ZITTO: UBUNGE SASA BASI!
![]()  | 
| Zitto Kabwe | 
Na: Frank Sanga na Anthony Kayanda, Kigoma, MWANANCHI.
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe amesema hana mpango wa kugombea ubunge mwaka 2015 badala yake anajipanga kuwania urais. Zitto alisema hayo jana alipozungumza na wananchi katika mjadala ulioandaliwa na asasi ya kiraia ya Meza ya Duara uliokuwa unafanyika maeneo ya Soko la Mwanga, mjini Kigoma. Zaidi ya watu 200, ambao walihudhuria katika mjadala huo wa wazi walimuuliza maswali mbalimbali mbunge huyo, huku mmoja akigusia kuhusu tetesi za mara kwamba Zitto anataka kugombea urais katika uchaguzi ujao.
 “Nimefanya
 kazi kubwa katika kazi yangu ya ubunge, nimeleta mabadiliko mengi 
kuanzia bungeni  mpaka jimboni. Nadhani inatosha na hata nikiongezewa 
miaka mingine sitaweza kufanya yale yaliyonishinda katika kipindi cha 
miaka kumi.
 
“Kama Mungu ataniweka mpaka mwaka 2015, sitagombea ubunge tena kwa 
sababu kazi niliyofanya inatosha. Natangaza rasmi kuwa nitagombea urais 
kupitia chama changu cha Chadema, bila kusababisha msuguano wowote na 
sitaki kuingia katika historia ya kurudisha nyuma harakati za upinzani 
kushika dola,” alisema Zitto.
 “Nataka
 kuleta changamoto mpya, nitawaeleza watu wa chama changu nia hiyo na 
nitatoa hoja za msingi. Hata kama sitapata ridhaa yao, lakini huo ndio 
msimamo wangu.
 
“Iwapo chama kikiona sistahili au sifai, nitakubaliana na uamuzi huo. 
Watu wengi wanadhani urais ni cheo, hawajui kuwa ni nafasi ambayo 
inakufanya ufanye vitu ambavyo ni vikubwa na vya maendeleo kwa 
wananchi.”
 
Atangaza kugombea urais
Katika hatua nyingine Zitto alisema ana mpango wa kuwania urais kupitia 
Chadema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
 
“Kwanza nataka niwahakikishia watu wa Kigoma msiwe wanyonge…mna uwezo wa
 kutoa rais wa nchi hii,” Zitto alianza kujibu swali hilo na kuendelea. 
Hata
 hivyo Zitto alipoulizwa baadaye na Mwananchi kuwa mwaka 2015 atakuwa na
 miaka 39, hivyo kukosa sifa ya kugombea urais kwa mujibu wa katiba 
alijibu; “Nadhani nina uwezo wa kuwa rais, sidhani kama Katiba inaweza 
kumzuia mtu mwenye uwezo asigombee na ndio maana ninaamini kuwa 
kipengele cha kuwa na miaka 40 kitabadilishwa katika katiba mpya.”
 “Nchi
 za Kidemokrasia lazima vyama vibadilishane utawala wa kuongoza nchi  
kama ilivyo katika nchi za Ghana na Zambia. Tanzania inatakiwa kuiga 
mfano wa nchi hizo,” alisema Zitto
 
Katika kukazia hilo, Zitto alisema anashangazwa na umaskini uliopo 
Tanzania wakati mwaka 1976 uchumi wake ulikuwa sawa na nchi ya Malaysia,
 lakini mpaka kufikia mwaka 2001, Malaysia ilipunguza idadi ya watu 
wanaoishi chini ya dola moja kutoka asilimia 56 mpaka kufikia asilimia 
tatu huku Tanzania ikipunguza kutoka  51 mpaka 46.
 
Katika hatua nyingine, Zitto alikana kuwa, Chadema ni chama cha udini, 
ukanda, ukabila  ila akasisitiza kuwa ni chama cha kitaifa. 
 “Ndugu
 zangu naomba mnielewe, Chadema si chama cha ukabila, ukanda wala udini 
bali ni chama cha kitaifa. Hizo ni propaganda za wapinzani wetu,” 
alisema Zitto baada ya kuulizwa na mmoja wa washiriki kuhusu tuhuma za 
chama hicho kuwa cha Kikanda.
 “CCM
 imewahi kudai CUF ni chama cha Waislamu, na sasa wanasema Chadema ni 
chama cha Wakristo, sasa wao CCM ni chama cha wapagani au cha watu 
gani?” Alihoji Zitto.
 
Alisema ili kuthibitisha kuwa Chadema si chama cha Kikanda, matokeo ya 
urais wa mwaka 2010, Dk Wilbroad Slaa aliongoza dhidi ya wagombea urais 
wengine kwa kupata kura nyingi katika Jimbo la Manyovu mkoani Kigoma na 
hivyo kufanya kupata asilimia nyingi kuliko sehemu yoyote Tanzania. 
Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/habari

No comments:
Post a Comment