TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Friday, September 12, 2014

WACHIMBAJI WADOGO WAISIFIA SERIKALI 

pix 1-day 2
Wadau wa madini ya vito kutoka sehemu mbalimbali duniani, wakipatiwa huduma katika Banda la Tanzania katika Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara – Bangkok, Thailand.
pix 6-day 2
Mfanyabiashara wa madini ya vito kutoka Tanzania, Latifah Abdallah akitoa maelezo kuhusu madini hayo kwa wadau waliotembelea Banda la Tanzania katika Maonesho ya Vito ya Bangkok.
pix 8-day 2
Baadhi ya Washiriki kutoka Tanzania katika Maonesho ya Vito ya Bangkok wakipozi kwa picha muda mfupi kabla ya kuanza  kwa siku ya tatu ya maonesho hayo. Kutoka Kushoto ni Asimwe Kafrika, Iddi Pazzi, Gregory Kibusi, Nelson Magawa, Teddy Goliama na Matiko Sanawa.
Wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini ya vito nchini, wameishukuru na kuipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, kwa jitihada inazofanya za kuwaendeleza na kuwainua kiuchumi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika Maonesho ya Kimataifa ya Vito na Usonara yanayoendelea jijini Bangkok, nchini Thailand Viongozi waliowawakilisha wachimbaji wenzao katika maonesho hayo, Gregory Kibusi na Kassim Pazi walisema Serikali imewapa fursa adhimu kwa kuwawezesha kujionea na kujifunza zaidi kuhusu sekta hiyo ili waendane na viwango vya kimataifa na kumudu ushindani wa soko.
“Hatua iliyochukuliwa na Serikali kuandaa na kuwezesha ushiriki wa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini ya vito kuja kushiriki maonesho makubwa kama haya inastahili kupongezwa,” alisema Pazi.
Alifafanua kuwa ushiriki wa wachimbaji na wafanyabiashara wa vito utawapa fursa kupanua mtandao na wigo wa biashara kwa kukutana na wadau wa madini hayo kutoka sehemu mbalimbali duniani na kubadilishana uzoefu katika kazi hiyo.
Aliongeza kwamba fursa hiyo pia imewawezesha kutambua aina ya madini ya vito yaliyo katika soko ili kuwarahisishia kuzalisha madini hayo kwa wingi badala ya kuzalisha kwa kubahatisha tu hali inayopelekea kukosa soko na kupata hasara.
“Siku za nyuma kwa mfano, kuna madini tuliyokuwa tunayatupa tu kwa kudhani hayana thamani, lakini tumeshangaa kwamba katika maonesho haya, wadau wengi wanayaulizia. Tumechukua mawasiliano yao ili tukirudi nyumbani tuwatumie,” alisema Pazi.
Kwa upande wake, Kibusi alisema ushiriki wao katika maonesho husika umekuwa wenye tija kwa kiasi kikubwa kwani mbali na kupanua wigo wa mtandao na soko, pia wameweza kuuza shehena kubwa ya madini kwa bei nzuri.
“Sisi kama Viongozi, tunawajibika kuhakikisha wachimbaji wenzetu waliobaki nyumbani wananufaika pia kwa namna moja au nyingine kutokana na ushiriki wetu katika maonesho haya, hivyo tutahakikisha tunaandaa semina na kuwashirikisha tuliyoyaona na kujifunza huku,” alisema Kibusi.
Aidha, alitoa ushauri kwa Serikali kuwapatia nafasi kubwa ya ushiriki wachimbaji wadogo katika Maonesho ya Vito yanayotarajiwa kufanyika Arusha mwezi Novemba mwaka huu ili wapate fursa ya kukutana na wadau wao kutoka sehemu mbalimbali duniani na kujifunza.
Naye Kiongozi wa Ujumbe wa Watanzania wanaoshiriki katika maonesho hayo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Uthaminishaji wa Madini ya Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini (TANSORT), Archard Kalugendo alitoa wito kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ya vito kuyatumia maonesho hayo kuboresha kazi na biashara zao.
Alisema, lengo la Serikali ni kuona madini ya aina zote yakiwamo ya vito na usonara yanainufaisha nchi na wananchi wake ipasavyo ndiyo sababu Serikali inatumia njia na mbinu mbalimbali kuwezesha maendeleo hayo.
“Sisi kama Serikali, tumefungua njia kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ya vito nchini. Ni vema sasa wakaanza kusimama wenyewe taratibu ili kuendelea kujifunza na kufanya shughuli zao kwa viwango vya kimataifa waweze kumudu ushindani wa soko,” alisema Kalugendo.
Aidha, Kalugendo aliwataka wachimbaji na wafanyabiashara waliopata fursa kushiriki maonesho ya Bangkok, kuwa mabalozi wazuri ili wawasaidie wenzao pasipo ubinafsi wala choyo.
Alisema ni wakati sasa madini ya vito yaingize fedha nyingi katika uchumi wa nchi na hivyo alitoa changamoto kwa wachimbaji na wafanyabiashara kushirikiana na Serikali ili kuhakikisha wanatekeleza mikakati iliyowekwa ya kuhakikisha wadau mbalimbali wa madini ya vito wanakuja kwa wingi Tanzania badala ya kuwafuata wao nje ya nchi.
“Ifike mahala tusilazimike kuleta madini yetu Bangkok, bali Wa-Thailand na mataifa mengine waone umuhimu wa kuja kwetu,” alisisitiza Kalugendo.

Hii ni mara ya pili kwa Wizara ya Nishati na Madini kupitia TANSORT kuratibu na kuwezesha ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok ambapo wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini hayo hushirikishwa.
(Awadh Ibrahim).

 

No comments:

Post a Comment