TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Sunday, April 14, 2013

SERIKALI YAOMBA SH. BILLION 1 KUZIKA VIONGOZI WATAKAOKUFA MWAKA HUU

Katika hali inayotafsiriwa kuwa ni ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma, Ofisi ya Waziri Mkuu, imeomba Shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuwazika viongozi wa kitaifa watakaokufa katika mwaka wa fedha unaoanza Juni, mwaka huu.
Iliwasilisha ombi hilo kwenye bajeti yake iliyosomwa bungeni Jumatano wiki hii.
Kufuatia ombi hilo, wabunge Lucy Owenya Viti maalumu (Chadema) na Kange Lugora (CCM) Mwibara, wameishambulia ofisi hiyo na kuhoji ni viongozi gani wa kitaifa watakaokufa mwaka ujao.
Owenya ndiye aliyeibua hoja hiyo wakati akichangia hotuba ya makadirio na matumizi ya ofisi hiyo iliyowasilishwa bungeni Jumatano wiki hii na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Owenya alisema inashangaza kutumia mabilioni kwa watu watakaokufa badala ya kuwekeza fedha hizo kwa maendeleo ya walio hai.
Aliitaka Ofisi ya Waziri Mkuu kupunguza fedha hizo na kujenga chumba cha upasuaji cha hospitali ya Mawenzi na kuisaidia hospitali teule ya St Joseph kununua vitanda vya wodi ya wazazi.
Lugora kwa upande wake akiponda bajeti hiyo alisema licha ya kuwa mbunge wa CCM haungi mkono bajeti ya Waziri Mkuu, akiituhumu kuomba kutengea Sh bilioni kwa ajili ya mazishi ya viongozi watakaokufa ni ubadhirifu.

“Siungi mkono hoja mpaka nione bajeti inaeleza mikakati na dhamira ya dhati ya kumaliza rushwa na dawa za kulevya nchini,” alisema.
“Mazishi gani ya viongozi bilioni moja huu ni wizi, wizi mtupu ndani ya serikali kama wasipokufa tutapata ripoti ya matumizi mengine ya fedha hizo.”

RUSHWA
Alisema “sikubaliani na bajeti ya namna hii mpaka kwanza ionyeshe itakavyomaliza janga la rushwa na madawa ya kulevya nchini.”
Alisema kama watuhumiwa hao wanafahamika lakini hawakamatwi kutokana na rushwa ama baadhi yao ni vigogo wa serikali wakiwamo mawaziri.
Lugora aliahidi kuwa kabla ya bunge kumalizika atawasilisha orodha ya majina ya watendaji wa serikali wanaojihusisha na rushwa na dawa za kulevya.
Aliwatetea polisi kuwa hawahusiki na rushwa badala yake wanasingiziwa akieleza mishahara midogo na kukosa nyumba za kuishi kuwa ndicho chanzo cha mianya ya rushwa ndani ya jeshi hilo.

PAKISTAN CHANZO CHA MIHADARATI
Mbunge wa Wawi (CUF) Mohamed Rashid aliitaja Pakistan kuwa ni njia kuu inayoingiza madawa ya kulevya nchini na kushauri idhibitiwe.
Aidha alisema inashangaza kwa miaka 50 ya uhuru hakuna halmashauri inayojitegemea kwa mapato badala yake zinaitegemea serikali kuu.
Alitaka sharia na sera za kodi zirekebishwe ili halmashauri zijitegemee na pia zichangie pato la taifa.
VURUGU ZA KIDINI
Mbunge wa Mbinga Mashariki (CCM) Gaudence Kayombo aliitaka serikali itimize wajibu wake wa kulinda wananchi wasidhurike na chokochoko za kidini badala ya kuwaambia viongozi wa dini wazungumze na waumini wao.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment