TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Friday, September 26, 2014

Wajumbe wa Bunge watishiwa maisha 

Ukumbi-wa-Bunge-la-Katiba_73be3.jpg
Siku tatu kabla ya Bunge la Katiba kuanza kupigia kura Rasimu ya Katiba inayopendekezwa, watu wasiojulikana wameanza kusambaza vitisho vya kuwatia hofu wajumbe wa Bunge hilo.
Watu hao wamesambaza vipeperushi katika maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma usiku wa kuamkia jana, wakiwataka wajumbe kutoingia bungeni vinginevyo yatakayowapata watajuta, huku wajumbe kutoka Zanzibar wakitishiwa kwa ujumbe wa simu kupitia mtandao wa WhatsApp.
Tayari, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd ametoa kauli kuhusu vitisho hivyo akisema Serikali itachukua kila hatua kuhakikisha wajumbe kutoka visiwani humo ambao wamekuwa wakipokea vitisho wanakuwa salama.
Mbali na kusambazwa kwa karatasi hizo, maandishi mekundu yamechorwa katika kuta za jengo la Makao Makuu ya CCM mjini Dodoma yakisomeka, "No Katiba. No ufisadi."(P.T)
Vikaratasi vilivyosambazwa vinasomeka: "Onyo. Dodoma si mahali pa kufuga wezi wa fedha za umma. Utakayeingia bungeni kuanzia kesho (leo), yatakayokupata utajuta."
Mkazi wa Dodoma, Sospeter Samwel alimwambia mwandishi wetu jana kuwa aliokota baadhi ya vipeperushi hivyo jana saa moja asubuhi katika eneo maarufu la kuuzia magazeti linalotazamana na Jengo la CCM.
"Tulikuta hayo makaratasi yametupwa tu ovyoovyo ila baadaye nikasikia maeneo mbalimbali mengine nayo yameonekana yametupwa. Sijui nani hasa watakuwa wameyasambaza," alisema.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa jana kuhusu na maandishi hayo alijibu kwa kifupi "No comment" (sina cha kusema).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime jana alitoa taarifa ya maandishi kwa wanahabari akisema jeshi hilo linawasaka watu waliosambaza vipeperushi hivyo.
"Wananchi na wageni wapenda amani waendelee na shughuli zao kama kawaida kwani polisi tumejiimarisha ipasavyo kukabiliana na yeyote atakayekiuka sheria na maelekezo yaliyotolewa.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Rehema Nchimbi alitoa onyo kwa watu aliodai wanafanya mzaha akisema vyombo vya usalama viko macho saa 24. Aliwataka wajumbe kutoa taarifa kwa vyombo vya dola wanapoona viashiria vya kutokuwa na usalama.
"Kama ng'ombe mzima tumeshakula tumebakiza mkia tu, niwahakikishie wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, usalama umekuwapo na utaendelea kuwapo.
Wazanzibari kulindwa
Akizungumzia vitisho hivyo hasa kwa wajumbe kutoka Zanzibar, Balozi Idd alisema Serikali itachukua kila hatua kuhakikisha wanakuwa salama.
Alisema kuna ujumbe unazunguka katika mitandao ya jamii ukitoa vitisho kwa wajumbe wa Bunge hilo na watumishi wa sekretarieti ya Bunge hilo.
"Vyombo vya dola vipo na vitafanya kazi yake. Vinajua vitisho vyote. Niwahakikishie wajumbe mtakuwa salama na Serikali itachukua kila hatua kuhakikisha hakuna kitakachotokea.
Hoja 17 za Zanzibar
Akizungumzia kuhusiana hoja 17 ambazo ziliwasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Masoud Othman zenye masilahi ya visiwa hivyo, Balozi Idd alisema kati yake 13 zilikubalika na kubakia nne.
Hata hivyo, alisema baada ya kuangalia zaidi Rasimu ya Katiba inayopendekezwa waligundua kuwa zilibakia hoja tatu tu.
Alizitaja hoja hizo kuwa ni ibara 86 ambayo inasema Rais wa Jamhuri ya Muungano atashinda kwa kupata kura zaidi ya asilimia 50.
Hata hivyo, alisema waliona kwenye Katiba ya sasa jambo hilo liko kimya kidogo endapo itatokea mgombea hakupata kura upande wa Zanzibar.
"Tukaona kuwa huyu ni Rais wa Muungano, hivi asilimia 50 yote apate Bara legitimacy (uhalali) yake kama rais wa Muungano iko wapi?" alisema na kuongeza kuwa vyema katika Rasimu ikaingizwa kuwa mgombea huyo pamoja na kwamba anatakiwa ashinde kwa zaidi ya asilimia 50, basi angalau katiba iweke kiwango fulani cha kupata upande wa Zanzibar.
Alisema baada ya kutafakari ikakubaliwa Zanzibar angalau mgombea huyo apate asilimia 10 au 15. Hata hivyo, alisema majadiliano kuhusu suala hilo bado yanaendelea.
Chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment