo hautakii mema Muungano na ndio maana anaibua mambo aliyodai kuwa ni ya uongo na ya uchochezi.

No comments:

Post a Comment