TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Wednesday, May 21, 2014

MAPINDUZI MAKUBWA YA VIWANDA 


WIZARA ya Viwanda na Biashara imewasilisha bungeni bajeti yake inayoonesha mapinduzi makubwa katika viwanda, ikiwamo kuanza kwa miradi ya chuma ya Liganga na Mchuchuma na kiwanda cha kuua viluwiluwi vya mbu waenezao malaria.
Pia kiwanda cha matairi cha General Tyre kinatarajiwa kuanza tena uzalishaji katika mwaka ujao wa fedha. Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda aliwasilisha bajeti yake hiyo bungeni jana.(Martha Magessa)
Dk Kigoda alisema ukuaji wa sekta ya viwanda ni mzuri kwani umeongezeka kutoka asilimia 5.5 mwaka 1998 hadi asilimia 7.7 mwaka 2013, ingawa ukuaji huo uko chini kidogo ukilinganisha na mwaka 2012.
“Ukuaji huu umechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuimarika kwa uzalishaji viwandani, hususani viwanda vya vinywaji, saruji, bidhaa za chuma, na usindikaji wa mazao ya kilimo,” alisema Dk Kigoda.
Kuhusu Liganga na Mchuchuma, alisema katika mwaka 2013/14, utafiti uliofanywa na Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) umethibitisha kuwapo kwa mashapo ya makaa ya mawe ya tani milioni 370 katika eeno la kilometa za mraba 30.
Alisema utafiti huo, pia umethibitisha kuwapo kwa mashapo ya madini ya chuma ya tani milioni 219 katika eneo la kilometa za mraba 10.
“Mpango wa awali ni kuzalisha tani milioni moja za chuma na megawati 600 za umeme. Kiasi hicho cha uzalishaji wa chuma kitaifanya Tanzania kuwa ya tatu barani Afrika katika uzalishaji chuma.
“Aidha, kukamilika kwa miradi hiyo kutawezesha ajira zipatazo 32,000 na mapato ya takriban Sh trilioni 2.8,” alisema Dk Kigoda.
Alieleza kuwa jambo la kutia moyo ni kwamba tayari dola za Marekani bilioni tatu (Sh trilioni tano) zimepatikana na wabia wa miradi hiyo, NDC na Tanzania China International Mineral Resources Ltd (TCIMRL) na kuwezesha ujenzi wa viwanda vya chuma kuanza mwaka 2014/15.
Kuhusu ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha viuadudu vya kuua viluwiluwi vya mbu waenezao malaria mjini Kibaha, kwa kutumia teknolojia kutoka Cuba, alisema ujenzi wa majengo umekamilika kwa asilimia 90.
“Mitambo imekwishanunuliwa na kufikishwa katika eneo la ujenzi na hivi sasa inawekwa tayari kwa uzalishaji mwanzoni mwa mwaka 2014/205 yaani mwezi Julai 2014,” alisema Waziri.
Alisema kukamilika kwa mradi huo ni ukombozi mkubwa kwa Taifa katika kupambana na malaria kwa kuwa viuadudu vitakavyozalishwa, kazi yake ni kuua mbu kuzaliana na hivyo kupunguza wagonjwa wa malaria, gharama za kununua vyandarua na dawa za kuulia mbu.
Akizungumzia kiwanda cha General Tyre Ltd (GTEA), alisema NDC imekamilisha kukarabati majengo na ukarabati wa mfumo wa umeme unaendelea na kisha utafuatiwa na kujaribu mitambo.Kuhusu uzalishaji wa magadi soda Ziwa Natron na Engaruka, alisema utafiti umekamilika kuhusu wingi na ubora wa rasilimali za magadi.
Alisema kiasi cha meta za ujazo bilioni 4.68 za magadi ambazo huongezeka kwa kiasi cha mita za ujazo milioni 1,8675 zimegundulika katika Bonde la Engaruka. Kwa sasa, anatafutwa mtaalamu mshauri na makadirio ya ujenzi wa yatajulikana baada ya usanifu wa mradi huo ambao unatarajiwa kuanza uzalishaji mwaka 2016/17.
Utaingiza dola za Marekani milioni 320 kwa mwaka na utatoa fursa za ajira 3,900. Dk Kigoda akizungumzia saruji alisema kumeanzishwa viwanda katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani, na miradi hiyo itakapokamilika pamoja na viwanda vilivyopo, vitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni sita kwa mwaka na kutoa ajira zaidi ya 5,000.
“Kiasi hicho cha saruji kitakuwa mara mbili ya mahitaji ya saruji nchini, na hivyo kuwezesha kujitosheleza kabisa,” alisema waziri.
Kuhusu fidia katika maeneo yaliyochukuliwa kwa ajili ya uwekezaji, Dk Kigoda alisema kimsingi Serikali inawajibika kuwalipa fidia wananchi katika maeneo hayo, itajaribu kukamilisha fidia hiyo mwaka 2014/15.
Aliyataja maeneo yenye kuhitaji fidia kuwa ni Kurasini Dar es Salaam, Bagamoyo, Ruvuma, Mtwara na Tanga.
Aliyataja baadhi ya malengo ya mwaka 2014/15 ni kukamilisha Sheria ya Kusimamia Biashara ya Chuma Chakavu na kuandaa kanuni zake, kuandaa Sera ya Taifa ya Kumlinda mlaji na kuendeleza utekelezaji wa utaratibu wa kupima ubora wa bidhaa zote mahali zinapotoka kabla ya kuingia nchini.
Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara ya Viwanda na Biashara imeomba kutengewa jumla ya Sh 112,497,801,000.
 CHANZO:HABARILEO

No comments:

Post a Comment