CHADEMA KUMPINGA ZITTO MAHAKAMA YA RUFANI
Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), kiko katika harakati za kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu, Kanda
ya Dar es Salaam, uliompa ushindi aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama
hicho Zitto Kabwe. (HM)
Zitto ambaye pia ni Mbuinge wa Kigoma
Kaskazini, juzi aliibuka mshindi katika maombi yake ya kuizuia Kamati
Kuu (CC) ya chama hicho kumjadili na au kuchukua uamuzi wowote kuhusu
uanachama wake, hadi kesi ya msingi kuhusu suala hilo itakapokuwa
imesikilizwa.
Kadhalika, chama hicho kupitia kwa
Mkurugenzi wake wa Mawasiliano na Uenezi, John Mnyika kimesema
kinaendelea na utekelezaji wa uamuzi wa Kamati Kuu wa kutompa Zitto
ushirikiano wa aina yoyote.
Wakili wa Chadema, Peter Kibatala,
alisema jana kuwa japo wanauheshimu uamuzi wa Mahakama, hawajaridhika
nao na kwamba wanakusudia kwenda Mahakama ya Rufani kuupinga.
"Ingawa uamuzi huu ni Interlocutory
(uamuzi usiomaliza kesi), lakini sisi hatukuridhika nao. Hatukuridhika
na uamuzi wa kutupilia pingamizi letu la awali, hati ya kiapo na hata
amri yenyewe ya zuio la muda," alisema Wakili Kibatala na kuongeza:
"Kuna namna nyingi za kufanya kupinga
uamuzi huo, kama vile kukata rufaa, kuomba marejeo au namna nyinginezo.
Kwa hiyo kwa sasa tunaangalia namna bora ya kwenda Mahakama ya Rufani
bila kuathiri matakwa ya kisheria."
Wakili Kibatala ambaye pia ni Makamu
wa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), alisema kuna haja ya
kuiomba Mahakama ya Rufani kuuchunguza uamuzi huo kwa kuwa una athari si
kwa Chadema tu, bali hata vyama vingine dhidi ya wanachama wake.
Kauli ya Mnyika
Mnyika kwa upande wake alisema kutompa
ushirikiano Zitto ni uamuzi wa Kamati Kuu ambao ulitokana na hatua yake
ya kwenda mahakamani kwa masuala ya chama, kinyume cha matakwa ya
Katiba ya Chadema na Kanuni zake.
Mnyika alikuwa akirejea taarifa
iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, baada ya kikao
hicho akiwataka viongozi wa ngazi zote za chama hicho, wanachama,
mashabiki na wapenzi wake, kutoshiriki wala kusaidia kwa namna yoyote
mikutano yote ya nje, ndani au shughuli nyingine yoyote ya kisiasa
itakayofanywa na Zitto na mawakala wake.
Ushindi wa Zitto
Katika maombi hayo namba 1 ya 2014,
Zitto kupitia kwa Wakili Albert Msando, Zitto aliiomba Mahakama itoe
zuio hilo la muda kwa CC ya Chadema, hadi kesi yake ya msingi namba 1 ya
2014 aliyoifungua mahakamani hapo itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Awali, mawakili wa Chadema,
Mwanasheria Mkuu wa chama hicho, Tundu Lissu na Kibatala walipinga
maombi hayo wakidai kuwa hayajakidhi matakwa ya kupewa zuio la muda.
Katika uamuzi wake juzi, Jaji John
Utamwa alikubaliana na hoja za Wakili Msando kuwa maombi hayo yametimiza
matakwa yote ya kupewa zuio hilo.
Maombi hayo ya Zitto yaliyotolewa
uamuzi juzi yalitokana na kesi ya msingi aliyofungua mahakamani hapo
Januari 2, 2014, dhidi ya Bodi ya Wadhamini wa Chadema na Katibu Mkuu wa
Chadema.
Katika kesi hiyo anaiomba mahakama
ikizuie chama hicho, wakala wake na vyombo vyake vya uamuzi kumchukulia
hatua zozote au kumjadili kuhusiana na uanachama wake, hadi hapo rufaa
anayokusudia kuikata Baraza Kuu la chama hicho kupinga kuvuliwa
nyadhifa, itakaposikilizwa.
Pia aliiomba Mahakama Kuu imwamuru
Katibu Mkuu wa Chadema ampatie mwenendo na taarifa za CC za kumvua
nyadhifa zake zote alizokuwa nazo ndani ya chama na iwazuie walalamikiwa
kumwingilia katika utekelezaji wa majukumu yake kama Mbunge wa Kigoma
Kaskazini. Kesi hiyo ya msingi imepangwa kutajwa mahakamani hapo
Februari 13, mwaka huu. Chanzo: Mwananchi