KAMATI YA MAADILI NA HAKI YAKWAMA KUMUHUKUMU WENJE

Na Hudugu Ng'amilo
Hukumu 
dhidi ya mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Ezekiah Wenje imekwama 
kutolewa jana baada ya mjumbe huyo kushindwa kupatikana ili kuwasilisha 
utetezi wake.
Wenje 
anadaiwa kuwatuhumu mawaziri wanne akiwemo Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa
 kutoa rushwa kwa wajumbe wa kundi la 201, ili wapitishe kura ya wazi na
 kuunga mkono serikali mbili.
Viongozi 
wengine waliohusishwa na tuhuma hizo ni Waziri wa Maji Profesa Jumanne 
Maghembe, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa na 
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka.
Mwenyekiti
 wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta aliamua kulipeleka shauri 
kwenye kamati ya maadili na haki za Bunge, baada ya Wenje kukataa kufuta
 kauli yake na kuwaomba radhi wajumbe hao.
Akiwasilisha
 taarifa ya kamati hiyo bungeni jana kwa niaba ya mwenyekiti, Pandu 
Ameir Kificho, makamu mwenyekiti, Dk Susan Kolimba alisema jitihada za 
kumtafuta Wenje bado zinaendelea.
Hata 
hivyo Dk Kolimba alisema kamati yake imefanikiwa kuwahoji Dk Kawambwa na
 Kabaka pamoja na wajumbe wawili kutoka kundi la 201 waliolalamika, 
Esther Mlimba na Dk Eve Semakafu.
"Mwenyekiti
 alipomtaka kuomba radhi alisema anaweza kuomba radhi kwa msingi tu 
kwamba ukweli aliousema umewaudhi watu, hivyo anaomba radhi kwa ukweli 
aliousema," alisema Dk Kolimba.
Alisema 
baada ya Wenje kutopatikana, kamati hiyo iliona ni busara kuwasikiliza 
mawaziri waliotuhumiwa pamoja na wale waliolalamikia kauli hiyo ya Wenje
 ambao ni Semakafu na Mlimba.
"Jitihada
 za kumtafuta Maghembe zilishindikana...Tunatarajia baada ya Wenje 
kufika mbele ya kamati tutawasilisha mapendekezo yetu mbele ya Bunge 
hili,"alisema Dk Kolimba.
Baada ya 
kutolewa kwa taarifa hiyo, Sitta alisema suala hilo litaamuliwa hapo 
baadaye baada ya kamati hiyo kukamilisha kazi yake ikiwamo kumhoji Wenje
 na wengine waliotuhumiwa.
:Chanzo Mwananchi.
:Chanzo Mwananchi.
No comments:
Post a Comment