IPTL yazua Kizaazaa Mahakamani 
            
Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya IPTL na PAP, Harbinder Singh Sethi
Kampuni 
za Pan Africa Power Solution Tanzania Limited (PAP) na Independent Power
 Tanzania Ltd (IPTL), zimewasilisha maombi ya kutaka Kamishna Mkuu wa 
Mamlaka ya Mapato (TRA) akamatwe kwa kukiuka amri ya Bodi ya Rufaa za 
Kodi (TRAB) kwa kufuta Hati za Malipo ya Kodi za Mauzo ya Hisa (Capital 
Gain Certificate).
Kampuni 
hizo mbili, ambazo ziko kwenye mgogoro wa umiliki, ndizo zinahusika 
kwenye sakata la uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta 
Escrow iliyofunguliwa kuhifadhi fedha za malipo ya tozo ya kuuza umeme 
unaofuliwa na IPTL, kwa Shirika la Umeme (Tanesco), wakati wa kusubiri 
uamuzi wa mahakama katika kesi ya kupinga tozo hilo.
PAP, 
ambayo inadai imenunua hisa zote za IPTL, ndiyo iliyolipwa fedha zote 
zilizokuwa kwenye akaunti hiyo na kuamsha mjadala mkubwa bungeni 
ulioisha kwa Bunge kufikia uamuzi wa kuwawajibisha kisheria wote 
waliohusika, wakiwemo mawaziri.
Lakini 
uamuzi huo wa Bunge haukuwa tamati la sakata hilo baada ya kampuni hizo 
mbili kukata rufaa TRAB dhidi ya Kamishna wa TRA na Msajili wa Kampuni 
na Leseni (Brela) zikipinga kusudio la kufuta hati hizo.(P.T)
 
Jana 
kampuni hizo mbili ziliwasilisha maombi ya hati ya kutaka Kamishna Mkuu 
wa TRA akamatwe, zikidai kuwa amepuuza amri hiyo iliyomzuia kutekeleza 
azma yake ya kufuta Hati za Malipo ya Kodi ya Mauzo ya Hisa.
Katika 
maombi hayo walalamikaji hao wanadai kuwa licha ya TRAB kutoa zuio hilo 
Novemba 26, 2014, Kamishna Mkuu wa TRA, ambaye ni mlalamikiwa wa kwanza,
 alitoa amri ya kuziondoa hati hizo siku iliyofuata, yaani Novemba 27, 
2014, bila kujali amri hiyo.
Walalamikaji
 hao pia wanaiomba TRAB, baada ya kumkamata Kamishna Mkuu wa TRA, itoe 
amri afungwe kwa kudharau amri halali iliyotolewa na bodi na pia 
imwamuru akidhi matakwa ya amri ya TRAB ya Novemba 26.
Pia 
walalamikaji hao wanaiomba TRAB imwamuru mlalamikiwa huyo, kulipa 
gharama za uendeshaji wa shauri hilo pamoja na amri nyingine ambazo 
itaona kuwa zinafaa.
Maombi 
hayo ya PAP na IPTL ya hati ya kumkamata na kuamuru Kamishna Mkuu wa TRA
 afungwe yamepangwa kusikilizwa leo na Katibu wa TRAB, Respicius 
Mwijage.
Hati ya 
kiapo inayounga mkono maombi hayo inaeleza kuwa mlalamikiwa, akiwa ni 
raia wa Tanzania, siyo tu kwamba alipaswa kuwa mtiifu kwa mamlaka ya 
bodi hiyo, bali pia alipaswa kutekeleza sheria za nchi ambazo bodi hiyo 
ni sehemu yake.
Hati hiyo
 ya kiapo ya mkurugenzi wa operesheni wa IPTL, Parthiban Chandrasakaran,
 inaeleza kuwa kwa kitendo hicho cha kutotii amri ya bodi hiyo, 
mlalamikiwa amepoteza sifa ya kuwa mtumishi wa umma katika Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania.
Pia 
inaelea kuwa kama bodi hiyo isipotumia mamlaka yake kukubali maombi hayo
 ya kutoa amri inayoombwa, basi walalamikaji watapata hasara isiyoweza 
kufidiwa.