NYALANDU AKARIBISHA WAFANYABIASHARA WA SAUDI ARABIA KUWEKEZA SEKTA YA UTALII NCHINI
Waziri wa
 Maliasili na Utalii Mhe. Lazaro Nyalandu (wa pili kushoto) akimsikiliza
 kwa makini Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara ya Saudi Arabia Dk. 
Abdulrahman Al-Zamil (wa tatu kushoto) jijini Riyadh, Saudi Arabia. 
Wengine katika picha kutoka kulia ni Mshauri wa Ushirikiano wa Kimataifa
 wa Mamlaka ya Wanyamapori ya Saudia Mohammad Sulayem; Katibu Mkuu wa 
Maliasili na Utalii Dk. Adelhelm Meru na Balozi wa Tanzania nchini Saudi
 Arabia Prof. Abdillah Omari.
Waziri wa
 Maliasili na Utalii Mhe. Lazaro Nyalandu (kushoto) katika mazungumzo na
 Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara ya Saudi Arabia Dk. Abdulrahman 
Al-Zamil jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Mwenyekiti
 wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira Mhe. 
James Lembeli (kushoto) akikaribishwa na Mwenyekiti wa Chemba ya 
Biashara ya Saudia Dk. Abdulrahman Al-Zamil jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Waziri 
Kivuli wa Maliasili na Utalii Mhe. Peter Msigwa (kushoto) akikaribishwa 
na Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara ya Saudia Dk. Abdulrahman Al-Zamil 
jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Ujumbe wa
 Serikali ya Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. 
Lazaro Nyalandu (wa tano kushoto) ukiwa katika picha ya pamoja na 
Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara ya Saudia Dk. Abdulrahman Al- Zamil (wa
 sita kushoto) mara baada ya kumalizika kwa mazungumzo baina ya pande 
mbili jijini Riyadh, Saudi Arabia. Wengine pichani kutoka kushoto ni 
pamoja na Mkurugenzi wa Wanyamapori Herman Keraryo; Mkurugenzi Mkuu 
TANAPA Allan Kijazi; Mhe James Lembeli; Mhe Peter Msigwa; Katibu Mkuu 
Maliasili na Utalii Dk. Adelhelm Meru pamoja na maafisa kutoka Chemba ya
 Biashara ya Saudia.
Waziri wa
 Maliasili na Utalii Mhe. Lazaro Nyalandu amewakaribisha wafanyabiashara
 kutoka Saudi Arabia kuwekeza katika sekta ya utalii nchini ambayo ina 
fursa nyingi za uwekezaji. Nyalandu alitoa wito huo kufuatia mazungumzo 
yake na Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Saudi Arabia Dk. 
Abdulrahman Al-Zamil yaliyofanyika Riyadh, Saudi Arabia jana.
Waziri 
Nyalandu ambaye anaongoza ujumbe wa Wizara ya Maliasili na Utalii nchini
 Saudia alibainisha kuwa mazingira ya uwekezaji nchini yanavutia na 
kutaja maeneo hayo kuwa ni pamoja na ujenzi wa hoteli na loji za kisasa 
zitakazoweza kuvutia watalii wengi zaidi katika maeneo ya mijini pamoja 
na ndani ya maeneo ya uhifadhi.
Alisema 
kuwa utalii wa Tanzania unakua kwa kasi nzuri kutokana jitihada 
zinazofanywa na serikali pamoja na wadau mbalimbali katika kutangaza 
vivutio vya utalii na kuwa juhudi hizo lazima ziende sambamba na 
upatikanaji wa huduma bora za malazi. "Upatikanaji wa huduma nzuri za 
malazi ya bei nafuu utasaidia kuvutia watalii wengi zaidi nchini na kwa 
maana hiyo tunawakaribisha kuja kuzitumia fursa zilizopo ili kuweza 
kukuza uchumi wa nchi yetu", alisema Nyalandu.
Waziri 
Nyalandu ambaye anaongoza ujumbe wa Wizara ya Maliasili na Utalii nchini
 Saudia, alisema kuwa Tanzania ni ya pili ulimwenguni baada ya Brazil 
kwa kuwa na vivutio vizuri vya asili vya utalii na kuwa rasilimali hizi 
zinapaswa sasa kutumiwa vema ili kuinua uchumi na njia pekee ni pamoja 
na kuvutia wawekezaji na mitaji kutoka Saudia ili kufikia azma hiyo.
Kwa 
upande wake Dk. Al-Zamil aliahidi kuwashirikisha wafanyabiashara wenzake
 kutikia wito huo na kwa kuanzia timu ya wafanyabiashara pamoja na 
mawakala wa utalii watafika nchini katika siku chache zijazo ili kuona 
namna gani wataweza kuzitumia fursa zilizopo kikamilifu. Aidha, katika 
eneo la utalii Al- Zamil alisema kuwa Chemba yake itafanya kila 
liwezekanalo kubadilisha mtazamo wa Wasaudia wanaotembelea kwa wingi 
maeneo mbalimbali ya utalii duniani ili waweze kuitembelea Tanzania na 
kujionea vivutio mbalimbali vya utalii vinavyopatikana nchini.
Aidha, 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dk. Adelhelm Meru alisema 
kuwa serikali itaandaa Kongamano Maalum la Uwekezaji nchini Saudi Arabia
 ili kuweza kutangaza fursa mbalimbali zzilizopo nchini ambazo 
zikitumika vema zinaweza kuinua uchumi wa taifa.
Hivi sasa
 Tanzania inategemea idadi kubwa ya watalii kutoka Mataifa ya Ulaya na 
Amerika na kwamba japokuwa idadi ya watalii kutoka nchi za kiarabu 
haizidi 15,000 kwa mwaka, bado jitihada za utangazaji na uwekezaji 
zikifanywa vizuri idadi ya watalii kutoka mataifa ya kiarabu itaweza 
kuongezeka nchini.
Ujumbe wa
 Tanzania unajumuisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dk. 
Adelhelm Meru; Balozi wa Tanzania Saudi Arabia Prof. Abdillah Omari; 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira
 Mhe. James Lembeli, Waziri kivuli wa Maliasili na Utalii Mhe. Mchingaji
 Peter Msigwa; Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa Allan Kijazi pamoja 
na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori Herman Keraryo.
No comments:
Post a Comment