TIFFAN ENT

TIFFAN ENT

TUKO WANGAPI

TUKO WANGAPI

GLORY FREIGHT

GLORY FREIGHT

Thursday, December 19, 2013

KAGAME ASHTUSHA MSIBA WA MANDELA 

 paul20kagame1 42102

*Alitua ghafla na kwenda kumuaga Mandela
*Aondoka bila kumpa mkono wa pole Rais Zuma
KATIKA hali isiyotarajiwa, Rais Paul Kagame wa Rwanda Jumatano iliyopita aliwashangaza wengi baada ya kufika ghafla jijini Pretoria, Afrika Kusini na kuaga mwili Mzee Nelson Mandela na kuondoka mara moja. (HM)

Pamoja na kuwasili ghafla bila taarifa Pretoria, Kagame alikwenda moja kwa moja katika majengo ya Union Buildings na kwenda kuaga mwili huo kisha alielekea uwanja wa ndege na kuondoka.
Aliondoka saa chache baada ya kuuaga mwili wa shujaa Mandela na kuelekea Rwanda ambako alikwenda kuongoza Mkutano Mkuu wa chama tawala cha Rwanda Patriotic Front (RPF), ambapo alichaguliwa kuwa Mwenyekiti.
Habari za ndani zimesema kuwa Kagame ambaye alikuwa na ulinzi mkali, aligoma kwenda kusalimiana na mwenyeji wake Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini.
Kuja ghafla kwa Kagame na Rais Omar al Bashir wa Sudan katika kumuaga Mandela kulizua maswali mengi, kwa vile Rwanda ilitangaza kuwa Rais Kagame hatahudhuria mazishi hayo na badala yake itatuma ujumbe wa viongozi wa juu wa nchi hiyo nchini Afrika Kusini.
Serikali ya Afrika Kusini awali ilitangaza kuwa Waziri Mkuu wa Rwanda, Pierre Habumuremyi, Katibu Mkuu wa RPF Francois Ngarambe, ndio wangeongoza ujumbe wa nchi hiyo katika mazishi hayo.
Clyson Monyela, Naibu Mkurugenzi Mkuu na Msemaji wa Wizara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Mahusiano alisema kuwa Serikali awali ilipokea jina la Waziri Mkuu na Katibu Mkuu wa RPF, lakini baadaye waliambiwa kuwa Kagame amewasili mwenyewe na ujumbe wa watu wachache.
Monyela alisema walipokea orodha ya maraisi wengi wa Afrika wakiwamo kutoka Kenya, Uganda, Congo DRC na Burundi lakini hawakupokea jina la Kagame ingawa alitokea ghafla na wala hakwenda kumpa pole Zuma, ila alituma ujumbe kwa Rais Zuma na wananchi wa Afrika Kusini.
"Hatukupokea jina la Rais Kagame kwa vile Serikali ya Afrika Kusini haina tabia ya kumualika mtu kwenye msiba wala mazishi, hiyo ni tabia ya wananchi wa nchi hii," alisema.
Msemaji huyo alisema kuwa hakuna hata Rais au kiongozi yoyote aliyealikwa katika msiba na mazishi hayo, na ilikua ni utashi wa kiongozi kuthibitisha kuwa atahudhuria.
Rais Kagame katika muda wa hivi karibu amekuwa na ugomvi wa chini chini na maraisi Zuma, Kikwete na Banda kutokana nchi hizo wanachama wa jumuiya ya nchi zilizoko kusini mwa Afrika (SADC) kupeleka askari wao nchini Congo kuwaondoa waasisi wa kikundi cha M23 wanaosaidiwa na nchi za Uganda na Rwanda.
Naibu Mkurugenzi huyo wa habari aliongeza kuwa Kagame alikwenda katika majengo ya Makao Makuu ya nchi hiyo na alisalimiana na Mchungaji Jesse Jackson wa Marekani.
"Siwezi kujua walizungumza nini lakini walikutana, wakakumbatiana na kuzungumza, ila kwenye misa ya kitaifa ya kumuombea Mandela pale katika viwanja vya FNB hakuhudhuria," alisema Monyela.
Hata hivyo, taarifa ndani zimedai kuwa mke wa Rais Kagame aligoma kuhudhuria mazishi hayo na kuaga mwili huo kutokana na kutoridhishwa na uhusiano wa nchi ya Rwanda na Afrika Kusini.
Kuna taarifa kuwa kulikua na kutokuelewana katia ya Rais Kagame na familia yake kutokana na nia yake ya kuhudhuria mazishi hayo.
Hata hivyo Serikali ya Rwanda kama zilivyo nchini nyingine duniani zilishusha bendera yake nusu mlingoti kuomboleza kifo cha Mandela.
Mandela alifariki Alhamisi wiki iliyopita baada ya kuugua kwa muda mrefu na viongozi wengi duniani akiwamo raisi wa Marekani Barack Obama walihudhuria ibada maalumu na kuaga mwili wake.
Hata hivyo Kagame aliandika barua kwa familia ya Mandela na ilikabidhiwa familia hiyo na balozi wa Rwanda nchini humo.
Wakati marehemu Mandela alipochaguliwa kuwa Rais wa kwanza mwafrika nchini Afrika Kusini mwaka 1994, Rwanda ilikua katika machafuko ya mauaji ya wenye kwa wenye kati ya Wahutu na watusi. Chanzo: Mtanzania

No comments:

Post a Comment