WIZARA ya Viwanda na Biashara 
imewasilisha bungeni bajeti yake inayoonesha mapinduzi makubwa katika 
viwanda, ikiwamo kuanza kwa miradi ya chuma ya Liganga na Mchuchuma na 
kiwanda cha kuua viluwiluwi vya mbu waenezao malaria.
Pia 
kiwanda cha matairi cha General Tyre kinatarajiwa kuanza tena uzalishaji
 katika mwaka ujao wa fedha. Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah 
Kigoda aliwasilisha bajeti yake hiyo bungeni jana.(Martha Magessa)
         
            
Dk Kigoda
 alisema ukuaji wa sekta ya viwanda ni mzuri kwani umeongezeka kutoka 
asilimia 5.5 mwaka 1998 hadi asilimia 7.7 mwaka 2013, ingawa ukuaji huo 
uko chini kidogo ukilinganisha na mwaka 2012.
“Ukuaji 
huu umechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuimarika kwa uzalishaji viwandani,
 hususani viwanda vya vinywaji, saruji, bidhaa za chuma, na usindikaji 
wa mazao ya kilimo,” alisema Dk Kigoda.
Kuhusu 
Liganga na Mchuchuma, alisema katika mwaka 2013/14, utafiti uliofanywa 
na Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) umethibitisha 
kuwapo kwa mashapo ya makaa ya mawe ya tani milioni 370 katika eeno la 
kilometa za mraba 30.
Alisema 
utafiti huo, pia umethibitisha kuwapo kwa mashapo ya madini ya chuma ya 
tani milioni 219 katika eneo la kilometa za mraba 10.
“Mpango 
wa awali ni kuzalisha tani milioni moja za chuma na megawati 600 za 
umeme. Kiasi hicho cha uzalishaji wa chuma kitaifanya Tanzania kuwa ya 
tatu barani Afrika katika uzalishaji chuma.
“Aidha, kukamilika kwa miradi hiyo kutawezesha ajira zipatazo 32,000 na mapato ya takriban Sh trilioni 2.8,” alisema Dk Kigoda.
Alieleza 
kuwa jambo la kutia moyo ni kwamba tayari dola za Marekani bilioni tatu 
(Sh trilioni tano) zimepatikana na wabia wa miradi hiyo, NDC na Tanzania
 China International Mineral Resources Ltd (TCIMRL) na kuwezesha ujenzi 
wa viwanda vya chuma kuanza mwaka 2014/15.
Kuhusu 
ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha viuadudu vya kuua viluwiluwi vya mbu 
waenezao malaria mjini Kibaha, kwa kutumia teknolojia kutoka Cuba, 
alisema ujenzi wa majengo umekamilika kwa asilimia 90.
“Mitambo 
imekwishanunuliwa na kufikishwa katika eneo la ujenzi na hivi sasa 
inawekwa tayari kwa uzalishaji mwanzoni mwa mwaka 2014/205 yaani mwezi 
Julai 2014,” alisema Waziri.
Alisema 
kukamilika kwa mradi huo ni ukombozi mkubwa kwa Taifa katika kupambana 
na malaria kwa kuwa viuadudu vitakavyozalishwa, kazi yake ni kuua mbu 
kuzaliana na hivyo kupunguza wagonjwa wa malaria, gharama za kununua 
vyandarua na dawa za kuulia mbu.
Akizungumzia
 kiwanda cha General Tyre Ltd (GTEA), alisema NDC imekamilisha 
kukarabati majengo na ukarabati wa mfumo wa umeme unaendelea na kisha 
utafuatiwa na kujaribu mitambo.Kuhusu uzalishaji wa magadi soda Ziwa 
Natron na Engaruka, alisema utafiti umekamilika kuhusu wingi na ubora wa
 rasilimali za magadi.
Alisema 
kiasi cha meta za ujazo bilioni 4.68 za magadi ambazo huongezeka kwa 
kiasi cha mita za ujazo milioni 1,8675 zimegundulika katika Bonde la 
Engaruka. Kwa sasa, anatafutwa mtaalamu mshauri na makadirio ya ujenzi 
wa yatajulikana baada ya usanifu wa mradi huo ambao unatarajiwa kuanza 
uzalishaji mwaka 2016/17.
Utaingiza
 dola za Marekani milioni 320 kwa mwaka na utatoa fursa za ajira 3,900. 
Dk Kigoda akizungumzia saruji alisema kumeanzishwa viwanda katika mikoa 
ya Mtwara, Lindi na Pwani, na miradi hiyo itakapokamilika pamoja na 
viwanda vilivyopo, vitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni sita kwa 
mwaka na kutoa ajira zaidi ya 5,000.
“Kiasi 
hicho cha saruji kitakuwa mara mbili ya mahitaji ya saruji nchini, na 
hivyo kuwezesha kujitosheleza kabisa,” alisema waziri.
Kuhusu 
fidia katika maeneo yaliyochukuliwa kwa ajili ya uwekezaji, Dk Kigoda 
alisema kimsingi Serikali inawajibika kuwalipa fidia wananchi katika 
maeneo hayo, itajaribu kukamilisha fidia hiyo mwaka 2014/15.
Aliyataja maeneo yenye kuhitaji fidia kuwa ni Kurasini Dar es Salaam, Bagamoyo, Ruvuma, Mtwara na Tanga.
Aliyataja
 baadhi ya malengo ya mwaka 2014/15 ni kukamilisha Sheria ya Kusimamia 
Biashara ya Chuma Chakavu na kuandaa kanuni zake, kuandaa Sera ya Taifa 
ya Kumlinda mlaji na kuendeleza utekelezaji wa utaratibu wa kupima ubora
 wa bidhaa zote mahali zinapotoka kabla ya kuingia nchini.
Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara ya Viwanda na Biashara imeomba kutengewa jumla ya Sh 112,497,801,000.
 CHANZO:HABARILEO