Wajumbe wa Bunge watishiwa maisha

Siku tatu
 kabla ya Bunge la Katiba kuanza kupigia kura Rasimu ya Katiba 
inayopendekezwa, watu wasiojulikana wameanza kusambaza vitisho vya 
kuwatia hofu wajumbe wa Bunge hilo.
Watu hao 
wamesambaza vipeperushi katika maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma usiku 
wa kuamkia jana, wakiwataka wajumbe kutoingia bungeni vinginevyo 
yatakayowapata watajuta, huku wajumbe kutoka Zanzibar wakitishiwa kwa 
ujumbe wa simu kupitia mtandao wa WhatsApp.
Tayari, 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd ametoa kauli 
kuhusu vitisho hivyo akisema Serikali itachukua kila hatua kuhakikisha 
wajumbe kutoka visiwani humo ambao wamekuwa wakipokea vitisho wanakuwa 
salama.
Mbali na 
kusambazwa kwa karatasi hizo, maandishi mekundu yamechorwa katika kuta 
za jengo la Makao Makuu ya CCM mjini Dodoma yakisomeka, "No Katiba. No 
ufisadi."(P.T)
Vikaratasi
 vilivyosambazwa vinasomeka: "Onyo. Dodoma si mahali pa kufuga wezi wa 
fedha za umma. Utakayeingia bungeni kuanzia kesho (leo), yatakayokupata 
utajuta."
Mkazi wa 
Dodoma, Sospeter Samwel alimwambia mwandishi wetu jana kuwa aliokota 
baadhi ya vipeperushi hivyo jana saa moja asubuhi katika eneo maarufu la
 kuuzia magazeti linalotazamana na Jengo la CCM.
"Tulikuta
 hayo makaratasi yametupwa tu ovyoovyo ila baadaye nikasikia maeneo 
mbalimbali mengine nayo yameonekana yametupwa. Sijui nani hasa watakuwa 
wameyasambaza," alisema.
Katibu wa
 Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa jana kuhusu na 
maandishi hayo alijibu kwa kifupi "No comment" (sina cha kusema).
Kamanda 
wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime jana alitoa taarifa ya maandishi 
kwa wanahabari akisema jeshi hilo linawasaka watu waliosambaza 
vipeperushi hivyo.
"Wananchi
 na wageni wapenda amani waendelee na shughuli zao kama kawaida kwani 
polisi tumejiimarisha ipasavyo kukabiliana na yeyote atakayekiuka sheria
 na maelekezo yaliyotolewa.
Mkuu wa 
Mkoa wa Dodoma, Dk Rehema Nchimbi alitoa onyo kwa watu aliodai wanafanya
 mzaha akisema vyombo vya usalama viko macho saa 24. Aliwataka wajumbe 
kutoa taarifa kwa vyombo vya dola wanapoona viashiria vya kutokuwa na 
usalama.
"Kama 
ng'ombe mzima tumeshakula tumebakiza mkia tu, niwahakikishie wajumbe wa 
Bunge Maalumu la Katiba, usalama umekuwapo na utaendelea kuwapo.
Wazanzibari kulindwa
Akizungumzia
 vitisho hivyo hasa kwa wajumbe kutoka Zanzibar, Balozi Idd alisema 
Serikali itachukua kila hatua kuhakikisha wanakuwa salama.
Alisema 
kuna ujumbe unazunguka katika mitandao ya jamii ukitoa vitisho kwa 
wajumbe wa Bunge hilo na watumishi wa sekretarieti ya Bunge hilo.
"Vyombo 
vya dola vipo na vitafanya kazi yake. Vinajua vitisho vyote. 
Niwahakikishie wajumbe mtakuwa salama na Serikali itachukua kila hatua 
kuhakikisha hakuna kitakachotokea.
Hoja 17 za Zanzibar
Akizungumzia
 kuhusiana hoja 17 ambazo ziliwasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa 
Zanzibar, Othman Masoud Othman zenye masilahi ya visiwa hivyo, Balozi 
Idd alisema kati yake 13 zilikubalika na kubakia nne.
Hata hivyo, alisema baada ya kuangalia zaidi Rasimu ya Katiba inayopendekezwa waligundua kuwa zilibakia hoja tatu tu.
Alizitaja hoja hizo kuwa ni ibara 86 ambayo inasema Rais wa Jamhuri ya Muungano atashinda kwa kupata kura zaidi ya asilimia 50.
Hata 
hivyo, alisema waliona kwenye Katiba ya sasa jambo hilo liko kimya 
kidogo endapo itatokea mgombea hakupata kura upande wa Zanzibar.
"Tukaona 
kuwa huyu ni Rais wa Muungano, hivi asilimia 50 yote apate Bara 
legitimacy (uhalali) yake kama rais wa Muungano iko wapi?" alisema na 
kuongeza kuwa vyema katika Rasimu ikaingizwa kuwa mgombea huyo pamoja na
 kwamba anatakiwa ashinde kwa zaidi ya asilimia 50, basi angalau katiba 
iweke kiwango fulani cha kupata upande wa Zanzibar.
 Alisema 
baada ya kutafakari ikakubaliwa Zanzibar angalau mgombea huyo apate 
asilimia 10 au 15. Hata hivyo, alisema majadiliano kuhusu suala hilo 
bado yanaendelea.
Chanzo:Mwananchi
No comments:
Post a Comment