DR.KHAMIS KINGWANGALLAH ATANGAZA NIA YA KUGOMBEA URAIS 2015

Mwenyekiti
 wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya serikali za Mitaa na Mbunge wa jimbo la
 Nzega Dr. Khamis Kigwangallah akitangaza nia yake ya kugombea urais 
waJamhuri ya Muungano ya Tanzania wakati alipokutana na waandishi wa 
habari kwenye ambapo amesema hajasukumwa na mtu yeyote ila ni yeye 
mwenyewe ameamua kwa moyo wake. 

Mwenyekiti
 wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya serikali za Mitaa na Mbunge wa jimbo la
 Nzega Dr. Khamis Kigwangallah akimtambulisha mke wake Dr Bayoum Awadh 
wakati wa mkutano huo. 

Mzee Nasser SAid Mussa baba mzazi wa Dr. Khamis Kigwangallah na mama yake mzazi Mama Bagaile Lumola.(P.T)

Mzee 
Nasser SAid Mussa baba mzazi wa Dr. Khamis Kigwangallah na mama yake 
mzazi Mama Bagaile Lumola. na watoto wake Sheila kulia ni Hawa. 

Mchungaji Patrick Saso akifanya maombi kabla ya kuanza kwa mkutano huo. 

Baadhi ya waandishi wa habari wakiwa katika mkutano huo. 

Baadhi ya waandishi wa habari wakiwa katika mkutano huo.

Sheikh Abubakary Mwita akiomba dua kabla ya kuanza kwa mkutano huo.
Ndugu viongozi mlioko hapa, wageni waalikwa, wanahabari na watanzania wenzangu mnaonisikiliza;
Ni 
heshima kubwa sana kwangu kupata fursa hii. Ni katika nchi chache sana 
duniani, mtoto wa maskini kama mimi, aliyewahi kutembea mitaani akiuza 
karanga, Big G, maandazi, jerebi na samaki ili kusaidia wazazi kupata 
chochote kwa ajili ya kulisha familia anaweza kuota kuwa Rais wa nchi 
yake. Kwamba, mtoto aliyeenda shule bila viatu anaweza kuwa Daktari. 
Hii 
inamaanisha misingi ya haki na usawa kwa wote iliyowekwa na waasisi wa 
Taifa hili haikuwa ndoto za alinacha, bali ukweli na uhalisia, na 
inafanya kazi. Kwamba, siyo lazima uwe mtoto wa tajiri ndiyo uoneshe 
kipaji chako.
Hili peke
 yake linanipa sababu ya ziada ya kwa nini nitamani kuota kuwa Rais – 
nataka niwe mfano hai wa mafanikio ya Ndoto ya waasisi wa Taifa letu, 
kuwa sote ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuna haki na fursa 
sawa bila kujali nani anatokea familia ipi. Hii ni Tanzania ya ndoto za 
waliotutangulia. Ni lazima atokee kiongozi wa kizazi hiki anayetamani 
kuiongoza Tanzania itakayodumu kwenye misingi hii:
 kwamba 
sisi sote ni ndugu, na tuna fursa sawa. Kwamba, kuendelea kimaisha na 
kibinafsi ni haki ya binadamu na si hisani. Kwamba, mtoto wa mama ntilie
 kama nilivyokuwa mimi hapa, ana haki na fursa ya kuwa mbunge ama Rais 
wa nchi, sawa kabisa na mtoto wa Mbunge.
Kwa namna
 ya kipekee nichukue fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza waasisi wa 
Taifa letu kwa kusimamia tunu hizi. Niwashukuru pia viongozi wote 
walionitangulia kwa kuzilinda, na niahidi nitakuwa wa mwisho kuisaliti 
nchi yangu kwenye mambo haya.
Leo 
nimefika hapa kwa sababu chama change kina mfumo mzuri ulioasisiwa na 
Mwl. Nyerere na umelindwa na Wenyeviti waliomfuatia mpaka na sisi 
tumeukuta. 
Leo 
nimefika hapa kwa sababu Rais Jakaya Kikwete na wajumbe wenzake wa 
Kamati Kuu na Halmashauri Kuu walitumia misingi imara iliyowekwa na 
waasisi wa Chama changu kuamua kuwa nami nina haki ya kuwa Mbunge. Leo 
nazungumza hapa nikiamini kuwa ni misingi hiyo hiyo itatoa uongozi wa 
Taifa letu katika awamu ijayo. 
Babu 
yangu Kizaa Baba aliishi Kijijini Goweko, Mlimani, na alikuwa mfugaji 
mkubwa wa ng’ombe na mrina asali mashuhuri. Yeye na mkewe waliishi 
maisha ya heshima sana pale kijijini. Hawakuwahi kusoma wala kuajiriwa 
japokuwa Babu yangu aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali ndani ya Chama 
Cha TANU na baadaye CCM katika ngazi ya Kata.
Babu 
yangu na Bibi yangu kizaa mama waliishi Nzega, na ndiyo walionilea baada
 ya ndoa ya mama yangu na baba yangu kuvunjika. Walinifundisha mambo 
mengi, kubwa likiwa ni kujiamini, pia kufanya mambo yangu kwa bidii, 
uadilifu, umakini na kwa nidhamu ya hali ya juu. Bibi yangu huyu 
hakusoma shule ya kizungu japokuwa alijifunza kusoma na kuandika. Babu 
yangu alikuwa mjukuu wa Chifu na hivyo alipata fursa ya kusoma Tabora 
School miaka miwili mbele ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. 
Alifanya kazi mbalimbali chini ya serikali ya wakoloni, na alishiriki 
harakati za kuanzishwa na kusambaa kwa chama cha TAA na baadaye TANU. 
Babu yangu aliamini kuwa “binadamu wote ni sawa na kwamba kila mtu 
anastahili kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake”, na kwamba ukoloni 
haukuwa kitu cha sawa, na hivyo kujitawala wenyewe dhidi ya wazungu 
ilikuwa ni haki yetu; pia aliamini katika elimu, na hivyo alifanya 
juhudi kusomesha mabinti zake watatu, mama yangu aliishia kwenye ualimu 
kabla ya kuingia kwenye ndoa. Babu aliamini kuwa Tanzania ya mabinti 
zake itahitaji wasomi, ndoto ambayo ninaishi kuitekeleza kwa ajili ya 
mabinti zangu wawili na Kaka yao, HK Jr.
Japokuwa bibi na babu yangu wameishatangulia mbele ya haki, naamini wananitazama na kutabasamu huko waliko.
Ninaishi 
nikiamini kuwa hadithi ya maisha yangu ni mfano hai kwa maisha ya 
watanzania wengi. Na kwamba, nina deni la kulipa kwa vizazi vijavyo kwa 
kuwa mimi ninafaidi matunda ya mti uliopandwa na vizazi 
vilivyonitangulia. Naliona jukumu la kuhakikisha vizazi vijavyo 
vinafaidi urithi wa Tanzania kuwa ni la kwangu na wenzangu wa kizazi 
hiki.
Kazi 
yangu imenifikisha sehemu nyingi sana za nchi yetu – vijijini na kwenye 
majiji, imenikutanisha na watu wa kila aina – matajiri kwa maskini, 
wazee kwa vijana – hakuna hata mmoja kati ya watu hawa anayetegemea 
Serikali itamtatulia kero zake zote. Wanajua wanapaswa kufanya kazi kwa 
bidii ili wasonge mbele – na wana nia ya kufanya hivyo.
Nenda kwa
 wafanyabiashara wakubwa kule Pugu Road viwandani, kwa watumishi pale 
hospitali ya Taifa Muhimbili, ama pale sokoni Kariakoo kwa 
wafanyabiashara, wote watakuambia hawapendi kuona kodi zao zikitafunwa 
na wachache pale TRA, ama kulipa posho za bure kwa wabunge na mawaziri 
kule Bungeni, kulipia mashangingi ya viongozi na watendaji, kulipia 
tiketi za ndege daraja la kwanza kwa ajili ya safari za viongozi na 
wataalamu wetu kwenda kujifunza kupambana na umaskini wakati wakirudi 
wanauacha uzoefu uwanja wa ndege, ama kulipia semina, warsha na 
makongamano ya wataalamu ya kuandika sera za MKUKUTA, MKURABITA na 
kuandaa bajeti zisizotekelezwa kila mwaka.
Watanzania wanataka kupata huduma bora za afya, elimu, maji, miundombinu.
Nenda 
kule kwa watani zangu, Nanyumbu, ama Tandahimba, ama kwa ndugu zangu 
kule Nduli, Kyela, wazee kule watakuambia hawategemei Serikali 
itawaletea ubwabwa kwenye sahani za fedha, wanajua Serikali 
haitowafanyia kila kitu, lakini wanajua kabisa kuwa wanapaswa kufanya 
kazi kwa bidii na wamekuwa wakifanya hivyo siku zote. 
Wanachohitaji
 wao ni kujengewa mazingira wezeshi kushiriki shughuli zao za kilimo ama
 biashara, waelekezwe namna ya kuongeza uzalishaji kwa kutumia njia za 
kisasa za kilimo chenye tija na ufanisi, waelekezwe wanapataje pembejeo,
 wanapataje mikopo yenye riba nafuu, wanahitaji, mwisho wa siku, wajue 
wapi watauza mazao yao kwa uhakika na bila kudhulumiwa wala 
kucheleweshewa malipo.
Watu 
hawatarajii serikali itabeba mizigo yao yote. Lakini wanaamini kabisa, 
kwamba tukibadili kidogo tu vipaumbele vyetu, tukibadili namna 
tunavyoendesha serikali, tukibadili kidogo namna tunavyoendesha uchumi 
wetu, tutaweza, kwa kiasi kikubwa, kubadili muelekeo mzima wa maisha ya 
baadaye ya watoto na wajukuu zetu. Tutatoa uhakika wa kuiondoa nchi yetu
 kutoka miongoni mwa nchi maskini kabisa duniani.
Na mimi, 
kama watanzania wenzangu wengi, nina imani kubwa kabisa, kwamba tunaweza
 kubadili mustakabali wa Taifa letu. Tunaweza kufungua milango ya maisha
 bora zaidi kwa watanzania. Tutatoa fursa sawa kwa kila mtanzania kuishi
 kwa matumaini, kwamba atabadili maisha yake wakati wowote ule kuanzia 
leo. 
Tutaweza 
kuamsha ari ya kila mtanzania kuongeza bidii kwenye kazi akitumaini na 
kuamini kuwa kesho yake itakuwa bora kuliko jana yake, kuwa naye ataishi
 kwa heshima, raha na starehe ndani ya nyumba yake.
Ninaamini,
 kutokea ndani kabisa ya mifupa yangu, kuwa tukifanya uchaguzi sahihi wa
 vipaumbele vyetu, tukibadili namna tunavyoendesha serikali yetu, haya 
ninayoyasema si ndoto za mchana. Ni mambo yanayowezekana.
Watanzania
 wengi wanaamini, kuwa tukifanya uchaguzi sahihi wa vipaumbele vyetu, 
mabadiliko makubwa, na ya haraka yatatokea kwenye uchumi wetu. Wanaamini
 tukichagua kiongozi sahihi mwakani, anayejua mahitaji ya nchi yetu kwa 
sasa na baadaye, tutafanikiwa.
Nyote 
mliopo hapa na wanaotusikiliza kutokea nje ya hapa mna jukumu la 
kututazama kwa ukaribu sana, kututathmini na kutupima sote; 
tuliojitokeza hadharani, walioanza safari za matumaini, wanaotajwa 
tajwa, na wale wanaosubiri kuoteshwa ili wakati muafaka ukifika muwape 
taarifa sahihi watanzania, kuwa kati yetu sote, ni nani anafaa 
kutuongoza kuelekea Tanzania ya ndoto zetu!
Kuwa, ni 
nani kati yetu ataweza kuwa Amiri-jeshi-mkuu, siyo kwa uanajeshi wake 
bali kwa uwezo na utayari wake wa kuwashirikisha wataalamu wa majeshi na
 kuamua kwa busara kutumia nguvu za kijeshi pale inapolazimika baada ya 
kupima na kuchambua aina nyingine zote za kutafuta suluhu za migogoro 
kabla ya kuamua vita.
Kuwa, ni 
nani kati yetu anayeamini katika uhuru, haki na usawa na wajibu wa watu 
wote, kama unavyolindwa na Katiba, anayeamini katika haki ya kuabudu 
lakini asiyekuwa tayari kuitumia haki hiyo kuwagawa watanzania kutokana 
na dini zao.
Kuwa, ni 
nani kati yetu anayeamini katika Haki ya kupata huduma bora za afya, 
elimu, maji, kama wanavyopata wabunge na mawaziri wetu, kama wanavyopata
 mahakimu na majaji wetu, kama wanavyopata wafanyabiashara na 
wakurugenzi wetu.
Kuwa, ni 
nani kati yetu ataweza kuhakikisha kuwa watanzania wote wanapata haki 
hizi bila kutazama hali zao kiuchumi ama daraja zao kijamii.
Kuwa, ni 
nani kati yetu anaamini zaidi katika uhuru na kujitegemea kwenye masoko 
na malighafi ili kudhibiti uchumi wetu mpana wa ndani, kujitegemea 
kwenye masoko ya pamba na nguo, kwenye mafuta ya kula, kwenye chakula 
cha uhakika kwa ajili ya watu wetu, kwenye mafuta na gesi ili tukwepe 
mtego wa kuwa sehemu ya uchumi, masoko na biashara za hasara na faida za
 makampuni makubwa ya kimataifa nje ya mipaka yetu. 
Ili 
tulinde thamani ya fedha yetu, ili tuwe na uhakika wa ustawi wa maisha 
ya watu wetu ndani ya nchi bila athari kubwa kutoka nje ya nchi yetu.
Kuwa, ni 
nani miongoni mwetu anaakisi taswira sahihi zaidi ya watanzania walio 
wengi, historia yake, rekodi yake, wajihi wake, mtazamo wake, ndoto 
zake, zinaakisi ‘utanzania’ halisi. Kuwa, yeye ni hitaji sahihi la 
watanzania.
Wakati ukifika, muwaeleze watanzania ukweli, wafanye uamuzi unaotokana na taarifa sahihi, wachague mtu sahihi.
Mimi, Ndugu zangu, natangaza rasmi sasa, kuwa ninatia nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2015. 
Na 
nimefikia uamuzi huu bila kuelekezwa, kusukumwa, kushawishiwa, kupangiwa
 ama kupanga na mtu ama na kikundi cha watu, bali kwa utashi na utayari 
wangu. Na ninayasema haya, haswa baada ya kutafakari mambo mengi kwa 
kina:
 mahitaji
 ya sasa na baadaye ya Tanzania ya ndoto zangu, uwepo wa fursa ya 
kugombea na kushinda uchaguzi ujao, uwezo wangu wa kuchambua mambo, 
kutafakari, kufanya maamuzi sahihi, kuchukua hatua za utekelezaji na 
kusimamia utekelezaji, uadilifu na uzalendo wangu, na zaidi nia yangu ya
 kuwa sehemu ya watanzania wengi tunaotaka kuona mapinduzi ya kifikra 
katika nchi yetu – mapinduzi ambayo yatatia chachu ya mabadiliko ya 
namna tunavyochagua vipaumbele vyetu kama Taifa na namna tunavyosimamia 
utekelezaji wa mambo mazuri tunayojipangia kama Taifa.
Ninatangaza
 nia ya kugombea Urais nikiwapa fursa watanzania wanipime na kunitazama 
mwenendo na uwezo wangu, nikiamini kabisa nitapimwa na kuungwa mkono ama
 kutoungwa mkono si kwa rangi ya ngozi yangu, si kwa jinsi yangu, si kwa
 umri wangu, na wala si kwa daraja langu kwenye jamii, dini yangu, ama 
kabila langu. Ninaamini nitapimwa kwa sifa na uwezo wangu, kama 
mtanzania.
Watanzania
 tuna sifa moja kubwa; kwenye mambo ya msingi ya kitaifa, tunakubaliana 
kuwa maslahi ya Tanzania hupanda juu ya maslahi yetu binafsi. Tudumishe 
utanzania wetu.
Ninaamini
 katika Ndoto ya Tanzania. Kuwa leo miaka 50 ya kuwa Jamhuri ya Tanzania
 tuna kila sababu ya kuwa Taifa la dunia ya kwanza, viongozi 
waliotutangulia wameandaa misingi ya kuifikisha Tanzania kwenye 
matamanio yetu. Kizazi chetu cha kina jukumu na wajibu wa kuikimbiza 
Tanzania kufikia kwenye ahadi inayotokana na ndoto za wazee na waasisi 
wa Taifa letu. Binafsi, niko tayari kulibeba jukumu hilo bila woga wala 
wasiwasi, maana naamini tusipojitokeza watu kama mimi, tutajikuta 
tunaongozwa na watu wasiostahili. Nina suluhu ya changamoto kubwa za leo
 na kesho:
 kupigana
 na njaa na kuhakikisha usalama wa chakula kwa watu wetu, tatizo la 
ajira kwa vijana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi ni miongoni 
mwa mambo ambayo kizazi chetu kitapaswa kuyafanyia kazi kwa haraka na 
umakini wa hali ya juu.
Mimi 
ninaamini kwamba, kama hata mimi nimefika hapa, basi kila mtanzania 
anaweza, na ana haki ya kufika hapa na kwenda mbele zaidi yangu. 
Mafanikio siyo haki ya wachache, ni tunu ya Mwenyezimungu kwa kila mtu. 
Ninaamini ni haki ya kila mtanzania kuota ndoto yake, kuifanyia kazi na 
kuifikia. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina wajibu wa kutoa fursa kwa 
watu wake kuota ndoto zao na kufikia mafanikio bila kukwama.
Na ndugu 
watanzania wenzangu, amini nawaambia, kuwa, mbele yetu tuna kazi ya 
ziada ya kufanya. Kazi ambayo ninaamini tunaiweza tukiamua; uwezo tunao,
 sababu tunazo na nia tunayo – sema tuna mapungufu makubwa kwenye 
kuchukua hatua za kutenda.
Mimi naamini kwamba; E Pluribus unum. Baina ya wengi, mmoja! 
Kwamba; 
Mimi ni mmoja kati ya uwingi wetu. Siwezi kuwa salama kama wengine 
hawako salama, siwezi kuwa na raha kama wengine wanateseka. Ninaongozwa 
na ile dhana kwamba, matatizo ya mwenzangu, ni ya kwangu, na si yangu 
peke yangu, ni yetu sote kama jamii moja.
Hivyo:
- kitisho
 cha njaa ya familia fulani maskini kule Sakasaka, wilayani Meatu, ni 
kitisho changu na familia yangu, hata kama siyo familia yangu.
- Kucheleweshewa haki ya kuhukumiwa kwa mtuhumiwa wa mauaji ya kule Sombetini, ni kitisho kwangu pia, hata kama kesi siyo yangu.
- Mzee 
Makame wa kule Wete, Pemba, aliyefiwa na watoto wake akakosa msaada na 
yeye hana nguvu za kuzalisha tena, anavyokula mlo mmoja kwa siku ili 
asukume siku, inaniumiza na kunigusa moyoni, hata kama yeye siyo babu 
yangu.
- Mama 
John ni mpishi mzuri wa wali nazi kwa maharage, na ana wateja wengi 
mtaani kwake maeneo ya Mtaa wa Sikukuu, Sokoni Kariakoo; akifukuzwa, 
akapigwa virungu, akanyang’anywa pesa zake, akadhalilishwa na kumwagiwa 
chakula chake na mgambo wa jiji la Dar es salaam kwa kuwa anafanya 
biashara mahala pasiporuhusiwa, inaniumiza na kunigusa moyoni, hata kama
 yeye si mama yangu.
- Kama 
kuna mtoto asiyejua kusoma na kuandika kule Mrijo Chini kwa watani zangu
 warangi, hiyo inaniuma na kunigusa sana moyoni, hata kama yeye si 
mwanangu.
- Bwana 
Kalumanzila ni mmachinga nguo za mitumba mitaani. Yeye huchukua nguo 
zake kumi kwa kuaminiwa na mwenye belo kutokea soko la Karume, akiuza 
anachukua kifaida kidogo cha juu kinachozidi hapo juu na kurudisha pesa 
ya mwenye mali Karume jioni ya siku hiyo. Elfu mbili ama tatu anayopata 
inamfanya aishi yeye na mkewe na watoto wake. 
Akifukuzwa
 barabarani na akanyang’anywa mali, anakosa kazi ya kufanya na 
analazimika kumtumikia bosi mwenye mali mpaka atakapofidia mali 
iliyopotea bila kupata cha juu. Shida na madhila anayoyapata bwana 
Kalumanzila zinaniumiza na kunigusa sana moyoni, hata kama yeye si 
mjomba wangu.
Tarehe 4,
 Agosti 2014, Rais Kikwete akihutubia kwenye Kituo cha kimataifa cha 
maendeleo (Center for Global Development) alisema: “…Nataka na natamani 
kuwa Rais wa mwisho wa Tanzania kuongoza nchi masikini. 
Raslimali
 ya gesi inatoa nafasi na fursa kubwa kwa nchi yetu kuondokana na 
umasikini. Mimi nimeongoza nchi masikini, lakini nataka mrithi wangu 
kuongoza nchi yenye ustawi na utajiri…” Mimi nasema hivi: nataka na 
natamani kuwa Rais wa kwanza wa Tanzania kuongoza nchi Tajiri. Kama 
nitafanikiwa kuwa Rais, nitatumia miaka ya awali ya uongozi wangu 
kuikimbiza Tanzania kuelekea kwenye ndoto hii. 
Mungu awabariki. Mungu ibariki Tanzania. Mungu ibariki Afrika.
No comments:
Post a Comment