TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Monday, May 5, 2014

SERIKALI KUFUTA MISAMAHA YA VAT

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi. Picha na Maktaba
Dar es Salaam. Serikali itawasilisha bungeni rasimu ya maboresho ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo itafuta misamaha ya kodi hiyo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema jana kwamba mpango huo unafanyiwa uchambuzi na Serikali na kwamba utawasilishwa katika Bunge la Bajeti wiki mbili zijazo.
Kwa nyakati tofauti, mwenyekiti wa CUF ambaye pia ni mtaalamu wa uchumi, Profesa Ibrahim Lipumba alikuwa akipigia kelele juu ya wingi wa misamaha ya kodi akisema imekuwa ikipoteza kiasi kikubwa cha mapato ya Serikali.
Profesa Lipumba alisema hivi karibuni kuwa ili kuondoa kasi ya ukuaji wa nakisi, Serikali inatakiwa kufuta kabisa misamaha holela ya kodi inayofikia Sh1.8 trilioni ambayo ni sawa na asilimia tano ya pato la taifa.
Siku tano zilizopita, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, wakati akiwasilisha mpango wa Bajeti ya mwaka 2014/15 kwa wabunge, alisema Serikali imepanga kukamilisha utungwaji mpya wa Sheria ya VAT.
Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na kuongeza wigo wa kodi kwa kuimarisha vyanzo vilivyopo na kuanzisha vyanzo vipya pamoja na kurasimisha sekta isiyo rasmi ili iingie kwenye mfumo rasmi wa kodi.
Katika bajeti ya mwaka 2013/14, Serikali iliondoa msamaha wa VAT kwa viwanda vya nguo vinavyotumia pamba ya ndani.
Kwa mujibu wa ripoti ya utafiti ya taasisi ya CRC Sogema ambayo inaishauri Wizara ya Fedha, misamaha chini ya Kodi ya VAT ilifikia Sh802 bilioni kwa mwaka 2012, wakati jumla ya misamaha yote ilikuwa Sh1.8 trilioni.
Ripoti hiyo ya mwaka 2013 inasema: “Matokeo ya utafiti huu muhimu yanapendekeza kuwa kuna ufanisi zaidi kwa nchi zinazoendelea kujikita zaidi katika kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji kuliko kutoa misamaha ya kodi kwa mashirika.”
Jana, Lukuvi alisema: “Serikali ina mpango huo na hivi sasa rasimu ya VAT bado inaandaliwa na jambo hilo lipo mikononi mwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.”
Hata hivyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema hakupatikana jana kuzungumzia hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya rasimu hiyo.
Wasomi watofautiana 
Hatua hiyo imepokewa kwa mitizamo tofauti na baadhi ya wachumi, wengine wakisema itaongeza mapato ya Serikali tofauti na ilivyokuwa awali na wengine wakisema itawaumiza zaidi wananchi.
Profesa wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Humphrey Moshi alisema ni hatua nzuri ambayo itaongeza mapato kwa Serikali kwa sababu taasisi nyingi zilikuwa zikitumia vibaya misamaha hiyo.
“Fedha zitakazopatikana zitumike vizuri kwa kugharimia miundombinu, kutoa huduma bora za elimu na afya na si posho na vikao visivyo na tija,” alisema.
Alisema hata kama Serikali itaondoa misamaha hiyo, bado ina wajibu wa kufanya uchambuzi wa kina na kuujulisha umma kuwa ni taasisi gani zilitumia vibaya misamaha hiyo.
Hata hivyo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (Sua), Dk Damian Gabagambi alisema hatua hiyo ikifanikiwa itaathiri jamii kwa kuwa baadhi ya taasisi zilizokuwa zinasamehewa kodi zilikuwa zikisaidia kwa kiasi kikubwa.
Alisema Serikali na baadhi ya watu wanaopinga misamaha ya kodi wamekuwa wakiangalia upande wa gharama au hasara inayotokana na misamaha hiyo bila kuangalia faida zake.
“Nipo tofauti kabisa na wanaounga mkono hatua hiyo; kwa sababu taasisi nyingi kama mashirika ya dini yamekuwa yakitoa huduma nzuri kwa wananchi. Wasikurupuke kuondoa misamaha kwa kuwafurahisha watu,” alionya Dk Gabagambi.
Alisema Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilishindwa kufanya uchunguzi wa kina kugundua ni kina nani waliokuwa wakitumia vibaya misamaha hiyo kutokana na usimamizi mbovu.
“Unapokuwa umetoa misamaha ni lazima uweke mifumo mizuri ya ufuatiliaji kubaini watu watakayoitumia vibaya, lakini TRA hawatumii mfumo huo,” alisema.
Alisema iwapo Serikali itafuta misamaha hiyo kuna uwezekano mkubwa wa kuwepo madhara makubwa katika uwekezaji, ajira na huduma kwa jamii kwa kuwa baadhi ya mashirika yanayosamehewa kodi yalikuwa yanaajiri watu wengi na kutoa huduma nzuri.
Serikali imekuwa ikitafuta vyanzo mbalimbali vya mapato na moja ya ha Mkakati mwingine ni kuanzisha kodi ya kila mwezi ya matumizi ya kadi za simu ambao haukufanikiwa kutokana na kupingwa na wadau mbalimbali. CHANZO: MWANANCHI (FS)

No comments:

Post a Comment