WACHIMBAJI WADOGO WAISIFIA SERIKALI

Wadau wa 
madini ya vito kutoka sehemu mbalimbali duniani, wakipatiwa huduma 
katika Banda la Tanzania katika Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na 
Usonara – Bangkok, Thailand.

Mfanyabiashara
 wa madini ya vito kutoka Tanzania, Latifah Abdallah akitoa maelezo 
kuhusu madini hayo kwa wadau waliotembelea Banda la Tanzania katika 
Maonesho ya Vito ya Bangkok.

Baadhi ya 
Washiriki kutoka Tanzania katika Maonesho ya Vito ya Bangkok wakipozi 
kwa picha muda mfupi kabla ya kuanza  kwa siku ya tatu ya maonesho hayo.
 Kutoka Kushoto ni Asimwe Kafrika, Iddi Pazzi, Gregory Kibusi, Nelson 
Magawa, Teddy Goliama na Matiko Sanawa.
Wachimbaji
 wadogo na wafanyabiashara wa madini ya vito nchini, wameishukuru na 
kuipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, kwa jitihada 
inazofanya za kuwaendeleza na kuwainua kiuchumi.
Wakizungumza
 kwa nyakati tofauti katika Maonesho ya Kimataifa ya Vito na Usonara 
yanayoendelea jijini Bangkok, nchini Thailand Viongozi waliowawakilisha 
wachimbaji wenzao katika maonesho hayo, Gregory Kibusi na Kassim Pazi 
walisema Serikali imewapa fursa adhimu kwa kuwawezesha kujionea na 
kujifunza zaidi kuhusu sekta hiyo ili waendane na viwango vya kimataifa 
na kumudu ushindani wa soko.
“Hatua
 iliyochukuliwa na Serikali kuandaa na kuwezesha ushiriki wa wachimbaji 
wadogo na wafanyabiashara wa madini ya vito kuja kushiriki maonesho 
makubwa kama haya inastahili kupongezwa,” alisema Pazi.
Alifafanua
 kuwa ushiriki wa wachimbaji na wafanyabiashara wa vito utawapa fursa 
kupanua mtandao na wigo wa biashara kwa kukutana na wadau wa madini hayo
 kutoka sehemu mbalimbali duniani na kubadilishana uzoefu katika kazi 
hiyo.
Aliongeza
 kwamba fursa hiyo pia imewawezesha kutambua aina ya madini ya vito 
yaliyo katika soko ili kuwarahisishia kuzalisha madini hayo kwa wingi 
badala ya kuzalisha kwa kubahatisha tu hali inayopelekea kukosa soko na 
kupata hasara.
“Siku
 za nyuma kwa mfano, kuna madini tuliyokuwa tunayatupa tu kwa kudhani 
hayana thamani, lakini tumeshangaa kwamba katika maonesho haya, wadau 
wengi wanayaulizia. Tumechukua mawasiliano yao ili tukirudi nyumbani 
tuwatumie,” alisema Pazi.
Kwa
 upande wake, Kibusi alisema ushiriki wao katika maonesho husika umekuwa
 wenye tija kwa kiasi kikubwa kwani mbali na kupanua wigo wa mtandao na 
soko, pia wameweza kuuza shehena kubwa ya madini kwa bei nzuri.
“Sisi
 kama Viongozi, tunawajibika kuhakikisha wachimbaji wenzetu waliobaki 
nyumbani wananufaika pia kwa namna moja au nyingine kutokana na ushiriki
 wetu katika maonesho haya, hivyo tutahakikisha tunaandaa semina na 
kuwashirikisha tuliyoyaona na kujifunza huku,” alisema Kibusi.
Aidha,
 alitoa ushauri kwa Serikali kuwapatia nafasi kubwa ya ushiriki 
wachimbaji wadogo katika Maonesho ya Vito yanayotarajiwa kufanyika 
Arusha mwezi Novemba mwaka huu ili wapate fursa ya kukutana na wadau wao
 kutoka sehemu mbalimbali duniani na kujifunza.
Naye
 Kiongozi wa Ujumbe wa Watanzania wanaoshiriki katika maonesho hayo 
ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Uthaminishaji wa Madini ya 
Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini (TANSORT), Archard 
Kalugendo alitoa wito kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ya 
vito kuyatumia maonesho hayo kuboresha kazi na biashara zao.
Alisema,
 lengo la Serikali ni kuona madini ya aina zote yakiwamo ya vito na 
usonara yanainufaisha nchi na wananchi wake ipasavyo ndiyo sababu 
Serikali inatumia njia na mbinu mbalimbali kuwezesha maendeleo hayo.
“Sisi
 kama Serikali, tumefungua njia kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa 
madini ya vito nchini. Ni vema sasa wakaanza kusimama wenyewe taratibu 
ili kuendelea kujifunza na kufanya shughuli zao kwa viwango vya 
kimataifa waweze kumudu ushindani wa soko,” alisema Kalugendo.
Aidha,
 Kalugendo aliwataka wachimbaji na wafanyabiashara waliopata fursa 
kushiriki maonesho ya Bangkok, kuwa mabalozi wazuri ili wawasaidie 
wenzao pasipo ubinafsi wala choyo.
Alisema
 ni wakati sasa madini ya vito yaingize fedha nyingi katika uchumi wa 
nchi na hivyo alitoa changamoto kwa wachimbaji na wafanyabiashara 
kushirikiana na Serikali ili kuhakikisha wanatekeleza mikakati 
iliyowekwa ya kuhakikisha wadau mbalimbali wa madini ya vito wanakuja 
kwa wingi Tanzania badala ya kuwafuata wao nje ya nchi.
“Ifike
 mahala tusilazimike kuleta madini yetu Bangkok, bali Wa-Thailand na 
mataifa mengine waone umuhimu wa kuja kwetu,” alisisitiza Kalugendo.
Hii
 ni mara ya pili kwa Wizara ya Nishati na Madini kupitia TANSORT 
kuratibu na kuwezesha ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya Kimataifa 
ya Vito na Usonara ya Bangkok ambapo wachimbaji wadogo na 
wafanyabiashara wa madini hayo hushirikishwa.
(Awadh Ibrahim).
No comments:
Post a Comment