Lukuvi: Tukipitisha serikali tatu jeshi litatawala nchi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Uratibu na Bunge), William Lukuvi.PICHA|MAKTABA
Waziri wa
 Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Uratibu na Bunge), William Lukuvi 
ameanza kampeni kanisani kuwataka wananchi kupinga serikali tatu 
zilizopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, vinginevyo nchi 
itatawaliwa na jeshi kwa kuwa Serikali ya Muungano itashindwa kuwalipa 
mishahara wanajeshi.
Alisema hayo jana katika Kanisa la Methodist, Jimbo la Dodoma alipokuwa mgeni rasmi akimwakilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Katika 
hotuba yake, Lukuvi aliwaeleza waumini waliofurika katika ibada ya 
kumsimika Mchungaji Joseph Bundala kuwa askofu wa kanisa hilo katika 
jimbo kuwa waendelee kuliombea Bunge lifanye uamuzi sahihi wa serikali 
mbili.(MM)
Aliwataka
 Watanzania kuipuuza Rasimu ya Katiba katika suala la Muungano na 
Serikali tatu kwa madai kuwa kutaka kuwapo mfumo huo ni kutaka 
Watanzania waingie vitani.
"Serikali
 tatu zikipita ni wazi kuwa hata makanisa yatafungwa kwani nchi haiwezi 
kuwa na amani tena, angalieni nchi ya Korea Kusini na Korea Kaskazini 
ambao waligawanyika na sasa ni maadui wakubwa wanaokaa mipakani 
wamenyoosheana bunduki," alisema na kuongeza:
"Waumini 
ndugu zangu wapendwa, kwa sasa tupo katika hali mbaya sana hapo bungeni,
 tunaomba mtuombee kuna watu ambao wanataka madaraka kwa nguvu na 
wameanza kutafuta jinsi ya kuvunja Muungano na kudai kuwapo kwa Serikali
 tatu, nawaomba sana wapuuzeni wale wote ambao wanataka serikali tatu."
Alisema 
watu wa aina hiyo wanaonekana kuwa wana huruma na Watanzania na wanadai 
kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika wakati hiyo Tanganyika wanayoidai ni 
jina tu ambalo Wajerumani walikaa mezani wakabuni na kutuletea.
Lukuvi 
alisema Wazanzibari wanaotaka kuwa na nchi yao hawawezi kujitegemea, 
bali wanataka Serikali ili wapate nafasi ya kujitangaza kuwa ni nchi ya 
Kiislamu.
Alisema 
wanaopiga kelele wana ajenda za siri na nia yao kutaka kufanya fujo na 
kusababisha machafuko... "Kwani ukiwa na mke mmoja akakushinda unafikiri
 utatuzi ni kuoa mke mwingine?"
Baadaye 
alipotakiwa kufafanua kauli yake, Lukuvi alisema alichokizungumza 
kanisani hapo ni mawazo yake binafsi ambayo yanafanana na Watanzania 
wengi, akiwamo Rais Jakaya Kikwete.
"Unajua 
jeshi haliwezi kukaa na bunduki bila fedha. Hiyo Serikali ya tatu ambayo
 jeshi litakuwa chini yake haina vyanzo vya mapato vya kueleweka, sasa 
hao wanajeshi watalipwa nini? Wenye mitutu watakubali kuishi bila 
fedha?"
Alisema 
hata vyanzo vya mapato ambavyo vimeandikwa katika Rasimu ya Katiba ni 
lazima visimamiwe na pande mbili za Muungano, akiwa na maana ya 
Tanganyika na Zanzibar na kwamba kama upande mmoja ukishindwa kuchangia 
hali itakuwa mbaya.
CHANZO:MWANANCHI
No comments:
Post a Comment