Dar es 
Salaam. Wakati wananchi wakisubiri vigogo wa serikalini na mawaziri 
wanaotuhumiwa kuhusika kwenye kashfa ya uchotaji fedha kwenye Akaunti ya
 Tegeta Escrow kufikishwa mbele ya vyombo vya umma, ni watumishi watano 
tu wa umma waliofikishwa mahakamani, lakini Mkurugenzi wa Takukuru, Dk 
Edward Hoseah ana jibu la suala hilo; kazi yao ni kufikisha mahakamani 
'vidagaa'.
Katika 
kashfa hiyo ya Sh306 bilioni, mawaziri wa sasa na zamani pamoja na 
makatibu wakuu wa wizara, wanatuhumiwa kwa njia moja au nyingine 
kuhusika kwenye kufanikisha kwa makusudi au uzembe uchotwaji wa fedha 
hizo, kuikosesha mapato Serikali na kupokea mgawo wa fedha hizo, lakini 
hadi sasa ni watumishi wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Wizara ya Nishati na 
Madini, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Tanesco na Benki Kuu 
(BoT) pekee waliofikishwa mahakamani.
 
            
Wote 
watano, ambao ni vigogo kwenye taasisi zao, wameshtakiwa kwa kosa la 
kuomba na kupokea rushwa ili kufanikisha mkakati huo ulioibuliwa na 
gazeti la The Citizen na baadaye Bunge kulidaka na kufikia maazimio ya 
kutaka wahusika wote wawajibishwe na mamlaka zinazowahusu.
Juzi, 
mkurugenzi huyo wa Takukuru aliliambia gazeti hili kuwa taasisi yake 
itaendelea kuchunguza watu wote waliohusika katika kashfa ya escrow bila
 ya ubaguzi, lakini akabainisha kuwa kazi ya kuwapeleka mahakamani 
mawaziri na vigogo inatakiwa ifanywe na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka 
(DPP).
Dk 
Hoseah, ambaye aliwahi kuingia kwenye mzozo wa DPP wa zamani kutokana na
 madai yake kuwa mafaili mengi ya kesi za rushwa hayafanyiwi kazi, 
alisema sheria haiwaruhusu kuwapeleka mahakamani mawaziri iwapo 
watabainika kuhusika kwenye vitendo vya rushwa.
Kwa 
mujibu wa kifungu cha 57 cha Sheria Namba 11 ya Kuzuia na Kupambana na 
Rushwa ya Mwaka 2007, endapo vigogo na mawaziri watabainika kuhusishwa 
na vitendo vya rushwa, jalada la uchunguzi wao litakabidhiwa kwa DPP ili
 achukue hatua ya kuwapeleka mahakamani.
Dk Hoseah
 alisema kwa sasa Takukuru inaendelea na uchunguzi wake mpaka 
itakapojihakikishia ushahidi wa kutosha dhidi ya vigogo hao.
"Bunge 
lilitoa maazimio yake na likaagiza kuchukuliwa hatua...Takukuru 
tulishaanza na tunaendelea na uchunguzi. Taratibu zote zikishakamilika 
kisha ushahidi ukapatikana kwa vielelezo vyote, basi watafikishwa 
mahakamani wala hakuna tatizo lolote," alisema.
"Lakini 
watafikishwa mahakamani baada ya sisi kuwasilisha jalada letu la 
uchunguzi kwa DPP ambaye ndiye mamlaka ya kuwafikisha mahakamani kama 
sheria inavyotuagiza."
Udhaifu 
huo wa sheria pia ulizungumziwa na Bunge wakati wa kujadili kashfa ya 
escrow na kuazimia kuwa sheria inayounda Takukuru ifanyiwe kazi ili iwe 
na mamlaka hayo ya kufikisha mahakamani vigogo wa rushwa kubwa.
Waliohusishwa na rushwa
Mawaziri 
waliotajwa kwenye sakata hilo ni Profesa Anna Tibaijuka, ambaye alikuwa 
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na ambaye aliingiziwa 
Sh1.6 bilioni na mwanahisa wa zamani wa Kampuni ya IPTL, James 
Rugemarila. Tibaijuka alivuliwa wadhifa huo kutokana na sakata 
hilo.Wengine ni Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, 
ambaye Rais Jakaya Kikwete alisema amemuweka kiporo baada ya Bunge 
kumuona kuwa hakushughulikia vizuri suala hilo na kuisababishia Serikali
 kukosa mapato.
Wengine 
ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti na ambaye alikuwa Mwanasheria
 Mkuu, Andrew Chenge, ambaye aliingiziwa pia Sh1.6 bilioni kwenye 
akaunti yake na Rugemarila; waziri wa zamani wa Nishati na Madini, 
William Ngeleja, aliyeingiziwa Sh40.4 milioni; aliyewahi kuwa Waziri wa 
Nishati na Madini, Daniel Yona (Sh40.4 milioni), mbunge wa zamani wa 
Sumbawanga (CCM), Paul Kimiti (Sh40.4 milioni) na aliyekuwa mjumbe wa 
Bodi ya Tanesco, Dk Enos Bukuku (Sh161.7 milioni).
Vigogo 
waliotajwa kwenye sakata hilo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na 
Madini, Eliackim Maswi, ambaye amesimamishwa, Fredrick Werema, ambaye 
alijiuzulu kwa maelezo kuwa ushauri wake kuhusu suala la kodi kwenye 
fedha hizo haukueleweka na ulisababisha tafrani.
Awali, Dk
 Hoseah aliliambia gazeti dada la The Citizen kwamba katika uchunguzi 
wake, hakuna kiongozi wala kigogo yeyote ambaye atapona.
"Yeyote 
yule ambaye atabainika katika uchunguzi wetu, lazima afikishwe mbele ya 
sheria, hakuna kigogo wala kiongozi yeyote ataweza kukwepa endapo 
ushahidi utaonekana wazi," alisema.
Alipoulizwa
 kama uchunguzi huo unamjumuisha Profesa Tibaijuka, mkurugenzi huyo 
alisema hawezi kutaja jina la mtu kwa kuwa ni kinyume cha sheria kutaja 
jina au taarifa ambazo ziko kwenye uchunguzi."
Waliofikishwa
 mahakama ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu hadi sasa ni Mhandisi Mkuu 
wa Mradi wa Umeme Vijijini (Rea), Theophillo Bwakea na Mkurugenzi wa 
Huduma za Kisheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, 
Rugonzibwa Mujunangoma, ambao kwa pamoja wanadaiwa kupokea rushwa ya 
Sh485.1 milioni.
Wengine 
ni Meneja Misamaha ya Kodi wa TRA, Kyabukoba Leonard Mutabingwa, 
Mwanasheria Mwandamizi wa Tanesco, Steven Roman Urassa na Mkurugenzi wa 
Fedha BoT, Julius Rutta Angello wanaokabiliwa na mashtaka ya kuomba na 
kupokea rushwa ya jumla ya Sh1.923 bilioni.
Maoni ya wasomi
Akizungumzia
 suala hilo, Profesa Gaudence Mpangalla kutoka Chuo Kikuu cha Ruaha 
alihoji sababu za Serikali kushindwa kuchukua hatua za haraka kuijengea 
uwezo Takukuru ili iweze kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wa aina hiyo.
"Kama 
tunavyoona hivi sasa inawapandisha kizimbani watumishi wengine, sasa 
kuna tofauti gani na waziri atakayebainika kukutwa na kosa kama hilo? 
Sioni tofauti yoyote kwa wakosaji hao," alisema.
"Udhaifu 
huo unaweza kujenga imani kwamba Serikali inawabeba mafisadi kwa mgongo 
wa ofisi ya DPP kwa sababu mashtaka mengi hayafanyiwi kazi katika ofisi 
hiyo."Mara kadhaa Dk Hoseah amekuwa akitoa kauli zinazoonyesha kuwa 
ameshawasilisha majalada mengi ofisi ya DPP, lakini amekuwa akiyakalia 
au kuyarudisha kutaka uchunguzi ukamilike.
Hata hivyo, Profesa Chris Maina wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), anaona hilo halitafanyika kwa hivi sasa.
"Kwa 
jinsi sakata hilo lilivyoibuliwa na ushahidi kuwekwa wazi na Rais 
akaonyesha hisia zake, lazima DPP ajaribu kuwa makini sana na mawaziri 
au vigogo watakaofikishwa mbele yake," alisema.
"Inamlazimu
 achukue hatua za haraka. Hili suala siyo sawa na mashtaka mengine... 
lakini tusubiri kwa sababu ni kiongozi mpya aliyeingia ofisi hiyo 
hatujui itakuwaje."
CHANZO:MWANANCHI