KODI YA SIMU KURUDI BUNGENI AGOSTI MWAKA HUU KWA AJILI YA KUJADILIWA UPYA
SAKATA la kodi ya simu ya Sh 1,000 kwa kila laini ya simu kwa mwezi, inayolipwa na watumiaji wa simu, litamalizwa bungeni kisheria.
Waziri wa Fedha, William Mgimwa, amesema 
wameanza kutekeleza agizo la Rais Jakaya Kikwete, la kuitaka Wizara ya 
Fedha kukutana na wadau wengine, kuangalia namna ya kupata vyanzo 
vingine vya mapato mbadala wa kodi hiyo.
 
Alisema hayo alipozungumza jana na Habari leo, baada ya kusaini mkataba wa msaada wa zaidi ya Sh bilioni 
344, kutoka Benki ya Dunia, ili isaidie masuala mbalimbali katika sekta 
ya usafirishaji. 
Mgimwa alisema katika suala hilo, masuala ya kisheria 
yatafikishwa bungeni mwezi ujao, ili kumaliza utata wa kodi hiyo.
Alisema uamuzi wa kushughulikia suala 
hilo, ulifikiwa kutokana na agizo la Rais Kikwete la hivi karibuni, 
kutaka wizara hiyo na ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia kukaa na 
kampuni za simu kumaliza utata uliojitokeza kuhusu kodi hiyo.
Awali Umoja wa Wamiliki wa Kampuni za 
Simu (MOAT), ulitoa maoni kutaka kufutwa kwa kodi hiyo, kutokana na 
kulalamikiwa na wadau wa sekta ya mawasiliano.
Mbali na Moat, pia baadhi ya viongozi wa
 Serikali, wabunge na wananchi, walipinga kodi hiyo kwa walichokieleza 
kuwa itaongeza mzigo wa ugumu wa maisha kwa mtumiaji, hususan wa kipato 
cha chini.
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari 
Makamba, alipozungumza na gazeti hili jana, alisema mara baada ya Rais 
kutoa agizo, wizara husika zilikutana kufanyia kazi agizo hilo.
"Rais akishaagiza kinachofuata ni 
utekelezaji na sisi kesho yake tulianza vikao na ninachoweza kukwambia 
tuko pazuri na tukikamilisha majadiliano yetu, tutatoa taarifa," alisema
 Makamba.
Alisema lengo ni kuangalia kama Serikali
 inaweza kupata Sh bilioni 178 kutoka vyanzo vingine, iwapo itaamua 
kufuta kodi inayotokana na tozo ya Sh 1,000 kutoka kwenye laini za simu.
Hivi karibuni, Rais Kikwete aliagiza 
Wizara za Serikali zinahusika na kodi na mawasiliano na kampuni za simu 
za mikononi nchini, kukutana kutafuta jinsi ya kumaliza mvutano wa kodi 
hiyo.
Alitoa maelekezo hayo baada ya kukutana 
na viongozi wa Wizara ya Fedha, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na 
Teknolojia na wawakilishi wa kampuni za simu za TTCL, Airtel, Vodacom, 
Tigo na Zantel. 
Rais alisema lengo kuu la mkutano huo, liwe kupendekeza 
jinsi ya kuziba pengo la Sh bilioni 178 ambazo zitapotea katika bajeti, 
iwapo kodi hiyo itafutwa na Serikali kupitia marekebisho kwenye Muswada 
wa Fedha wa Bajeti ya Mwaka 2013/14.
Aliwaambia wawakilishi wa pande hizo 
mbili kuwa hawezi kuifuta moja kwa moja kodi hiyo, bila kutafuta njia 
nyingine za kupata fedha za kujaza pengo litakalotokeza, huku tayari 
Bunge limezipangia matumizi.
“Nakuombeni kaeni pamoja, wekeni bongo 
zenu pamoja, wekeni akili yenu pamoja tutafute namna gani tutajaza pengo
 hili la Sh bilioni 178, endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha
 wananchi mzigo mzito na kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni 
ngumu,” alisema Rais Kikwete.
Habari Leo
Habari Leo

































