MAKARANI 800 WAGOMA KULA KIAPO CHA SENSA
MAANDALIZI
 ya Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti 26, mwaka huu
 yameingia dosari baada ya matukio kadhaa ya kukwamisha kazi hiyo 
kujitokeza katika mikoa mbalimbali, ukiwamo Dar es Salaam ambako zaidi 
ya makarani 800 wamegoma kula kiapo cha utii na kutunza siri.
Habari
 zilizopatikana jana zimeeleza kuwa mbali na makarani hao, vipeperushi 
vyenye ujumbe wa kutaka watu wagomee Sensa vimesambazwa mkoani Arusha, 
huku mkoani Tanga kukiwa na tukio la Sheikh mmoja kutiwa mbaroni kwa 
kusambaza vipeperushi vya aina hiyo.
Makarani
 hao waligoma jana ikiwa ni siku yao ya mwisho ya mafunzo ya kazi ya 
kuhesabu watu na makazi. Makarani hao kutoka vituo mbalimbali 
kulikotolewa mafunzo hayo, walisema wameamua kugomea kiapo hicho 
kutokana na fedha zilizotengwa kwa ajili ya malipo ya kazi hiyo 
kuchakachuliwa kinyume na makubaliano.
Baadhi
 ya vituo ambavyo makarani wake wamegoma ni  Shule ya Sekondari 
Makumbusho, Kambangwa, Shule ya Msingi Zawadi na vituo kadhaa vilivyopo 
maeneo ya Buguruni na Kawe.Baadhi ya makarani hao walionekana wakiwa 
katika makundi, muda ambao walipaswa kuendelea na mafunzo yao kabla ya 
kula kiapo cha kushiriki Sensa kwa uaminifu na ukamilifu.Baadhi ya 
makarani ambao waliomba majina yao yasitajwe gazetini, walisema imekiuka
 makubaliano ya awali.
“Serikali
 imesema imetenga Sh141 bilioni kwa ajili ya Sensa. Sisi tayari 
tuliingia makubaliano nayo kwamba tunatakiwa kulipwa Sh35,000 kwa siku, 
kwa muda wa siku saba jambo ambalo limegeuka na kuwa kinyume.”
“Ukipiga
 mahesabu fedha ambazo tungetakiwa kulipwa kwa siku hizo saba ni 
Sh245,000 lakini wao wamekuja hapa na kutupa Sh140, 000 tu. Hatuwezi 
kuendelea na kazi mpaka tulipwe fedha zetu.”
Karani
 mmoja katika Kituo cha Sekondari ya Kambangwa, alisema wameamua kugomea
 kiapo baada ya kuona kuwa mpaka mafunzo yanahitimishwa jana, baadhi yao
 hawajalipwa chochote.
RC Dar:Watalipwa
Akizungumzia
 madai ya makarani hao, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki 
alisema mpaka jana mchana makarani wote walipaswa kulipwa awamu ya pili 
ya fedha zao. Alisema awamu ya kwanza ya malipo hayo ilifanywa katika 
siku tano za mwanzo.“Kuna watu wamejichomeka katika zoezi hili, lakini 
kama kweli karani ameteuliwa lazima atalipwa pesa zake na kama imetokea 
amesahaulika basi afanye mawasiliano na mratibu wa Sensa wilaya 
anayotoka ili alipwe,” alisema.
Sheikh mbaroni
Katika
 hatua nyingine Sheikh Juma Koosa (52) anashikiliwa na polisi wilayani 
Morogoro akituhumiwa kutumia kipaza sauti kuwatangazia wananchi 
wasishiriki Sensa.
Sheikh
 huyo ambaye pia ni mwanafunzi wa mwaka wa pili wa Chuo Kikuu cha 
Kiislamu Morogoro, alikamatwa Agosti 19 mwaka huu alipokuwa kwenye 
Msikiti wa Miembeni, Mazinde mara baada ya kukaribishwa na wenyeji wake 
kuzungumza.Imedaiwa kuwa Koosa alitoa kitabu chenye kueleza sababu za 
kuwakataza Waislamu kutokushiriki Sensa mwaka huu.