TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Friday, April 19, 2013

DKT. MGIMWA : UCHUMI WA TANZANIA UNAKUA
IMG 3548 a7715

Waziri wa Fedha Mhe. Dr. Augustao Wiliam Mgimwa amewaeleza Benki ya Dunia pamoja na Shirika la Fedha la Kimataifa vipimo vya ukuaji wa nchi yetu kiuchumi ambapo unakuwa kwa asilimia 6.9. Ukuaji huu wa uchumi ni mkubwa ukilinganisha na ilivyokuwa  mwaka uliopita 2011 ambapo ilikuwa ni asilimia 6.3. 

Akizungumzia mfumuko wa bei, Mgimwa alisema kuwa, mfumuko wa bei umepungua  kutoka asilimia 19.8 kwa Desemba mwaka 2011 na kufikia asilimia 9.8 kwa mwezi Machi mwaka huu 2013. Aidha aliendelea kuongeza kuwa viwango vya ubadilishaji fedha umeendelea kuimarika na upatikanaji wa vyakula nao unakwenda vizuri.
Akiendelea kufafanua Mhe. Dkt Mgimwa alisema katika “Mikutano hii ya majira ya kipupwe inayoendelea hapa Washington inatupatia fursa ya kueleza hali tuliyofikia katika kuendesha uchumi wetu, nafasi tuliyonayo kiuchumi, na tunapata nafasi ya kujieleza ni namna gani Tanzania inavyoweza kukidhi mahitaji ya wananchi wake pamoja na utendaji wa uchumi wetu. Aidha alisema kuwa Tanzania inapata nafasi ya kuishawishi dunia ili iweze kutuunga mkono katika maeneo tunayowekeza.
 “Katika mikutano hii ya Majira ya kipupwe tunapata nafasi ya kuwa katika muda mzuri wa kupata uwezekano wa kuyatatua matatizo yetu ya kiuchumi kwa kuwekeza zaidi ili vyanzo vyetu tunavyowekeza viweze kutuletea maendeleo ya haraka”. Aidha Mgimwa aliendelea kueleza kuwa hivi sasa Serikali inawekeza katika gesi iliyoko Mtwara ili itumike kutoa umeme kwani bei yake ni ndogo ukilinganisha na bei ya mafuta ambayo yanatumika. Aidha alisema kuwa Gesi hii itasaidia viwanda kupata umeme na kuongeza ajira pamoja na mapato ya Taifa yatakuwa kwa haraka zaidi.

“Serikali ina mpango wa kupanua Reli, Bandari ya Dar es Salaam, Mtwara, Tanga na Bagamoyo ili kurahisisha uingizaji wa mizigo na kukuza biashara kwa nchi zinazotuzunguka pamoja na kurahisisha usafiri kwa wananchi kwa njia ya reli.” Aliongeza Mgimwa.

“Tumezungumzia namna ya kuunganisha reli za nchi zinazotuzunguka kama vile Zambia, Burundi, Rwanda na Uganda hivyo tunavyowaeleza hivi tunapata wawekezaji wengi wanaotuunga mkono kwa kupitia Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa. Mpaka sasa hivi wameonyasha kwamba utendaji wa uchumi wa nchi yetu unakwenda vizuri kwa hivyo wana imani kubwa na nchi yetu. Kwa kuwaeleza hivyo wao wanaweka ushawishi kwa wawekezaji wakubwa walioko katika nchi zingine”. Alisema Mhe.Dkt Mgimwa.  
 Mgimwa alimalizia kwa kuwaomba wananchi kuwa, waunge mkono sera zinazowekwa mbele yao ambazo zinaboresha uchumi, tunaomba wawekezaji binafsi katika sekta binafsi nao watuunge mkono kwa kuwekeza katika miradi ambayo tunaiweka mbele yao ili washirikiane kuiboresha na kuijenga Tanzania. Kila mtu atuunge  mkono kwa sababu tunataka Tanzania ibadilike na kuongeza kasi ya maendeleo ili kila mtu apate nafasi ya kuboreka kiuchumi. Chanzo: Ingiahedi Mduma, Msemaji- Wizara ya Fedha.

No comments:

Post a Comment